Na WMJJWM - Morogoro

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Wizara za kisekta pamoja na Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) imeanza zoezi la kufanya tathmini ya utendajii kazi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) kwa kipindi cha miaka mitano 2020/2021 - 2024/2025.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi akikabidhi Tuzo maalumu Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah (wa pili kushoto), kwa niaba ya kampuni hiyo na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia watu wenye uhitaji.

...............................

 Na Dotto Mwaibale, Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi ametoa Tuzo maalum kwa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar na Qatar Foundation kwa kutambua mchango wao mkubwa katika kusaidia watu wenye uhitaji.

Dkt. Mwinyi alitoa tuzo hizo katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Watu Wenye Ulemavu yaliyofanyika Desemba 4, 2025 kwenye Ukumbi wa Dr. Shein – Tunguu, Chuo Kikuu cha SUZA, Mkoa wa Kusini Unguja tukio lililohudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa maendeleo, mashirika ya kijamii, na wananchi kutoka sehemu mbalimbali za Zanzibar.

Akihutubia katika maadhimisho hayo Rais Mwinyi aliwataka wadau kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuwawezesha watu wenye ulemavu na alisisitiza kuwa maendeleo ya kweli ni yale yanayowahusisha watu wote bila kuacha kundi lolote nyuma.

Aidha, Dkt. Mwinyi alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wadau na wahisani kwa kujitolea kwao kuchangia maendeleo ya jamii zenye watu wenye ulemavu na kueleza kuwa Serikali itayafanyia kazi maoni na ushauri uliotolewa ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa kamili za kutimiza malengo yao.

Kwa upande wake Meneja Mkazi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Paul Atallah, alilishukuru Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar kwa kutambua mchango wa Emirates Leisure Retail na kueleza kwamba kampuni hiyo itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa Serikali na jamii katika kuleta maendeleo chanya kwa watu wenye ulemavu.

Utambuzi wa Wadau Maalumu

Katibu Mtendaji wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamis Debe, akizungumza kwenye maadhimisho hayo  alitoa shukrani kwa wadau wote wanaounga mkono juhudi za Serikali katika kusaidia watu wenye ulemavu.

Aidha, kwa nafasi ya kipekee alimshukuru Afisa Utawala Msaidizi wa Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar, Ramadhan Hussein Layya (Maarufu Msokolo),kwa mchango wake mkubwa na wa muda mrefu, hususan katika kusaidia watu wenye ulemavu wa ngozi kupitia misaada, ushiriki, na michango inayobadilisha maisha ya wanufaika.

Kaulimbiu ya Maadhimisho:

"Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa Watu Wenye Ulemavu kwa Maendeleo Jumuishi."

Misaada Iliyotolewa katika maadhimisho hayo kwa ajili ya makundi mbalimbali ya wahitaji ni

Vyerehani kwa ajili ya kujiajiri, kofia maalumu (round hats) kwa ulinzi wa ngozi, miwani ya kinga na vifaa vya kurekebisha uoni, baiskeli za mwendo kwa watu wenye ulemavu wa viungo, fedha za mikopo kwa kuanzisha au kuendeleza biashara.

Vifaa vingine vilivyotolewa ni vya kuongeza uwezo wa kujitegemea mashine za kusaga nafaka.

Misaada hiyo imeleta furaha, matumaini, na thamani kubwa kwa wanufaika na familia zao, ambayo inakwenda kuwasaidia kutimiza ndoto zao na kuimarisha ustawi wa familia zenye watu wenye uhitaji maalumu.

Kauli ya Emirates Leisure Retail Zanzibar na Qatar Foundation:

Uongozi wa kampuni hizo umeeleza dhamira zao za kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine kuhakikisha watu wenye ulemavu Zanzibar wanapata fursa sawa za ustawi na maendeleo, na kuendelea kuwekeza katika miradi ya kijamii inayobadilisha maisha ya watu wenye uhitaji maalumu.

Viongozi wa Kampuni hizo na wadau mbalimbali wakiwa kwenye maadhimisho hayo.
 

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imekuwa mshindi wa kwanza na kupewa tuzo ya umahiri katika utayarishaji bora wa taarifa za hesabu kwa mwaka 2024 kwa kufuata viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Hesabu International Public Sectors Accounting Standards (IPSAS) katika kundi la Taasisi za Serikali zinazojitegemea.

MAMLAKA ya Mapato tanzania (TRA), imeibuka Mshindi wa kwanza wa jumla katika tuzo ya Uandaaji wa Hesabu za Kifedha zinazozingatia viwango vya Kimataifa vya Uhasibu katika Sekta ya Umma (IPSAS), zinazotolewa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA).

Pia imeibuka mshindi wa kwanza katika tuzo ya kipengele cha Taasisi za Serikali (Government Agency Categories).

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika hafla ya kukabidhi tuzo hizo, Naibu Waziri wa Fedha Laurent Luswetula, alizipongeza taasisi zilizoibuka na ushindi, huku akisema wizara hiyo itaendelea kutoa ushirikiano kwa NBAA, ili kuendelea kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora.

Pia alisema serikali itahakikisha NBAA inasimama imara ili iendelee kuzalisha watendaji bora kwa maslahi mapana ya taifa.

"Wizara ya fedha itaendelea kuhakikisha inatoa ushirikiano kwa NBAA ili kuzalisha wahasibu na wakaguzi bora kwa mslahi mapana ya taifa letu."alisema

Vilevile Naibu Waziri huyo alipongeza NBAA kwa kuendelea kupanua wigo wa kuongeza washiriki kila mwaka.

Naye Naibu Kamishina Mkuu wa TRA Mcha Hassan Mcha lisema, tuzo waliyopata ina umuhimu mkubwa, kwani inachangia kuonesha utendaji wao unakubalika Kimataifa.

Pia alisema tuzo hiyo inaonesha umahiri na ubunifu uliyopo kwa watumishi wa mamlaka hiyo.

"Tuzo hii ina umuhimu sana kwetu, inachangia kuonesha utendaji wetu unakubalika Kimataifa na ina waonesha Walipa Kodi kwamba kila shilingi inayokusanywa inafika katika mfuko Mkuu wa Serikali."alisema

Vilevile Mcha aliwashukuru Walipa Kodi kwa kuendelea kulipa kwasababu TRA imeendelea kuvuka malengo ya ukusanyaji mapato kila mwaka.

Kwamujibu wa Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA Profesa Slyivia Temu, katika hafla hiyo jumla ya taasisi 86 za Umma na binafsi zimeshiriki katika kujipima ubora wa kuwasilisha taarifa za fedha kwa mwaka 2024.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA Pius Maneno, lengo la tuzo hizo ni kuhakikisha taarifa za hesabu zinazotolewa zinakuwa na uwazi na uwajibikaji.

Alifafanua kuwa, tuzo hizo ni taarifa za hesabu za kuanzia Januari mwaka 2024 hadi Desemba, ambazo zimezalishwa kwa kufuata hesabu za Kimataifa na zilizopata hati safi.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifungua Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri.

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa wito kwa Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi katika kubuni vyanzo vipya vya mapato, sambamba na kuimarisha umoja, amani na uzalendo katika maeneo yao ya utawala.

Wito huo umetolewa katika ufunguzi wa Baraza la Madiwani lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri, muda mfupi baada ya madiwani hao kuapishwa rasmi kuanza kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Nyamwese amewataka madiwani kuhakikisha wanakuwa chachu ya amani na utulivu, akisisitiza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu kwa ustawi wa jamii na utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Amebainisha kuwa madiwani wana wajibu mkubwa wa kushirikiana kikamilifu na Mkurugenzi wa Halmashauri katika kubuni vyanzo vipya na endelevu vya mapato vitakavyoongeza uwezo wa Serikali ya Mtaa kusimamia na kutekeleza miradi ya wananchi.

Aidha, ameeleza kuwa kuimarisha ukusanyaji mapato na kusimamia miradi ya kimkakati kutasaidia kupunguza utegemezi na kuongeza kasi ya maendeleo ya Halmashauri.

“Madiwani mna wajibu wa kuhakikisha ushirikiano baina ya watendaji na wananchi unaongezeka ili kufanikisha malengo ya pamoja ya maendeleo,” amesisitiza.

 


MKUU wa wilaya ya Muheza Mkoani Tanga Ayubu Sebabili amesisitiza umuhimu wa ukusanyaji wa mapato huku akiwataka madiwani wa Halmashauri hiyo kuwasaidia katika eneo hilo kutokana na kwamba hayakusanywi mbinguni wala hewani bali ni katika maeneo yao yanayoishi.


Sebabili aliyasema hayo leo wakati akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri hilo ambalo awali lilitanguliwa na Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Halmashauri na Makamu wake ikiwemo kamati mbalimbali.

Alisema katika suala la ukusanyaji wa mapato wanahitaji kutoa ushirikiano kwa sababu maendeleo ya wilaya yataendana pia na kazi ya ukusanyaji wa mapato kama watakasanya kidogo hata asilimia 10 ya vijana,wanawake na walemavu watapata kidogo.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kwamba iwapo wakiendelea kupata kidogo fedha inayotoka haitatosheleza hivyo wanahitaji kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha mapato yanaongezeka.

“Kwenye hili la mapato tunahitaji uadilifu wa nyie madiwani mnaweza kutufikisha pazuri lakini kama mtashirikiana na watu ambao wamepewa dhamana ya kukusanya mapato halafu wakawa sio waadilifu maanake mnakwenda kuiharibu Halmashauri”alisema DC huyo

“Lakii kwenye mapato lazima tuwe na ubunifu pamoja na uwepo wa watalaamu lakini nyie ndio mnafanya maamuzi hivyo tunahitaji kuibua vyanzo vipya vya mapato ambavyo ni sahhi kwa mujibu wa sheria havina maudhi kwa wananchi na ubunifu wetu ni wa muhimu sana”Alisema

Akizungumza matumizi ya tekonolojia katika ukusanyaji mapato ,aliwataka madiwani waende wakasimamie suala hilo kama ni posi kufanya kazi zifanye inavyostahili kama ni control number zitolwe inavyostahili wote pamoja wewe kitu kimoja kuhakikisha jambo letu linakwenda vizuri tofauti na hapo wanakwenda kuiharibu halmashauri.



Akizungumzia suala utatuzi wa migogoro katika maeneo yao aliwaambie kwamba iwapo watashiriki vizuri katika utatuzi wa migogoro wana uhakika kwa asilimia kubwa wananchi wataweza kuwaelewa kwa sababu haiwezekani mgogoro una miaka karibu 20 kijiji wanamsubiri mkuu wa wilaya kwenda kuupatia ufumbuzi.



“Hivyo lazima migogoro yote mnaipatia ufumbuzi kwa ushirikiano ngazi za chini fanyeni mikutano ya hadhara ya utatuzi kule kwenye kamati za maendeleo hakikishe kunakuwa agenda ya utatuzi wa migogoro muijue ambayo ni kero tukiweza kutatua migogoro chini hata suala la usalama linakuwa ni zuri”Alisema

Alieleza kwamba migogoro mingi ni ya ardhi hivyo wanaomba utaratibu wa kisheria utumike kutatua migogoro hiyo kwa kuyaelewa matatizo yaliyopo na hatua ambazo wamezichukua kuleta suluhu.

Hata hivyo aliwataka kujiepusha na vitendo vya rushwa kwa sababu Serikali haitomtetea kiongozi wa umma ambaye anahusika kwenye vitendo hivyo.

Hata hivyo akielezea usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo alisema katika eneo hilo kwa uzoefu wanafeli sana kutokana na baadhi yao kujihusisha na miradi ukishaamua kuwa mtumishi wa umma ndani ya halmashauri nidhamu ni kitu muhimu .


Awali akiungmza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muheza Dkt Jumaa Mhina alimpongeza Rais Dkt Samia Suluhu kwa ushindi mkubwa alioupata kwenye uchaguzi mkuu wa 2025 wanaendelea kumuunga mkono na kupokea maelekezo mbalimbali katika utekelezaji wa shughuli za kuwaletea maendeleo watanzania.


Naye kwa upande Mwenyekiti wa Halmashauri ya Muheza Salim Sechambo alisema kwamba moja ya vipaumbele vyake ni kuhakikisha wanasimamia kikamilifu suala la mapato katika halmashauri hiyo .


Alisema kwamba wana vyanzo vingi vya mapato kikubwa ni kushirikiana kwa kina na kuinyesha utulivu na kusimamia vyanzo vilivyopo na kubuni vyengine kwa maslahi mapana ya Muheza.

Aliongeza pia wanakwenda kusimamia vema miradi na ambayo wanaanza nayo ni kusimamia kwa nguvu zao zote na kuhakikisha kila fedha inayoingia kwenye Halmshauri hiyo ili dhamira ya Rais Dkt Samia Suluhu na Mbunge wao Hamisi Mwijuma “Mwana FA” inatimia

Mwenyekiti huyo wa Halmashauri alisema kwamba wanahitaji umoja na mshikamano hivyo wasitoe nafasi ya mpasuko bali waonyeshe umoja ili waweze kuijenga Halmashauri hiyo.
 

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni wameaswa kuzingatia miiko ya viongozi wa umma na kudumisha uadilifu katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa Baraza la Madiwani Desemba 4, 2025, kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Bakari Mussa kutoka Ofisi ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma amewataka madiwani hao kuzingatia maadili, kuepuka mgongano wa maslahi, na kushirikiana kikamilifu na Mkurugenzi wa Halmashauri katika kusimamia shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amewahimiza madiwani kufanya kazi kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi na ya Halmashauri. 

Amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji na kujiepusha na vitendo vinavyohatarisha uadilifu wa utumishi wa umma.



Mkoa wa Rukwa umejidhihirisha kwa kasi kama kitovu kipya cha kimataifa cha biashara ya madini, hatua inayojengwa na utajiri mkubwa wa rasilimali, miundombinu bora, usalama ulioboreshwa na mifumo rafiki ya Serikali katika usimamizi wa sekta hiyo. Hali hii imeufanya Mkoa huo kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.


Akizungumza Desemba 04, 2025, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Joseph Kumburu, amesema Serikali imeweka mazingira madhubuti ya kuongeza uwekezaji kupitia mabadiliko makubwa katika utoaji wa leseni, usimamizi wa masoko ya madini na kuimarisha miundombinu ya kusafirisha bidhaa ndani na nje ya nchi. 


Amesisitiza kuwa Rukwa sasa inatambulika kimataifa kutokana na aina mbalimbali za madini pamoja na hatua za Serikali kuimarisha utawala bora na kupunguza urasimu katika mchakato mzima wa uwekezaji.


Kwa mujibu wa Mhandisi Kumburu, zaidi ya leseni 480 za madini tayari zimetolewa katika Mkoa wa Rukwa na maombi mengine zaidi ya 600 yanaendelea kushughulikiwa kupitia mifumo ya kidigitali ya Tume ya Madini, hatua iliyoongeza uwazi na kasi ya utoaji wa leseni. Takwimu zinaonesha kwamba kwa mwaka wa fedha 2024/2025, jumla ya tani 337.6 za madini mbalimbali ziliuzwa katika masoko na vituo rasmi vya Rukwa, zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 264, huku Serikali ikikusanya zaidi ya shilingi milioni 18 kupitia mrabaha, ada za ukaguzi na vibali vya usafirishaji.


Aidha, Ofisi ilikusanya jumla ya kiasi cha shilingi milioni 656.2 sawa na asilimia 87.5 ya makusanyo yote kwa mwaka wa fedha 2024/2025.


Rukwa inajivunia aina nyingi za madini ikiwemo dhahabu, shaba, makaa ya mawe, madini ya viwandani, vito na madini ya kimkakati kama helium na rare earth elements. Aidha, kijiografia Mkoa una faida ya pekee kutokana na kupakana na Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), pamoja na kuwa na Bandari ya Ziwa Tanganyika inayorahisisha biashara ya kimataifa na usafirishaji wa vifaa vya uchimbaji.


Kwa upande wa wachimbaji wadogo, Serikali inaendelea kutenga na kupima zaidi ya hekta 13,000 zitakazotumika kuendeleza shughuli za uchimbaji mdogo, ambapo maeneo hayo yanatarajiwa kutoa zaidi ya leseni 700. Mahitaji makubwa ya vifaa vya ujenzi kutokana na miradi ya kimkakati pia yamefungua milango kwa wawekezaji kuanzisha mitambo ya kuzalisha mazao kama kokoto, mchanga, kifusi na mawe.


Mhandisi Kumburu amesema mpango wa Mkoa unalenga kuimarisha masoko ya madini, kupanua masoko mapya ndani na nje ya nchi, kuwaunganisha wachimbaji na taasisi za kifedha pamoja na kuongeza ulinzi na matumizi ya teknolojia kupambana na utoroshaji wa madini. 


Amesema Serikali imewekeza nguvu kubwa katika kuongeza uwazi kwenye mnyororo wa thamani wa madini ili kuvutia wawekezaji na kulinda maslahi ya Taifa.


Aidha, Mhandisi Kumburu ametoa wito kwa vijana wa Mkoa wa Rukwa na mikoa ya jirani kuchangamkia fursa hizo, hasa katika maeneo mapya yanayofunguliwa na Serikali. 


Amesema pia Rukwa kwa sasa imeandaa mkakati wa kuweka kituo cha Mradi mkubwa wa madini ya shaba (Copper Industrial Park) katika Wilaya ya Nkasi ambapo majadiliano yanaendelea kati ya Mkoa na wawekezaji kutoka China baada ya wawekezaji kutembelea nchini na kujiridhisha na uwepo wa madini ya shaba katika Mkoa wa Rukwa na mikoa ya jirani.


“Rukwa imefunguka na sasa ni wakati wa wawekezaji kuchangamkia fursa hizi. Mazingira ya uwekezaji yameboreshwa na rasilimali zipo kwa wingi. Tunawakaribisha wote kuwekeza kwa manufaa ya Rukwa na Taifa kwa ujumla,” amesema.


Kwa ujumla, Rukwa inaendelea kupanda ngazi katika ramani ya uwekezaji Tanzania, ikiwa kama kitovu cha biashara, teknolojia na uchimbaji endelevu wa madini, huku mifumo dhabiti ya usimamizi na fursa nyingi ikiuweka Mkoa huo katika nafasi ya kipekee kwa wawekezaji wanaotafuta mazingira salama na yenye tija.

 


Na Mwandishi Wetu, Banjul

Afrika imeanza sura mpya ya mageuzi katika sekta ya misitu na wanyamapori baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Misitu na Wanyamapori Afrika (AFWC25), Prof. Dos Santos Silayo, kukabidhi rasmi uenyekiti kwa Mr. Ebrima Jawara wa Serikali ya Gambia, hatua iliyoweka mwelekeo mpya wa bara katika kukabiliana na changamoto za karne ya sasa.

Akizungumza katika kikao cha 25 cha AFWC, kilichofanyika Banjul, Prof. Silayo alionya kwamba bara la Afrika liko kwenye shinikizo kubwa linalotokana na kasi ya mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la migongano ya binadamu na wanyamapori, pamoja na mahitaji mapya ya kijamii na kiuchumi yanayoathiri rasilimali asilia. Alisisitiza kwamba Afrika haiwezi tena kutegemea mbinu za kale katika usimamizi wa misitu na wanyamapori.

“Mabadiliko ya tabianchi yamebadilisha mazingira, tabia za watu zimebadilika, na mienendo ya wanyama imebadilika pia. Hatuwezi kuendelea kwa mazoea; tunahitaji ubunifu jumuishi unaotumia sayansi na unaowajibika,” alisema.

Alibainisha kuwa sekta inaweza kuimarika tu ikiwa mataifa yatawekeza katika modeli sahihi za kaboni, teknolojia za kisasa za ufuatiliaji wa misitu, tafiti za mwingiliano wa maji na misitu, mbinu za kisasa za kupunguza uharibifu wa misitu, pamoja na kuimarisha taasisi za jamii ambazo ndizo msingi wa shughuli za uhifadhi.

Katika uchaguzi uliofanyika kwenye kikao hicho, Mr. Ebrima Jawara, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mazingira ya Gambia, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti mpya wa AFWC25. Akipokea wadhifa huo, Jawara alitoa hotuba ya shukrani, akiahidi kuendeleza mageuzi yaliyowekwa na mtangulizi wake na kusisitiza kwamba mustakabali wa uhifadhi wa Afrika unahitaji dira ya pamoja, uongozi unaotegemea ushahidi wa kisayansi, na ushirikiano wa kikanda.

Aidha, viongozi kutoka Rwanda, Chad na Botswana waliteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Tume, uteuzi uliopongezwa na wajumbe kama ishara ya uwakilishi mpana na mshikamano wa kikanda. Wajumbe pia walimhakikishia Jawara ushirikiano wa karibu, wakisema, “Tupo nyuma yako. Tuendelee kulinda rasilimali zetu na kuimarisha sera zetu.”

“Tunategemea ushirikiano wa viongozi wa nchi na wadau wote. Mwenyekiti Jawara na timu yake wana jukumu la kuimarisha usimamizi wa misitu na uhifadhi wa wanyamapori barani Afrika kwa njia endelevu na ya kisayansi,” alisema Katibu wa AFWC, Edward Kilawe, akisisitiza umuhimu wa uongozi mpya katika kuendeleza ajenda za kikanda.

Katika hatua nyingine, wajumbe kutoka nchi mbalimbali walimpongeza Prof. Silayo kwa uongozi wake katika kipindi kilichokabiliwa na changamoto za tabianchi, ongezeko la shinikizo la ardhi na mahitaji mapya ya kiuchumi.

AFWC25 ni kikao cha kikanda cha wakuu wa sekta ya misitu na wanyamapori barani Afrika, kilichokutana kwa mwaka wa 25 mfululizo kujadili changamoto, kushirikiana mbinu za kisayansi, na kuboresha sera za uhifadhi. Kikao cha mwaka huu, kilichoanza Desemba 1 hadi 5, 2025, kilihusisha wajumbe kutoka nchi zote za Afrika, wakijadili mwelekeo wa usimamizi wa misitu, migongano kati ya binadamu na wanyamapori, na mbinu za kuendeleza mageuzi endelevu ya sekta hiyo.



Tanzania, kupitia Wakala wa Huduma za Misitu (TFS), imeungana na nchi nyingine za Afrika katika warsha ya kimataifa iliyojadili mbinu mpya za kupima na kufuatilia kiwango cha hewa ukaa kinachofyonzwa na miti inayoota nje ya misitu, maarufu kama Trees Outside Forests (TOF).

Warsha hiyo ya siku mbili, Desemba 2 hadi 3, 2025 imefanyika katika Hoteli ya Sigelege, Salima nchini Malawi chini ya uratibu wa Michigan State University (MSU), kwa kushirikiana na vyuo na taasisi za utafiti kutoka Malawi, Senegal na Marekani.

Tanzania inawakilishwa na wahifadhi wawili kutoka TFS, Rogers Nyinondi na Jameseth Lazaro, walioalikwa kutokana na nafasi ya TFS kuratibu utekelezaji wa mpango wa kitaifa wa kurejesha uoto wa asili kupitia African Forest Landscape Restoration Initiative (AFR100). Kupitia mpango huo, Tanzania imeahidi kurejesha takribani hekta milioni 5.2 za maeneo yaliyoharibika ifikapo 2030.

Kwa mujibu wa Mkufunzi Mkuu kutoka Michigan State University (MSU), Prof. David L. Skole, warsha hiyo imetoa hatua kubwa ya kiufundi katika ufuatiliaji wa hewa ukaa kwa kutumia teknolojia za high-resolution satellite remote sensing, deep machine learning na allometric scaling models, mbinu zinazowezesha kutambua na kupima miti mmoja mmoja katika maelfu ya hekta. 

Skole alisema mafunzo hayo, ambayo yamemalizika leo, yamelenga kusaidia nchi wanachama kuimarisha mifumo ya uthibitishaji wa taarifa za urejeshaji mazingira na kuweka msingi thabiti wa usimamizi wa ardhi barani Afrika.

Kwa upande wa Tanzania, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Rogers Nyinondi, alisema ushiriki wa Tanzania umeongeza uelewa wa kitaalamu kuhusu mchango wa miti nje ya misitu, ikiwemo kilimo mseto katika kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi. Huku akibainisha kuwa mbinu mpya walizopatiwa zitaboresha ukusanyaji wa takwimu za kaboni, kuimarisha upangaji wa sera na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya urejeshaji ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Warsha hiyo imewaleta pamoja wanasayansi na wataalamu kutoka Rwanda, Kenya, Tanzania, DRC, Senegal, India na Malawi, pamoja na wadau wa AFR100, kujadili maendeleo ya mradi wa kimataifa unaofadhiliwa na MSU.

