Mkuu wa mkoa wa Arusha Mrisho Gambo amemwagiza katibu tawala mkoa wa Arusha Richard Kwitega kuwachukulia hatua za kinidhamu na kiutumishi watumishi sita (6) wa halmashauri ya wilaya ya Longido kutokana na makosa mbalimbali ya kiutumishi.

Miongoni mwa watakaochukuliwa hatua ni pamoja na aliyekua Kaimu Afisa Utumishi wa wilaya hiyo kwa mwaka 2016/17 Bwana Steven Mbombe na msimamizi wa mfumo wa mishahara LGHRIS Bwana Derek Rutenge kwa uzembe wa kuwalipa mishahara watumishi wawili marehemu na kuisababishia hasara serikali ya shilingi milioni saba na elfu themanini na nane (7,088,000/=).




Wengine ni Peter Sembe Mhasibu wa kitengo cha ukaguzi wa awali (pre-audit) kwa kupuuzia wito wa kikao cha mkuu huyo wa mkoa, vilevile ameagiza wahasibu watatu wa kitengo cha mapato kupewa barua za onyo kwa kutokuwepo bila kutoa taarifa kwa mwajiri wao mbali na kujulishwa juu ya uwepo wa kikao hicho cha ufuatiliaji wa hoja za mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali CAG.

Katika taarifa ya CAG kwa mwaka wa fedha 2016/17 halmashauri ya Longido imepata hati inayotia mashaka.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: