OR- TAMISEMI

Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI inataendelea kuwachukulia hatua wakandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa Barabara chini ya kiwango.

Hayo yamesemwa  leo Aprili 30, 2025 Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Rais – TAMISEMI Mhe. Zainab Katimba kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa wakati akijibu swali la nyongeza la Mhe. Aleksia Kamguna,mbunge wa Viti maalum aliyetaka kujua serikali inawachukulia hatua gani wakandarasi wanojenga Barabara chini ya kiwango

“Serikali inapotoa nafasi ya ujenzi wa barabara hizi kwa wakandarasi inatarajia wakandarasi waweze kuzingatia mkataba wanapokuwa wanatekeleza ujenzi wa barabara hizi za wilaya na serikali inakuwa makini kusimamia viwango” amesema Mhe.Katimba

Katika swali la msingi la Mhe. Kamguna ameuliza lini Serikali itajenga barabara za Wilaya ya Malinyi kwa kiwango cha Lami

Akijibu Swali hilo Mhe. Katimba amesema “Serikali inakusudia kujenga kwa tabaka la lami barabara za makao makuu ya wilaya zote hapa nchini ikiwemo wilaya ya Malinyi na katika mwaka 2024/25”

“Serikali inaendelea na ujenzi wa barabara ya Mnadani-Bomani inayoelekea Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Malinyi kwa tabaka la lami (kilomita 0.85) kwa thamani ya shilingi 759,000,000.00 Mpaka sasa ujenzi bado unaendelea na umefikia 30%”. Mhe. Zainab Katimba

 


WAZIRI wa Madini Mheshimiwa Anthony Mavunde (MB) ametoa maelekezo matano kwa Menejimenti ya  Tume ya Madini hasa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuzingatia na kusimamia  sheria katika utekelezaji wa majukumu yao na kufikiri nje ya boksi ili kuwa na kitu cha ziada katika kuendeleza Sekta ya Madini.

Waziri Mavunde ameyasema hayo leo Aprili 30, 2025 jijini Dodoma kwenye ufunguzi wa kikao cha Menejimenti ya Tume ya Madini ambapo  amewataka watendaji kuwa wabunifu katika maeneo yao, washirikiane, mkoa mmoja na mkoa mwingine pamoja na kushauriana.

“Kwenye Sekta ya Madini  ukiweka sheria pembeni utaivuruga sekta,  kuna wakati matumizi ya busara huwa yanahitajika lakini sheria kwanza, kaisimamieni, kesho keshokutwa mtu atakuuliza jambo lingine lolote dhamira yako ilikuwa nini na sheria inasema nini, kasimamie sheria kwanza na kama kuna maelekezo tofauti yasitokane na wewe, wewe katimize  wajibu wako wa kusimamia sheria ni muhimu sana,”amesema Waziri Mavunde.

Agizo la pili ambalo amelitoa Mheshimiwa Mavunde ni kutaka ubunifu na kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

“Nataka mkawe wabunifu, tumenunua magari 101 mengine yanakuja pikipiki 140  Rais Daktari Samia Suluhu Hassan ametupatia nyenzo, nataka mfikiri nje ya boksi  nini ufanye kwenye eneo lako ili sekta  iweze kushamiri zaidi, isiwe ‘business as usual’ tunatamani kuona kila mtu katika eneo lake anajitahidi,”amesema.

Katika  hatua nyingine Mheshimiwa Mavunde amewapongeza Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kwa ukusanyaji wa maduhuli na kuwataka kutorudi nyuma  na kuhakikisha kila mmoja anavuka lengo alilopangiwa na kuongeza kuwa,

“Mjitahidi kutafuta njia za kuongeza makusanyo pasipo kuleta athari kwa watu mnaowasimamia. Zipo njia nyingi za kufanya simamieni hilo, sisi tunaingiza fedha nyingi sana katika mfuko mkuu wa Serikali, miradi inayokuja mikubwa naamini tutafanya vizuri zaidi.

Katika agizo la nne la uadilifu Waziri Mavunde ameeleza kuwa hivi karibuni Sekta ya Madini imekuwa na utulivu pasipo kuwepo na malalamiko yoyote na kuwataka Maafisa  Madini Wakazi wa Mikoa kuendelea kutenda haki pasipo kuonea wadau wa madini na kutatua migororo na changamoto zinazowakumba wadau wa madini.

Amewasisitiza Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuhakikisha wanatatua migogoro kwa kufuata haki ili kujenga imani na wachimbaji wa  madini na kuendelea kutoa elimu kuhusu Sheria na Kanuni za  Madini ili kupunguza migogoro kabisa.

Akitoa agizo la Tano Mheshimiwa Mavunde amesema kuwa ili kuongeza ushiriki wa watanzania katika Sekta ya Madini, imeundwa kamati maalum ya kuwajengea uwezo watanzania kushiriki kikamilifu katika Sekta ya Madini ili baadaye wawe wachimbaji wakubwa wa madini na kuelekeza Watendaji wa Tume ya Madini kutoa ushirikiano kwa kamati hiyo.

“Wanapokuwepo wachimbaji wakubwa ambao ni wazawa faida lukuki zinapatikana ikiwa ni pamoja na ajira, mapato na ongezeko la manunuzi ya bidhaa na huduma za ndani ya nchi,” amesema  Waziri Mavunde.

Ameongeza kuwa Serikali imeendelea kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa viwanda vya uongezaji thamani madini nchini ambapo mpaka sasa wawekezaji wengi wamejitokeza kwenye ujenzi wa viwanda vya uongezaji thamani katika mikoa ya kimadini ya Chunya, Dodoma, Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro, Rukwa na Lindi.

Amesema kutokana na utendaji mzuri wa Sekta ya Madini hasa mchango wake kwenye Pato la Taifa kufikia asilimia 10.1 nchi ya Kenya kupitia Waziri wa Madini na Uchumi wa Bluu, Mheshimiwa Ali Hassan Joho wameomba kuja kujifunza nchini Tanzania.

Aidha, amewataka wachimbaji wa madini waliopewa leseni kuzifanyia kazi na kwa ambao hawajazifanyia kazi hatua mbalimbali za kisheria zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuandikiwa hati za makosa na kufutwa kwa mujibu wa sheria.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba akizungumza katika mkutano huo amewataka Viongozi wa Tume ya Madini kuendelea kuimarisha upendo sambamba na kushirikiana ili Sekta ya Madini iendelee kuwa na mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa.

Naye Kamishna wa Tume ya Madini, Mhandisi Theonestina Mwasha akielezea hali ya makusanyo ya maduhuli katika Tume ya Madini amesema kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024 jumla ya kiasi cha shilingi Bilioni 753.8 sawa na asilimia 85.45 ya lengo kilikusanywa.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2024/2025 kuanzia mwezi Julai hadi Aprili 29, 2025 Tume ya Madini imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi Bulioni 862.64 ambacho ni sawa na asilimia 86.53 ya lengo la Shilingi Trilioni Moja.

“Tunaamini kiasi kilichobaki tutakikamilisha ifikapo Juni, 30 mwaka huu kwa kuongeza nguvu na ubunifu kwenye ukusanyaji wa maduhuli na udhibiti wa mianya ya upotevu wa mapato,” amesisitiza Kamishna Mwasha.

 


Mwenyekiti wa kamati ya uongozi ya Taifa ya TASAF Peter Ilomo ameipa mwezi mmoja kamati ya usimamizi miradi ya jamii TASAF kijiji cha Igomba kuhakikisha majengo ya zahanati ya kijiji hicho yanakamilika ili iweze kuanza kutoa huduma na kuwapunguzia adha wakazi wa Igomba kufuata huduma ya afya umbali mrefu.

Ilomo ametoa agizo hilo mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa majengo ya zahanati hiyo iliyopo katika kijiji cha Igomba wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe ambapo amesema uwepo wa Zahanati ni muhimu katika kijiji hicho kwa kuwa wamekuwa wakifuata huduma ya afya kijiji jirani cha Isimike pamoja na kituo cha afya Saja vinavyopatikana umbali wa KM 6 kutoka kijijini hapo. 

"Tujitahidi usiku na mchana,nimeambiwa mpango ni kumaliza mwezi wa tano lakini na mimi naongeza kidogo mpaka mwezi wa sita kwa kazi nilizoziona ili ikiwezekana mwezi wa saba huduma zianze kutolewa hapa"ameagiza Ilomo

Joyce Mdemwa ni Mratibu wa TASAF wilaya ya Wanging'ombe ameeleza kupokea maelekezo ya kukamilisha mradi huo huku wakazi wa Igomba wakishukuru kukamilishiwa zahanati yao ili kupunguza changamoto ya kufuata huduma ya afya umbali mrefu.

"Tunatarajia kukamilisha mradi huu tarehe theleathini mwezi wa tano na agizo la Mwenyekiti sisi tunamuahidi tutakamilisha na mwezi wa saba tutaanza kutoa huduma"amesema Joyce Mdemwa

Kijiji cha Igomba ni miongini mwa vijiji vya wilaya ya Wanging'ombe  ambavyo vinanufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ambapo licha ya kusaidia kaya maskini lakini pia kijiji hicho kilipokea Milioni 200.2 kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Zahanati pamoja na nyumba ya mganga.







 


Serikali inaendelea kuhakikisha kwamba barabara ambazo zipo katika kila halmashauri ya wilaya zinafunguliwa ili kurahisisha usafiri na usafirishaji katika maeneo ya wananchi.

Hayo yamesemwa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Singida Mhandisi Ibrahimu Kibassa kwenye  Maonesho ya Usalama na Afya Mahali Pa Kazi katika viwanja vya Mandewa Mkoani Singida.

Mhandisi Kibassa alisema katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 TARURA ilipangiwa kutumia Sh.bilioni 886.3 ambazo zimefanikiwa kujenga barabara za kilometa 278.32 za kiwango cha lami na kilometa 9334 za kiwango cha changarawe.

Aliongeza kuwa TARURA imekuwa ikitumia teknolojia ya ujenzi wa madaraja kwa kutumia mawe ambapo yapo madaraja 401 nchini na kwa Mkoa wa Singida yapo madaraja 34 yaliyojengwa kwa mawe na mkoa wa Kigoma unashika nafasi ya kwanza kwa kujenga madaraja mengi ya mawe ikifuatiwa na Arusha.

"Ujenzi wa madaraja kwa teknolojia ya mawe tunatumia sana kwasababu gharama zinapungua kwa asilimia 60 ukilinganisha na teknolojia nyingine za kutumia kokoto kama ilivyo kawaida," alisema.

Alisema kushuka kwa gharama za ujenzi wa madaraja kwa kutumia mawe kunatokana na kwamba mawe hayo yanapatikana kwenye mazingira ya wananchi ambapo nao wananufaika kwa kipato na hivyo kuinua uchumi wao.








 


Jumla ya washiriki 1,800 wakiwemo Maafisa Elimu Kata 600, Walimu Wakuu 600, na Walimu wa TEHAMA 600 kutoka Halmashauri zote 184 nchini wamejengewa uwezo kuhusu matumizi bora na salama ya TEHAMA katika elimu.

Mafunzo hayo yanatekelezwa na Serikali chini ya Mradi wa Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi (BOOST), yakilenga kuongeza ufanisi katika kufundisha na kujifunza kwa kutumia TEHAMA.

Akihitimisha mafunzo hayo Aprili, 29, 2025 mkoani Pwani Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Charles Mahera, amesisitiza wanaufaika wote kuhakikisha wanatumia maarifa, vifaa na kuwa wabunifu katika ufundishaji.

Dkt. Mahera amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuweka mikakati ya kuimarisha usimamizi wa matumizi ya TEHAMA katika shule, kuhakikisha vifaa vinatunzwa na kutumika ipasavyo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu ya Awali na Msingi kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Bi Suzan Nussu, amesema shule  800 zitazopokea vifaa vya TEHAMA katika utekekezaji na kuwataka kuvutumia kunuifasha wakimu na wanafunzi kwa ujumla.

Afisa Elimu Kata wa Murusegamba, Ngara mkoani Kagera Bi Catherine Ntente, kwa niaba ya washiriki, amesema mafunzo yamewapa uwezo wa kutumia mbinu mbalimbali za kidijitali kufundisha kiurahisi na kwa ufanisi.










 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Ridhiwani Kikwete, amesisitiza umuhimu wa wananchi kujiunga na kuchangia Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ili kunufaika na mafao mbalimbali yakiwemo Mafao ya Matibabu kwa Wananchi waliojiajiri. Kwa upande wa wafanyakazi wa NSSF, Mhe.Waziri amewataka kuendelea kuhudumia wanachama kwa weledi.


Mhe. Ridhiwani amesisitiza hayo alipotembelea banda la NSSF kwenye Maonesho ya Wiki ya Usalama na Afya Mahala pa Kazi Duniani, yanayofanyika Kitaifa katika viwanja vya Mandewe, mkoani Singida.

Amesema NSSF ina jukumu kubwa la kutoa huduma za hifadhi ya jamii kwa wanachama wa sekta binafsi na kuwafikia wananchi waliojiajiri kupitia Mfumo wake wa Hifadhi Skimu, ili kuhakikisha hata wale waliojiajiri wenyewe wanapata mafao ya muda mfupi na mrefu.

“NSSF ina wajibu mkubwa wa kuimarisha maisha ya wanachama wake, hasa pale wanapokumbwa na majanga yanayoathiri kipato chao. Hivyo amesisitiza kuendelea kutoa elimu ya mafao na huduma zinazotolewa na Mfuko huo kwa wananchi.

Aidha, Mhe. Ridhiwani alionesha kuridhishwa na jinsi NSSF ilivyotekeleza dhana ya usalama na afya mahala pa kazi.

Kwa upande wake, Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Bw. Oscar Kalimilwa, amesema NSSF imeshiriki maonesho hayo kwa lengo la kutoa elimu kuhusu hifadhi ya jamii, kusajili wanachama wapya kutoka sekta binafsi pamoja na wale waliojiajiri wenyewe.

Bw. Kalimilwa alisisitiza kuwa maonesho hayo yamewapa nafasi ya kuwakumbusha waajiri wa sekta binafsi juu ya wajibu wao wa kuwasajili na kuwasilisha michango ya wafanyakazi wao kwa wakati.

“Ninatoa rai kwa waajiri kuhakikisha michango ya wafanyakazi wao inawasilishwa NSSF kwa wakati kwani hilo ni takwa la kisheria. Kufanya hivyo kutawahakikishia wanachama kulipwa mafao yao kwa wakati na kuondoa usumbufu usio wa lazima," alisema.

Vilevile, aliwahamasisha wananchi waliojiajiri, wakiwemo bodaboda, mama lishe, wavuvi, wakulima, wachimbaji wadogo, wasusi, vinyozi, wasanii na wajasiriamali wengine, kujiunga na kuchangia katika NSSF kupitia Hifadhi Skimu.

Alibainisha kuwa mwanachama aliyejiajiri anapaswa kuchangia si chini ya shilingi 30,000/- kwa mwezi ili kupata mafao mbalimbali yakiwemo ya matibabu, na shilingi 52,200/- mwanachama atapata Mafao ya matibabu yeye na familia yake wakiwemo watoto wanne. Ameongeza kuwa michango hiyo inaweza kufanyika kidijitali kupitia simu za kiganjani ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa uharaka.








 


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt.Doto Biteko amesema dhamira ya Serikali ni kutekeleza mradi mkubwa wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia (LNG) kutokana na faida zake kiuchumi ila kwa sasa kuna maeneo ambayo Serikali inayafanyia kazi kwa kina kupitia majadiliano na Wawekezaji ili mradi husika uwe na tija kwa nchi na wananchi.

Ameyasema hayo tarehe 29 Aprili 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu hoja mbalimbali zilizotolewa na Wabunge kuhusu Hotuba ya Bajeti ya  Wizara ya Nishati ya shilingi Trilioni 2.2 kwa mwaka 2025/2026 kabla ya kupitishwa kwa kishindo na Bunge hilo kwa asilimia 100.

“ Mradi wa LNG umeanza kusemwa kwa muda mrefu na kila mmoja angetamani mradi huu ukamilike jana lakini lazima tukubaliane kuwa lazima tujadiliane kwa kina na wawekezaji ili kupata kilicho bora na kuleta tija, ninachotaka kuwahakikishia ni kuwa timu ya majadiliano ya Serikali na Wawekezaji wanaendelea na majadiliano na tunatarajia kuwa ndani ya mwaka huu 2025 kama tutakuwa tumemaliza masuala matatu yaliyosalia kujadiliwa, mkataba huo utasainiwa ili mradi uanze mara moja.” Amesema Dkt.Biteko

Ameongeza kuwa, Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ana kiu ya kuona mradi huo  unaanza na alishatoa maagizo kwa Wizara ya kuhakikisha kuwa mradi unaanza kutekelezwa.

Akijibu hoja kuhusu vituo vya mafuta vinavyoongezeka na kujengwa kwa kukaribiana,

Dkt.Biteko amesema kuwa Wizara ya Nishati imeanza mazungumzo na Wizara ya Ardhi ili kuongeza umbali kati ya kituo kimoja na kingine kutoka mita 200 za sasa kwa lengo la kuleta usalama wa watu, mazingira na shughuli za kijamii.

Kuhusu msamaha wa kodi mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa gesi inayotumika kwenye vyombo vya moto kama vile magari (CNG), Dkt. Biteko amesema kuwa Serikali ilishatoa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa vifaa na mashine mbalimbali zinazotumika katika mnyororo wa thamani kwa miradi ya CNG kama vile mitungi ya CNG pamoja na vifaa vya kuwezesha kufunga mfumo kuwezesha magari kutumia gesi hiyo.

Ameongeza kuwa, katika mwaka 2024/2025 Wizara ya Nishati imewasilisha Wizara ya Fedha mapendekezo ya maboresho ya kodi katika gesi asilia inayotumika kwenye magari ili kuzidi kuhamasisha matumizi ya CNG na wawekezaji wanaowekeza kwenye miradi hiyo wapate faida na kurudisha gharama wanazowekeza kwa haraka.

Akijibu  hoja za Wabunge kuhusu gharama za kuunganisha umeme vijijini na mijini, Dkt.Biteko amesema kuwa imeundwa timu kwa ajili ya kuangalia namna gani gharama hizo zitapunguzwa lengo likiwa ni kuleta unafuu kwa wananchi.

Kuhusu usambazaji wa umeme Vijijini, Dkt.Biteko amesema kuwa, Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan anapaswa kupongezwa kwa kufikisha umeme katika Vijiji vyote 12,318 kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 huku kazi ya kupeleka umeme vitongojini ikiendelea kwa kasi.

Akizungumzia ujenzi wa vituo vya kupoza umeme katika wilaya zote nchini kupitia mradi wa gridi imara, Dkt. Biteko amesema kuwa tayari Serikali imeshanunua viwanja kwa ajili kujenga vituo hivyo na katika awamu ya kwanza vitajengwa vituo 14 huku utekelezaji ukiendelea na katika laini za umeme ambazo ni ndefu sana Serikali itaweka switching stations.

Aidha, kuhusu suala la kukatika kwa umeme nchini, Dkt.Biteko amesema kuwa  limepungua kwa asilimia 48 huku dakika za kukatika umeme zikipungua kwa asilimia 64 na kwa sasa umeme ukikatika ni kwa sababu tu ya matengenezo ya miundombinu. Hata hivyo amesema Serikali inaendelea kuimarisha kituo cha huduma kwa  Wateja TANESCO ili taarifa ziwafikie wananchi kwa wakati pale umeme unapokatika ikiwemo kila wilaya kuwa na kundi sogozi.

Awali, wakati wa kuhitimisha Hotuba hiyo ya Wizara ya Nishati, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga alimpongeza Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya katika Taifa hususan kwenye Sekta ya Nishati akieleza kuwa moja ya misingi ya ukuaji wa kiuchumi na maendeleo katika Taifa lolote ni uwekezaji katika Sekta ya Nishati.

Akizungumzia mikoa ambayo bado haijaunganishwa katika gridi ya Taifa ya umeme, Kapinga alisema kuwa kuna miradi mbalimbali inayoendelea ambapo katika Mkoa wa Rukwa kuna mradi mkubwa wa kusafirisha umeme unaoendelea wa kutoka Iringa-Tunduma hadi Rukwa na kipande kingine cha mradi kitakachounganisha gridi ya Tanzania na Zambia.

“Mhe.Spika  katika Mkoa wa Mtwara na Lindi tayari mkandarasi yupo eneo la kazi, mradi umeanza kwa kujenga njia ya umeme kutokea Songea-Tunduru-Masasi hadi Mahumbika na tumeshaanza kulipa fidia katika eneo la Tunduru hadi Masasi takriban shilingi bilioni 4.6 na eneo lililobakia la Songea kuelekea Namtumbo na Tunduru tutaendelea kulipa fidia ya takriban shilingi bilioni 2.7.” Alisema Kapinga

Kuhusu kupeleka gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kagera alisema kuwa kazi inaendelea kupitia ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya Benaco-Kyaka na katika Mkoa wa Katavi mradi wa kupeleka umeme wa gridi mkoani humo uko katika hatua za mwisho.

Akizungumzia kazi ya kupeleka umeme kwenye visiwa mbalimbali nchini, Kapinga alisema kuwa, Serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 9.89 ili kupeleka mifumo ya umeme jua katika visiwa 118 ambavyo vipo katika mikoa zaidi ya mitano hususan Wilaya ya Ukerewe.

Kuhusu maboresho miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Kapinga alieleza kuwa kuna kazi zinaendelea kwa lengo la kuwawezesha wananchi kupata umeme wa uhakika ikiwemo uboreshaji wa kituo cha Mbagala ambacho kilikuwa na transfoma yenye uwezo wa MVA 50 lakini sasa inawekwa transfoma mpya yenye uwezo wa MVA 120 ili kukiongezea uwezo kituo hicho ili wananchi wa Mbagala, Temeke, Yombo, Mkuranga na baadhi ya maeneo ya Kigamboni waendelee kupata umeme wa uhakika.

Alieleza kuwa kazi hiyo imefikia mwishoni na muda wowote transfoma hiyo itaanza kufanya kazi. Kwa eneo la Kigamboni amesema maboresho pia yanaendelea kufanyika na kwamba wananchi tayari wameshaanza kuona mabadiliko ya upatikanaji umeme kupitia maboresho hayo.











 


Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Amir Mohammed Mkalipa amewataka watumishi wa umma Wilayani Arumeru kufanyakazi kwa moyo wa kizalendo nyakati zote za utumishi wao ili kuwa kielelezo kwa vizazi vijavyo.

Mkalipa amesema hayo wakati wa sherehe mahafali ya 8 ya kidato cha sita ikiwa sambamba na  sherehe ya kumuaga rasmi Mkuu wa Shule hiyo Ndg.John Massawe aliyehudumu shuleni hapo Kwa Miaka 21.

Akizungumzia suala la uzalendo,,mhe.Mkalipa amesema kuwa Mwl.Masawe amekuwa kielelezo cha utumishi uliotukuka kwani shule hiyo imekuwa mara kwa mara ikifanya vizuri katika ufaulu wa Kitaifa chini ya usimamizi wa Mkuu huyo wa Shule mstaafu kwani wanafunzi wamekuwa wakipata ufaulu wa madaraja ya juu, huku akimtaka Mkuu wa shule mpya pamoja na wanafunzi kuendeleza juhudi ili kulinda hadhi ya shule hiyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Shule Bi Nai Molle ameongeza kwa kusema kuwa mkuu huyo wa shule Mwl.John Massawe ni mfano wa kuigwa na Kiongozi wa kipekee ambae amemudu kufanya kazu katika mazingira magumu na ambayo ameweza kuyabadilisha na sasa ni kivutio na shule ya mfano Kitaifa.

Ameongeza kusema kuwa walimu wa shule ya sekondari Mwandet, wanajuhudi kubwa katika kuwafundisha watoto, na matokeo ya juhudi hizo yanaonekana wazi jambo ambalo limetugusa wazazi wote, na kufanya maamuzi ya kumnunulia gari Mkuu wa Shule John Massawe ikiwa ni shukrani kwa kazi nzuri aliyofanya Kwa Miaka 21 ya Utumishi wake.

"Shule ya Mwandeti ni kubwa, ina walimu wengi, haina nyumba za kutosha kuishi walimu wote hapo shuleni, lakini pia eneo hili halina nyumba za kupangisha, hivyo asilimia kubwa ya walimu hulazimika kuishi Ngaramtoni, huku kukiwa hakuna usafiri wa kuaminika kufika shuleni, walimu wanateseka sana, wazazi tumeamua kuwaondolea adha hiyo wakati wakiwahudumia watoto wetu" amesisitiza Mwenyekiti huyo.

Aidha amefafanua kuwa Mkuu wa Shule John Massawe alihamasiaha ununuzi wa gari aina ya coaster ambao, umegharimu kiasi cha shilingi milioni 48, fedha zilizopatikana kwa kila wazazi kuchanga kiasi cha shilingi elfu thelathini, jambo ambalo limefanyika kwa muda wa miezi miwili baada ya makubaliano ya kikao cha wazazi wote.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Arusha, bwana Seleman Msumi, amempongeza mwl.John Massawe  na kusema moja ya kitu alichofanya ni kuunganisha wazazi na walimu kuwa kitu kimoja na hususan katika kuinua taaluma shuleni hapo pamoja kuifanya shule kuwa moja ya shule bora Nchini kwa matokeo ya mitihani ya kidato cha 4 na 6. 

Mkurugenzi Msumi, amefafanua kuwa, kutokana na Jiografia ya Halmashauri ya Arusha, walimu wa shule nyingi za pembezoni wanakabiliwa na changamoto ya nyumba za kuishi pamoja na usafiri wa kufika shuleni, licha ya kuwa walimu hao, hujitoa kwa hali na mali, kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kufundisha wanafunzi kwa kuweka uzalendo mbele.

Aidha amewasihi wazazi wengine kuigana mfano huo uliofanywa na wazazi wa Mwandet sambamba na kuwataka wadau wa elimu, kujitokeza kuisaidi serikali kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya elimu, hususani katika ujenzi wa nyumba za walimu pamoja na usafiri.

Hata hivyo mkuu huyo wa shule sekondari Mwandet, mwalimu John Masawe amewashukuru wazazi ,waalimu,watumishi na wanafunzi kwa kutambua na kuthamini kazi kubwa aliyofanya kama Mkuu wa shule kwa kushirikiana na wallimu walio chini yake na kuwaomba  kuendelea  kuchapa kazi ili kupataa matokeo maazuri kwa wanafunzi ili waweze kutimiza ndoto zao.

Shule ya sekondari Mwandet ni miongoni mwa shule za Kata, inayoendelea kufanya vizuri katika matokeo ya mitihani ya kitaifa, huku ikiwa ni miongozi wa shule 10 bora kitaifa kwa miaka mitatu mfululizo kwa matokeo ya kidato cha sita

Afisa Habari Mkuu,kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Bi. Joyce Mgaya,akizungumza na watoto Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam mara baada ya kuwasili jijini Dodoma kwa ajili ya ziara ya mafunzo pamoja na kutembelea Mji wa Serikali Mtumba ziara ya mafunzo iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
.....
WATOTO Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam wametembelea Mji wa Serikali Mtumba Dodoam huku wakiushukuru Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni ( BRELA) kwa kudhamini ziara ya mafunzo kwa kutumia reli ya kisasa (SGR).
Akizungumza leo Aprili 29,2025 kwa niaba ya BRELA, Afisa Habari Mkuu, BRELA Bi. Joyce Mgaya amesema ziara hiyo in aonesha dhamira ya BRELA katika kusaidia makundi yenye uhitaji maalum.
“Mtendaji Mkuu wetu aliona ni jambo jema kuwapa watoto hawa fursa ya kutembelea makao makuu ya nchi na kujionea miradi ya maendeleo inayotekelezwa,” amesema Bi Mgaya.
Hata hivyo ameongeza kuwa kwa wengi wao,ni mara ya kwanza kupanda treni ya SGR na kufika Dodoma, na kwamba ziara hiyo ni sehemu ya mikakati ya BRELA kusaidia jamii kupitia programu mbalimbali za kuwafikia wananchi.
Aidha Bi.Mgaya ametoa wito kwa Taasisi zingine ziendelee kuwakimbilia watu wenye mahitaji Kwa kuhakikisha wanawasaidia mahitaji mbalimbali.
Kwa upande wake Mkurugenzi na Mwanzilishi wa kituo cha TUYATA, Bi Fauzia Jabir amesema kuwa wanaishukuru BRELA kwa safari hiyo kwani watoto wengi wamefurahi na katika maisha yao hawajawahi kupanda treni.
“Watoto wamefurahi mno, jambo hili halijawahi kutokea. BRELA imefanya jambo kubwa kwa kusimama na watoto hawa wahitaji. Wamehamasika kusoma zaidi baada ya kuona uzuri na fursa zilizopo nchini,” amesema Bi Jabir.
Hata hivyo, ameeleza kuwa licha ya mafanikio ya kielimu waliyonayo, kituo hicho kinakabiliwa na changamoto kubwa ya makazi kwa watoto yatima, na hivyo kuomba msaada wa ujenzi wa nyumba za makazi kwa watoto na wajane.
Mmoja wa walionufaika na kituo hicho, Bi Ayman Jaffar Abubakar ambaye pia ni msemaji wa TUYATA, amesema kulea watoto kutoka mazingira mbalimbali si kazi rahisi lakini kwa neema ya Mungu, wanajitahidi kutoa malezi bora na kuwaelekeza katika njia sahihi.
“Watoto wengi wanaishi kwa walezi, hivyo ni changamoto kuwafuatilia kikamilifu. Tunaishukuru BRELA kwa kutuunga mkono na tunaomba waendelee kuwa nasi hadi tufikie malengo yetu,” amesema
WATOTO Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam wakiwa ndani ya reli ya kisasa (SGR) kuja jijini Dodoma kutembelea Mji wa Serikali Mtumba ziara ya mafunzo iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
WATOTO Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam wakishuka ndani ya reli ya kisasa (SGR) mara baada ya kuwasili jijini Dodoma kutembelea Mji wa Serikali Mtumba ziara ya mafunzo iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
Afisa Habari Mkuu,kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Bi. Joyce Mgaya,akizungumza na watoto Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam mara baada ya kuwasili jijini Dodoma kwa ajili ya ziara ya mafunzo pamoja na kutembelea Mji wa Serikali Mtumba ziara ya mafunzo iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
Watoto Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam wakifurahia Mji wa Serikali Mtumba baada ya kutembelea ziara ya mafunzo iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
Afisa Habari Mkuu,kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Bi. Joyce Mgaya,akizungumza na waandishi ya habari jijini Dodoma mara baada ya kudhamini ziara ya mafunzo ya Watoto Yatima na wenye Ulemavu 100 kutoka Kituo cha Kulelea Yatima cha Tulee Yatima Tanzania (TUYATA) kutoka Dar es Salaam mara baada ya kutembelea Mji wa Serikali Mtumba ziara iliyodhaminiwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA).
Mkurugenzi na Mwanzilishi wa kituo cha TUYATA, Bi Fauzia Jabir,akiishukuru BRELA kwa safari hiyo kwani watoto wengi wamefurahi na katika maisha yao hawajawahi kupanda treni.
Mmoja wa walionufaika na kituo cha TUYATA na msemaji wa TUYATA Bi Ayman Jaffar Abubakar,akielezea historia yake kwa waandishi wa habari.