Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA) imewataka watoa huduma wa tiketi mtandao kuunganisha mifumo yao na mfumo wa serikali inayosimamiwa na LATRA pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kabla ya Julai 1, 2025.

 


Na John Mapepele 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya  nchini kuwaongeza wananchi katika maeneo yao kufanya "jogging" na mazoezi ili kuimarisha afya.

Mhe. Mchengerwa ametoa  maelekezo hayo leo Juni 14, 2025 mara baada ya kuongoza na kuhitimisha  mbio za pole pole (jogging) za kilomita 10 zilizoratibiwa na Wizara yake katika eneo la Mji wa Serikali wa Mtumba jijini Dodoma.

"Hamasa hii ya kufanya mazoezi iliasisiwa na viongozi wetu wakuu kuanzia enzi za Baba wa taifa letu Mwalimu Nyerere hadi Rais wetu wa sasa Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan lengo likiwa kuimarisha afya na kujikinga na magonjwa nyemelezi hivyo na sisi tuna wajibu wa kuendelea kuwahamasisha watumishi wa Serikali na wananchi kwa ujumla kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye " amefafanua  Waziri Mchengerwa 

Aidha, amewataka  watumishi wa TAMISEMI kujenga utamaduni wa  kufanya mazoezi wao pamoja na familia zao ili jamii yote iweze kuimarisha afya.

Amesema  utamaduni wa kufanya mazoezi ukijengeka siyo tu kwamba utasaidia kuimarisha afya bali utasaidia kupunguza gharama za kutibu magonjwa ambayo yanaweza kujitokeza kutokana na tabia bwete.

Pia Waziri Mchengerwa ametoa wito kwa watanzania kuwa na tabia za kupima afya zao badala ya kungojea hadi wanapoumwa.

Mbio hizo za pole zilizohudhuriwa na mamia ya watumishi wa TAMISEMI ziliishia katika jengo  la Ofisi ya TAMISEMI ambako kulikuwa na zoezi la upimaji wa afya kwa hiari.

Kwa upande mwingine, Mhe. Mchengerwa amesema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo na Wizara ya Elimu zinaratibu Mashindano ya Michezo kwa Shule za Msingi ( UMITASHUMTA) na Sekondari (UMISSETA) ambapo amefafanua kuwa mashindano hayo  yanasaidia kuibua vipaji vya wachezaji.

Amesema Serikali imeendelea   kuboresha  mashindano hayo ili kuwajengea utamaduni wa wanafunzi kufanya mazoezi  na kupenda michezo katika umri mdogo.






  


Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina amepongeza jitihada na maono ya Rais Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa miradi ya miundombinu na ya Kimkakati, akiahidi kuwa Benki hiyo itaendelea kuwa Mbia wa Serikali ya Tanzania, katika kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.

Rais Dkt. Adesina amebainisha hayo wakati wa mkutano wa hadhara wa Rais Samia Mkoani Dodoma leo Jumamosi Juni 14, 2025, muda mfupi mara baada ya Rais Samia kukagua utekelezaji wa ujenzi wa uwanja wa Kimataifa wa ndege Msalato pamoja na ujenzi wa barabara ya mzunguko wa nje wa Jiji la Dodoma yenye urefu wa Kilomita 112.3.

Katika salamu zake, Dkt. Adesina amemtaja Rais Samia kama Kiongozi wa mfano barani Afrika na duniani kote kutokana na namna ambavyo ameendelea kufanikisha maendeleo kwenye sekta mbalimbali nchini sambamba na jitihada zake katika kuimarisha utengamano wa Kikanda.

Dkt. Adesina ambaye Benki yake inafadhili pia ujenzi wa uwanja wa ndege Msalato pamoja na barabara ya Mzunguko Dodoma, ameeeleza kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi huo pamoja na mafanikio yaliyopatikana kwenye ujenzi wa reli ya kisasa SGR, akisema Benki hiyo itaendelea kushirikiana na  Tanzania katika kuendeleza shoroba zinazoanzia bandari ya Dar Es salaam na kuunganisha nchi nane zinazoizunguka Tanzania na zisizokuwa  na mlango wa bahari.

Kulingana na Rais huyo wa Benki ya Afrika anayemaliza muda wake, Benki hiyo imetoa zaidi ya Dola bilioni 9 za Marekani kwa Tanzania ambapo katika fedha hizo Dola Bilioni 4.73 zimetolewa katika kipindi chake cha uongozi, akiwa pia ndiye Rais pekee wa Benki hiyo aliyeitembelea na kufanya kazi na Tanzania kwa ukaribu zaidi tangu kuanzishwa kwa benki hiyo mwaka 1971.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka, Juni 12,2024 alifanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Mji Njombe na kueleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa kwenye miradi hiyo muhimu ya sekta ya elimu. 

Katika ziara hiyo, Mhe. Mtaka alitembelea ujenzi wa jengo la gorofa lenye vyumba 8 vya madarasa na ofisi 4 za walimu na matundu 4 ya vyoo katika Shule ya Sekondari Uwemba, mradi uliokadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi milioni 600 hadi kukamilika.Pia alikagua ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Wikichi unaotekelezwa kupitia programu ya SEQUIP kwa gharama ya shilingi milioni 583.

Mhe. Mtaka alitoa pongezi kwa Halmashauri ya Mji Njombe kupitia Mkurugenzi wake Bi.Kuruthum Sadick kwa kutenga fedha za mapato ya ndani ili kuendeleza ujenzi wa jengo hilo la gorofa, pamoja na kusimamia vizuri miradi yote inayotekelezwa. \n\nAidha, alisifu mafundi wanaotekeleza kazi hizo kwa weledi na kujituma kwao kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.

"Mkurugenzi umejionea mwenyewe namna mafundi walivyofanya vizuri kuanzia kwenye gorofa, tafuta namna tuwaite pamoja na bodi ya usajili wakandarasi na benki ili waweje kujisajili na tuhakikishe tunaendelea kuwapa kazi maana huu ni uaminifu mkubwa majengo kama haya ni mwanzo mzuri."Alisema Mhe.Mtaka.

Mradi wa ujenzi wa jengo la gorofa katika Shule ya Sekondari Uwemba uliibuliwa na wananchi wa kata ya Uwemba mwaka 2022 kwa kushirikiana na Mhe.Mbunge,Diwani na uongozi wa shule.Mradi huo unatekelezwa kwa fedha kutoka Serikali Kuu, michango ya wananchi na wadau wa maendeleo, mchango wa Mbunge wa Jimbo, pamoja na mapato ya ndani ya halmashauri.

"Leo tunaona matokeo ya uthubutu wa kuanza, leo tuna mradi wa kipekee ndani ya mkoa kuwa na jengo la gorafa  linalojengwa kwa nguvu za wananchi Halmashauri na serikali kuu,nakupongeza sana Diwani na wananchi wa Uwemba" Alisema


 


Waziri wa Ujenzi Mhe. Abdallah Ulega amesema dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kuwa foleni na msongamano wa magari Jijini Dodoma unapungua pamoja na kusisimua uchumi wa Mkoa huo kupitia huduma za usafiri na usafirishaji.

Mhe. Ulega amebainisha hayo leo Jumamosi Juni 14, 2025 wakati wa hotuba yake kwenye Mkutano wa hadhara wa Rais Samia, Nala Mkoani Dodoma, mara baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kimataifa Msalato pamoja na barabara ya mzunguko ya nje ya Jiji la Dodoma, akimshukuru kwa maelekezo na msukumu wake katika miradi ya ujenzi nchini.

Aidha Kando ya kupunguza msongamano, Ulega amebainisha kuwa barabara hiyo ya mzunguko wa nje ya Jiji la Dodoma yenye urefu wa Kilomita 112.3 itaongeza pia fursa za kiuchumj kwenye usafiri na usafirishaji, kukuza utalii mkoani humk pamoja na kuimarisha shughuli za kiuchumi ikiwemo shughuli za viwanda na Kilimo.

Amebainisha pia kwamba ni mpango wa serikali kupitia mkopo wa masharti nafuu wa Benki ya dunia, kuweza kupanua barabara ya Chamwino mpaka kwenye mzunguko wa barabara Kimbinyiko na kuwa na njia sita, ikiwemo mbili katikati kwaajili ya mabasi yaendayo haraka.

Aidha serikali ya awamu ya sita pia imepanga kupanha barabara ya Dodoma- Arusha kuanzia kwenye eneo la Njiapanda ya wajenzi hadi Njiapanda ya Msalato yenye urefu wa Kilomita 8.5 ambapo Waziri Ulega amemshukuru Rais Samia kwa kutoa kipaumbele kwenye utekelezaji wa miradi ya ujenzi.

Aidha katika kupunguza msongamano Jijini Dodoma, serikali pia inajenga barabara ya kutoka Uwanja wa ndege wa Kimataifa Msalato kupitia Mji wa serikali mpaka Ikulu ya Chamwino ili kurahisisha huduma za usafiri kutoka Ikulu na Mji wa serikali bila kulazimika kupita katikati ya Jiji hilo la Dodoma.

 


Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), ameshuhudia tukio la kumtunuku Dkt. Akinwumi Adesina, Rais anayeondoka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Shahada ya Heshima ya Uzamivu (Honoris Causa), iliyotolewa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam jana tarehe 13 Juni 2025, kwa kutambua mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Afrika katika zama za sasa.

Mhe. Dkt. Nchemba alisema kuwa heshima hiyo ni uthibitisho wa yale ambayo wengi barani Afrika na duniani wanayajua tayari kwamba Dkt. Adesina ni kiongozi mwenye maono, bingwa wa maendeleo, na mwana wa kweli wa Afrika aliyejitolea kubadili simulizi la bara hili na kwamba Tanzania inajivunia kuwa miongoni mwa mataifa yanayosherehekea mafanikio na urithi wake wa kipekee.

Alisema kuwa kupitia mpango wa Building a Better Tomorrow (BBT), Vijana katika Kilimo Biashara, Benki ya Maendeleo ya Afrika chini ya uongozi wa Dkt. Adesina imewezesha zaidi ya vijana 11,000 wa Kitanzania kuwa wajasiriamali wa kilimo. Kwa kuwapatia ardhi, pembejeo, na mikopo, mpango huu haukuwa tu ajira kwa vijana bali umeleta matumaini mapya vijijini kuwa ustawi unawezekana.

“Dhamira ya Dkt. Adesina kwa Tanzania pia ilidhihirika wakati wa janga la COVID-19, moja ya nyakati ngumu zaidi kwa dunia nzima, Chini ya uongozi wake, Benki ilitoa msaada wa kifedha wa takribani dola za Marekani milioni 50, uliosaidia serikali yetu kushughulikia dharura ya afya, kuendeleza uchumi, na kuwalinda wanyonge” alisema Mhe. Dkt. Nchemba

Alieleza kuwa athari za Dkt. Adesina hazikuishia Tanzania pekee bali aliongoza ajenda mpya ya maendeleo Afrika. Pamoja na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Benki ya Dunia, Bw. Ajay Banga, aliasisi Mkutano wa Nishati Afrika na kuanzisha Mission 300, lengo la kuhakikisha upatikanaji wa nishati kwa Waafrika milioni 300 ifikapo mwaka 2030.

“Katika majukwaa ya kimataifa, Dkt. Adesina amekuwa sauti ya kuaminika ya Afrika, akitetea upatikanaji wa fedha kwa mabadiliko ya tabianchi, usalama wa chakula, na usawa katika ushirikiano wa kiuchumi unaozingatia matarajio ya mataifa ya Afrika” alisisitiza Dkt. Nchemba

Alisema kuwa chini ya uongozi wake, Benki ya Maendeleo ya Afrika ilileta mtazamo mpya wa kugharamia miradi mikubwa yenye athari za moja kwa moja. Kinyume na mikopo ya awali iliyokuwa ikigusa maeneo mengi bila athari kubwa kwa watu, ambapo Dkt. Adesina alihakikisha miradi yenye tija inapata msukumo. 

Dkt. Nchemba alitaja baadhi ya  miradi inayofadhiliwa na AfDB hapa nchini kuwa ni pamoja na

 Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato, Dodoma

 Barabara ya Iringa – Dodoma – Babati

Barabara ya mzunguko wa mji wa Dodoma

 Mradi wa Maji safi na Usafi wa Mazingira (AUWSA – Arusha) uliowafikia zaidi ya wakazi 600,000 wa Arusha na Viunga vyake.

Katika sekta ya nishati, kuna miradi kadhaa ikiwemo Mradi wa Gridi ya Kaskazini Magharibi – (msongo wa kilovolti 400 kutoka Nyakanazi hadi Kigoma), ambao umeongeza uwezo wa gridi ya taifa katika mikoa ya Kigoma na Kagera.

 Na zaidi ya yote, usaidizi katika reli ya SGR – Lot 6 (Tabora–Kigoma), na Lot 7 (Uvinza–Musongati, Burundi hadi DRC).

“Dkt. Adesina, urithi wako unaacha funzo kwa taasisi zote za kimataifa – kuwa msaada kwa Afrika lazima uambatane na mipango ya kitaifa, usiwe wa masharti yasiyokubalika, na uzingatie miradi ya kimkakati yenye uwezo wa kubadilisha maisha ya watu. Sio mikopo ya “chapati na mandazi” inayoongeza madeni bila kuleta mabadiliko” aliongeza Dkt. Nchemba

Alisema kuwa ni jambo la heshima kubwa kuona Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, taasisi  ya elimu ya juu ya muda mrefu na inayoheshimika sana, kumtunuku shahada hiyo ya heshima ambayo ni ishara ya heshima ya kitaaluma, na shukrani kwa ubora, mshikamano wa Kiafrika, na uongozi wa kweli.

Alitumia pia fursa hiyo kumpongeza kwa dhati Rais mpya Mteule wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Raia wa Mauritania, Dkt. Sidi Ould Tah kwa kuchaguliwa Tarehe 29 Mei 2025, kuiongoza Benki hiyo kuanzia  mwezi Septemba 2025 na kumtakia mafanikio makubwa katika nafasi hiyo muhimu.







Na Oscar Assenga,TANGA

MWENGE wa Uhuru unatarajiwa kuwasili katika wilaya ya Tanga Jumatatu June 16 mwaka huu na upitia katika miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya Sh.Bilioni 3,058,289,671.99.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa taarifa za ujio wa Mwenge huo,Mkuu wa wilaya ya Tanga Dadi H.Kolimba alisema wataupokea ukitokea wilayani Mkinga katika uwanja wa shule ya Msingi Mabambani Mtaa wa Mpirani Kata ya Chongoleani.

Aliitaja miradi ambayo itapitiwa na Mwenge ni ujenzi wa madarasa 4 ya Ghorofa ,matundu 13 ya vyoo na ofisi, shule ya Msingi Mbuyuni yenye thamani ya sh. 388,769,596.80/= na Ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa ya awali ya mfano shule ya msingi Mwakidila yenye thamani ya sh. 70,100,000.00.

Mkuu huyo aliitaja miradi mingine kuwa ni ujenzi wa ofisi ya mtendaji kata ya Tongoni uliogharimu kiasi cha sh. 85,000,000.00, ujenzi wa barabara ya Sahare awamu ya kwanza na ya pili yenye urefu wa mita 600 kwa kiwango cha lami  Kwa thamani ya Sh 489,606,700/00.

“Lakini pia Mwenge utapita katika ujenzi wa Jengo la X-Ray kituo cha Afya Makorora wenye thamani ya Sh. 84,721,640/00 pamoja na mradi wa ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla awamu ya kwanza wenye thamani ya Sh. 1,872,091,735.00 “Alisema 
 
Hata hivyo alisema kwamba mradi mwingine ambao utapitiwa na mwenge ni mradi wa kikundi cha vijana cha kutengeneza gypsum wenye thamani ya Sh.68,000,000/-

Alisema mbali na miradi hiyo saba mwenge wa uhuru utakagua shughuli za maandalizi ya uchaguzi,  kongamano la vijana pamoja na maswala mtambuka.

Mwisho.

 


Na. Eva Ngowi na Chedaiwe Msuya – WF Arusha

Taasisi Nunuzi zashauriwa kuzingatia sheria, kanuni, miongozo iliyowekwa kwa mujibu wa sheria na kuwa na maadili ili kukomesha mambo ambayo ni kinyume na matarajio ya Serikali. 

Hayo yameelezwa na Kamishna wa Sera ya Ununuzi wa Umma, Dkt. Frederick Mwakibinga wakati wa Kongamano la tisa la Ununuzi wa Umma la mwaka 2025 linaloendelea katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa AICC jijini Arusha. 

Alisema kuwa uzingatiwaji wa Sheria utaweza kupunguza kiwango cha upotevu wa mali na kuchukua hatua ambazo zimewekwa katika Sheria ili kukomesha mambo ambayo ni kinyume na matarajio ya Serikali na kuhakikisha kwamba fedha za umma zinalindwa kadiri inavyowezekana. 

“Kama mnavyofahamu ununuzi wa umma ni moja kati ya nyenzo zinazotumika kwa manufaa mbalimbali ikiwemo kuutumia ununuzi wa umma kwa kuzinufaisha kampuni za wazawa ili ziweze kukua na kuwa na mchango katika maendeleo ya nchi, kuyajali makundi mbalimbali ya jamii ambayo yakiachwa bila kusaidiwa au kuwezeshwa yanapata ugumu katika ushindani wa soko la ununuzi wa umma.” Alisema Dkt. Mwakibinga


Dkt. Mwakibinga alisema, kongamano hilo muhimu limekutanisha, Wadau wa Ununuzi wa Umma kwa maana ya Watendaji wa Umma, Makampuni, Viongozi, Wafanyabiashara na watu mbalimbali ili kufanya majadiliano ya kujenga himaya ya Ununuzi wa Umma iliyo thabiti. 


Kongamano hilo limeandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma- PPRA, iliyobeba dhima ya “Ununuzi wa umma kidijitali kwa maendeleo endelevu: Ukuzaji wa Kampuni za Wazawa na Makundi maalumu kwa ukuaji wa Uchumi jumuishi. 



Kamishna wa Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Dkt. Frederick Mwakibinga, akizungumza kwenye mdahalo wakati wa Kongamano la tisa la Ununuzi wa Umma la Mwaka 2025, lenye kauli mbiu “Ununuzi wa Umma Kidigitali kwa Maendeleo Endelevu: Ukuzaji wa Kampuni za Wazawa na Makundi Maalum kwa Ukuaji wa Uchumi Jumuishi”, lililofanyika katika Kituo cha Kimatifa cha Mikutano (AICC) jijini Arusha.

Kamishna wa Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Dkt. Frederick Mwakibinga (katikati) na Maafisa Ugavi, Bi. Jamila Byekwaso (wa pili kulia), Bw. Raphael Chima (wa kwanza kulia), Bi. Vaileth Mwakajisi (wa pili kushoto) na Bi. Beatrice Zenda (wa kwanza kushoto), kutoka Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa Kongamano la Tisa la Ununuzi wa Umma la Mwaka 2025, lenye kauli mbiu “Ununuzi wa Umma Kidigitali kwa Maendeleo Endelevu: Ukuzaji wa Kampuni za Wazawa na Makundi Maalum kwa Ukuaji wa Uchumi Jumuishi” lililofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Kimatifa cha Mikutano (AICC) jijini Arusha.

Baadhi ya Washiriki kutoka Taasisi mbalimbali wakifuatilia Kongamano la Tisa la Ununuzi wa Umma la Mwaka 2025, lenye kauli mbiu “Ununuzi wa Umma Kidigitali kwa Maendeleo Endelevu: Ukuzaji wa Kampuni za Wazawa na Makundi Maalum kwa Ukuaji wa Uchumi Jumuishi” lililofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Kimatifa cha Mikutano (AICC) jijini Arusha.

Afisa Ugavi  Mwandamizi kutoka Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Jamila Byekwaso akizungumza na  Mkaguzi wa Ndani kutoka Bodi ya Huduma za Maktaba Tanzania, (TLSB) Bi. Rukia Amini wakati alipotembelea Banda la Wizara katika Kongamano la Tisa la Ununuzi wa Umma la Mwaka 2025, lenye kauli mbiu “Ununuzi wa Umma Kidigitali kwa Maendeleo Endelevu: Ukuzaji wa Kampuni za Wazawa na Makundi Maalum kwa Ukuaji wa Uchumi Jumuishi”, lililofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Kimatifa cha Mikutano (AICC) jijini Arusha.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini - Arusha)

NA DENIS MLOWE IRINGA 

MKURUGENZI wa Masoko na Uzalishaji wa kampuni ya VunjaBei Fadhili Ngajilo ametangaza nia ya kugombea ubunge jimbo la Iringa Mjini katika uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi.

Akizungumza na wanahabari mjini Iringa, Ngajilo ambaye ni Mwenyekiti wa Wazazi Mkoa wa Iringa ametangaza nia hiyo kwa kuweka vipaumbele 10 endapo atachaguliwa na wajumbe na kupewa nafasi ya kugombea jimbo la Iringa mjini.

Ngajilo ambaye ameshatia nia kupitia Ccm kwa miaka 3 katika miaka ya 2010, 2025 na sasa 2025 na kuleta upinzani mkubwa ndani ya chama katika kura za maoni katika jimbo la Iringa mjini ametangaza pia kupumzika kwa muda nafasi ya uenyekiti wa wazazi mkoa.

"Nimeandika barua kwa chama changu ya kupisha kwa muda nafasi yangu ya Mwenyekiti wazazi mkoa wa lringa ili kuruhusu vikao vikao vya uchaguzi viendelee kwa sababu mimi nimetia nia ya kugombea ubunge jimbo fa Iringa Mjini na ni matumaini yangu kuwa chama na wanachama wenzangu wa CCM wataniamini kuwa ninaweza kubeba majukumu, lakini pia ni matumaini yangu kuwa wananchi wa jimbo la Iringa mjini watanipokea na kunikubalia kuwa Mbunge wao kwa kipindi cha 2025 hadi 2030." 

Aliongeza kuwa Imani huzaa Imani kuamini katika uwezo wa kuongoza kutokana na makuzi na malezi mazuri niliyoyapata ndani ya CCM kwa za zaidi ya miaka ishirini huku akishika nafasi mbalimbali ndani ya CCM na serikalini.

 
Akitangaza sababu za msingi za kuweka nia ya kugombea ubunge Iringa Mjini kwa mwaka 2025 alizitaja kuwa kutimiza wajibu wa kikatiba wa kugombea na kuchaguliwa kwa kuwa sifa na nia zote anazo na kuwa mwakilishi wa wananchi bungeni.

Alisema lengo la kutia nia ni baada ya kubaini kuwa Iringa mjini inahitaji "voice of the people" (sauti ya watu) ambayo ikisema jambo bungeni au popote basi ijulikane kuwa Iringa imesema jambo na kuongeza kuwa vita vya kiuchumi zinahitaji watetezi na watu wenye uwezo wa kujenga hoja kuvutia miradi na uwekezaji katika sekta za viwanda, biashara, 

"Sauti hii inahitajika kuwaunganisha wana Iringa kwa rika, jinsia na imani zao yaani watoto, vijana, wazee, wanaume na wanawake mimi Ngajilo nimejipima nimeona hili naliweza na kama mjuavyo wote kuwa sisi wakazi wa lringa Mjini tuna shughuli za mbalimbali zikiwemo kilimo, biashara/ ujasiriamali tunahitaji sauti ya mtu atakayewaunganisha wakulima na kutimiza ndoto zao, vivyo hivyo kwa wafanyabiashara na wajasiriamali kama wauzaji masokoni, machinga, mama na baba lishe, maafisa usafirishaji kama bodaboda, bajaji, daladala na mawakala katika stendi zetu za mabasi, bila kuwasahau mafundi mbalimbali wa nguo, vifaa vya mbao,vipuri vya magari,. Alisema

Aliongeza kuwa Iringa mjini inahitaji kiongozi mbunifu, msikivu, mwenye upendo wa dhati na wana Iringa mzalendo na anayeweza kukaa na wana Iringa wakabuni na kupanga mikakati mbalimbali ya maendeleo katika sekta mbalimbali hivyo nimejipanga vilivyo kuwatumikia wananchi kwa moyo wa dhati, moyo wa utumishi na kuwa mtumishi wa watu (servus populi) endapo nitapewa ridhaa.

lringa Mjini imesheheni Vyuo vikuu ni mji wa vyuo vikuu inahitaji mbunge aliyejaa uelewa wa mahitaji ya vyuo vikuu na elimu. mbunge anayeweza kuwaunganisha wana vyuo kuweza kuwa na mchango wa kiuchumi na kijamii kwenye mkoa wetu wa Iringa kwa kuwa ujuzi wa kuishi na kustawisha vyuo vikuu.

Ngajilo aliongeza kuwa lringa Mjini inahitaji mtu anayeamini katika kuweka mifumo ya usalama wa wananchi wote 
wakiwemo watoto, wanawake, wazee na vijana kuna matukio ya unyanyasaji Kuvunja haki za wengine aidha kuna maeneo vibaka na wezi wameshamiri hivyo kwa umoja na jamii uwezo ninao na kuweza kuwaaunganisha wana Iringa kuzuia unyanyasaji na uhalifu kwa vitendo.


Vile vile alisema kuwq jimbo la Iringa mjini linahitaji kiongozi anayetambua maana ya kuweka mifumo ya burudani na michezo kwani kwa kipindi cha miaka 15 nimewaunganisha wadau wa sekta hiyo kwa kuendesha kombe la NGAJILO CUP (Vunjabei Cup) kupitia taasisi ya NGAJILO Foundation.

Alisema Iringa tunahitaji timu ya Ligi kuu hivyo nimejipanga na nina mikakati madhubuti ya kurudisha heshima ya Iringa katika medani ya michezo na kutambua uwepo wa makundi mengine ya burudani kama mabondia, madansa, wasanii.

Kigezo kingine ni Iringa Mjini bado tuna changamoto za miundombinu ya barabara hasa kata za pembezoni mwa manispaa yetu hivyo anahitajika mtu jasiri wa kusukuma agenda ya miundombinu ambapo yupo tayari kulipambania hili ili libakie kuwa historia. 

Akizungumzia Agenda ya utalii kwa Iringa ni muhimu sana kwa kuwa imezungukwa na vivutio vya utalii vingi kama Ruaha NP, Isimila S.A.S, Kalenga H.S, nk. Uwanja wa ndege mzuri, Hali ya hewa, makampuni ya utalii, ukarimu wa wana lringa ni vigezo tosha kuvutia watalii wa kitaifa na kimataifa kuja lringa kukumbusha kuwa Iringa mjini kuwa katikati ya mikoa na vijiji vingi fursa inayohitaji mtu mbunifu kuitumia ili kuwanufaisha wana lringa Mjini


Alimalizia katika huduma za afya na elimu, pamoja na kuendelea kuimarika kimiundombinu lakini changamoto ni nyingi kwenye utoaji wa huduma zinahitaji msukumo mpya kuhakikisha wana lringa Miini wanapata huduma bora kwa kuona hilo amejipima na kuona hii changamoto ipo ndani ya uwezo wangu.