 


Mkoa wa Katavi umeendelea kuwa kivutio cha wawekezaji kufuatia maboresho makubwa ya miundombinu, usalama na kasi ya utoaji leseni katika Sekta ya Madini. 

Afisa Madini Mkazi wa mkoa huo, Mhandisi Andrew Mwalugaja, ametoa wito kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuchangamkia fursa zinazopatikana katika dhahabu, shaba, risasi, fedha, nikeli, manganese na madini ya ujenzi.

Amesema kuwa ofisi yake imeongeza kasi ya utoaji leseni, ikiwemo leseni tatu za utafiti na zaidi ya leseni 300 za uchimbaji mdogo na wa kati ndani ya miezi minne. Katika biashara ya madini, leseni 82 tayari zimetolewa kati ya Julai na Oktoba 2025, hatua inayodhihirisha mwamko mkubwa wa uwekezaji.

Serikali imeanzisha masoko mawili ya madini Mpanda na Karema ili kuhakikisha wachimbaji, hususan vijana, wanapata soko la uhakika na kufanya shughuli zao kwa uwazi zaidi. Hadi sasa, mkoa umefanikiwa kuongeza makusanyo ya maduhuli hadi Shilingi bilioni 3.80 ndani ya miezi minne tu.

Wachimbaji na wawekezaji wamesema maboresho ya mazingira ya uwekezaji, matumizi ya teknolojia za kisasa na ushirikiano mzuri na Serikali yameongeza uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali. Kampuni ya Jiuxing Tanzania Mining Company imeeleza kuwa ushirikiano na wataalam pamoja na teknolojia ya froth flotation umeongeza tija, usalama na ujuzi kwa vijana wa Mpanda.

  


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amefanya ziara ya kushtukiza katika huduma ya mabasi ya mwendokasi ya Gerezani - Kimara, ili kujiridhisha na utoaji wa huduma mara baada ya Serikali kuelekeza huduma hiyo irejee katika jiji la Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kusikiliza malalamiko ya wananchi wanaotumia usafiri wa Mwendokasi, ambapo wamelalamika juu ya uchache wa mabasi ya mwendokasi hatua iliyopelekea Prof. Shemdoe kumpigia simu na kumuelekeza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) Bw. Pius Andrew Ng’ingo kuongeza mabasi ya mwendokasi ili yawahudumie wananchi.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe kutembelea huduma ya mabasi ya mwendokasi imepokelewa vizuri na wananchi wanaotumia mabasi hayo, ambapo wamempongeza kwa kitendo chake cha kufanya ufuatiliaji ili kujiridhisha na huduma inayotolewa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe mara baada ya kuapishwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais ya kuwaletea wananchi tabasamu, hivyo ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya kuhakikisha wananchi wanapata tabasabu kupitia huduma zitolewazo na mabasi ya mwendokasi.

 


Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde leo Desemba 2, 2025 amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mkuu wa Fedha wa Kampuni mama ya Perseus na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga, Bi. Lee-Anne de Bruin ambao ni wawekezaji kwenye mgodi wa uchimbaji wa dhahabu wa Nyanzaga uliopo Wilayani Sengerema. Bi. Lee-Anne de Bruin aliongozana na Bw. Matt Cavedon, Meneja Mkuu na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga na Bw. Isaac Lupokela, Afisa Mkuu wa Fedha wa Mradi wa Nyanzaga.

Mazungumzo hayo yaliangazia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika utekelezaji wa uanzishwaji wa mgodi huo ambao unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi wa Nchi yetu na wananchi wa Sengerema.

Aidha, Waziri Mavunde aliwahakikishia wawekezaji wa Perseus kuwa Wizara itaendelea kuwa bega kwa bega na wawekezaji katika kufanikisha uendelezaji wa Mgodi wa dhahabu wa Nyanzaga ili uweze kuleta mafanikio kwenye uchumi wa Tanzania na kusaidia upatikanaji wa Ajira kwa Watanzania wengi.