Na Ferdinand Shayo ,Manyara


Kampuni ya kuzalisha vinywaji changamshi ya Mati Super Brands Limited yenye makao Makuu mjini Babati mkoani Manyara imetoa zawadi ya fedha Taslimu kwa madereva wa Bajaji waliobandika matangazo ya kinywaji cha Tanzanite Royal Gin kinachozalishwa na kampuni hiyo kama njia mojawapo ya kuunga mkono juhudi za vijana wanaojikwamua kiuchumi na kuiunga mkono kampuni hiyo ya wawekezaji wazawa.

Wakikabidhi zawadi kwa madereva wa bajaji ikiwa ni muendelezo wa kutoa zawadi baada ya Mkurugenzi wa Kampuni hiyo David Mulokozi kukabidhi zawadi ya Bajaji mpya kwa kijana aliyeweka picha yake na picha ya bidhaa ya Strong Dry Gin kwenye bajaji yake julai mwaka 2024.

Meneja Masoko wa Kampuni ya Mati Super Brands Limited Gwandumi Mpoma amesema kuwa kampuni hiyo itaendelea kutoa zawadi kwa madereva wa bajaji ambao ni wabunifu na wamekua wakiweka picha ya bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo katika bajaji zao kutokana na mapenzi mema waliyonayo kwa kampuni hiyo.

“Tumekua tukipishana na Bajaji zenye picha ya kinywaji cha Tanzanite Royal Gin hapa mjini baada ya kufuatilia kwa kipindi kirefu tumegundua hawa vijana wana damu ya Mati Super Brands Limited hivyo tutaendelea kuwaunga mkono kila mara ,tunatoa wito kwa madereva wengine kuendelea kutuunga mkono” Anaeleza Mpoma.

Meneja Chapa wa Kampuni ya Mati Super Brands Limited Izack Piganio amesema kuwa wamewakabidhi madereva wa bajaji fedha za mwezi mzima ambazo wamekua wakirejesha kwa wamiliki wa bajaji ili fedha wanazozipata wazitumie kwa maendeleo yao binafsi kama faida kwao .

Piganio amesema kuwa kampuni hiyo inatambua na kuthamini mchango wa madereva wa bajaji katika kutangaza bidhaa bora zinazozalishwa na kampuni hiyo zenye viwango vya kitaifa na kimataifa.











 


Na Munir Shemweta, WANMM NGARA

 

Tanzania na Rwanda zimetiliana saini Hati ya Makubaliano (MoU) ya Uimarishaji mpaka wa Kimataifa baina ya nchi hizo.

 

Makubaliano hayo yamefikiwa Juni 12, 2025 mara baada ya kukamilika kwa Kikao cha Kamati ya Pamoja cha Wataalamu (JTC) kati ya Tanzania na Rwanda kilichofanyia katika mji wa Ngara mkoa wa Kagera.

 

Utiaji saini makubaliano hayo umefanywa kati ya Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Hamdouny Mansour na Bw. Abel Buhungu ambaye ni kiongozi wa ujumbe kutoka nchini Rwanda

 

Akizungunza mara baada ya utiaji saini makubaliano hayo, Bw. Hamdouny Mansour, ameshukuru kwa hatua iliyofikiwa ya kutiwa saini makubaliano ya uimarishaji mpaka wa kimataifa kati ya Tanzania na Rwanda na kueleza kuwa, ni matumaini yake maazimio yaliyofikiwa yatatekelezwa kama walivyokubaliana.

 

Naye kiongozi wa ujumbe wa Rwanda ambaye ni Mkuu wa Ubalozi wa Rwanda nchini Sudan Mhe. Abel Buhungu ameshukuru serikali ya Tanzania kwa kuialika nchi yake kushiriki kikao cha pamoja cha uimarishaji mpaka wa kimataifa kwa nchi hizo mbili na kueleza kuwa, hana mashaka kwa kazi iliyofanyika muda si mrefu watafikia malengo yaliyokusudiwa.

 

Wakati wa kikao cha JTC wajumbe walipata fursa ya kukagua mpaka wa wa kimataifa wa Tanzania na Rwanda ambapo ukaguzi ulianzia katika alama ya mpaka ya Mafiga Matatu (Kasange) mahali ambapo mto Kagera/Akagera unakutana na mto Mwidu kisha kuelekea Rusumo mahali ambapo mto kagera unakutana na mto Ruvuvu/Ruvubu.

 

Lengo la ukaguzi wa mpaka ni kubaini hali halisi ya mpaka ulivyo, maendelezo yanayoyafanyika na yale yaliyofanyika pamoja na shughuli za kibinadamu zinazofanyika.

 

Mpaka wa Tanzania na Rwanda una urefu wa takriban km 230.

 

Zoezi la uimarishaji mipaka ya kimataifa ni utekelezaji wa makubaliano ya umoja wa Afrika kuwa ifikapo mwaka 2027 mipaka baina ya nchi za Afrika iwe imeimarishwa



Na Okuly Julius _ DODOMA


Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso, amekagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) na kukabidhi magari 19 kwa ajili ya ofisi za makao makuu na wilaya mbalimbali nchini.

Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo, Waziri Aweso alisema RUWASA ilianzishwa kutokana na changamoto kubwa ya upatikanaji wa huduma ya maji vijijini, jambo lililopelekea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, kuona umuhimu wa kuanzishwa kwa wakala huo.

“Leo hii suala la ujenzi wa miradi ya maji vijijini siyo tatizo tena. Namshukuru sana Rais Samia kwa kuwa ujenzi wa taasisi hii unaenda sambamba na mazingira bora ya kazi kwa watumishi,” alisema Waziri Aweso.

Ameeleza kuwa Rais Samia alitoa kiasi cha Shilingi bilioni 24 kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya RUWASA, na kupongeza juhudi hizo akisema: “Hakika Rais wetu ni mjenzi. Yote aliyotufanyia tutamlipa kwa kufanya kazi kwa bidii, kwani amefanya kazi kubwa katika utekelezaji wa miradi ya maji nchini.”

Ameongeza kuwa watahakikisha wanamfuatilia mkandarasi kwa karibu ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati, na fedha zitatolewa kwa wakati ili kuondoa changamoto au malalamiko yoyote.

“Ujenzi bora wa miradi ya maji unaendana na usimamizi makini na ufuatiliaji wa karibu. Nitahakikisha RUWASA wanapata ushirikiano wote wanaouhitaji ili kukamilisha yote waliyokusudia,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya RUWASA, Bi. Ruth Koya, alimshukuru Waziri Aweso kwa kuonesha uangalizi wa kipekee kwa taasisi hiyo, akisema magari 19 yaliyotolewa yataongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya RUWASA.

“Rais Samia Suluhu Hassan aliahidi kumtua mama ndoo kichwani na anaendelea kutekeleza hilo kwa vitendo. Waziri wa Maji naye anatekeleza wajibu wake kwa dhati. Magari haya yatasaidia kufanikisha lengo la Ilani ya CCM ya kuhakikisha huduma ya maji vijijini inafikia asilimia 85 ifikapo mwaka 2025,” alisema.

Katika kikao hicho, Mkuu wa Kitengo cha Ushauri Elekezi wa mradi huo, Bw. Peter Salyeem, aliwasilisha taarifa ya maendeleo ya ujenzi, akieleza kuwa mchakato ulianza Machi 2022 kwa maandalizi ya michoro, tathmini ya gharama na mazingira. Ujenzi ulianza rasmi Novemba 2023.

Alieleza kuwa mradi huo unagharimu Shilingi bilioni 24.9, huku gharama za ushauri elekezi zikiwa Shilingi milioni 499. Fedha zote zinatolewa na Serikali Kuu kupitia Wizara ya Maji.

“Mradi huu unahusisha ujenzi wa jengo kuu la ofisi ya RUWASA, kazi za nje, majengo saidizi kama mgahawa, kibanda cha mlinzi, jengo la jenereta pamoja na uzio wa eneo lote la kiwanja,” alisema.

Alibainisha kuwa mkandarasi wa mradi ni kampuni ya China Jiangxi International Economic and Technical Company Limited, huku mshauri elekezi akiwa ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA). Mradi huo unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 12, kuanzia Novemba 2023 hadi Desemba 31, 2024, na hadi sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji.

Naye Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kutoka RUWASA, Bw. Titus Mkapa, alithibitisha kuwa magari yaliyokabidhiwa ni 19 na yataelekezwa kwenye ofisi za makao makuu pamoja na wilaya ili kuongeza ufanisi wa shughuli za utoaji huduma za maji vijijini.




Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mh. Anthony Mavunde amezindua Ushirika wa waendesha Pikipiki na Bajaj Dodoma na kuwataka wasafirishaji hao kutumia fursa hiyo kujiimarisha kiuchumi kupitia mikopo mbalimbali.

“Ninawapongeza kwa uamuzi huu wa kuanzisha SACCOS yenu,ni wakati muafaka sasa kuwaona vijana mkimiliki vyombo vya usafiri vya kwenu wenyewe.

Kupitia SACCOS hii vijana wengi watabadilisha maisha yao na kujijenga kiuchumi.

Nitoe rai kwa viongozi wa SACCOS kuhakikisha mnatumia vizuri mkopo wa asilimia 10 wa mapato ya ndani ya Jiji la Dodoma ambapo mpaka sasa zimetengwa shilioni Bilioni 7 kwa ajili ya kukopesha vikundi vya wakina mama,vijana na watu wenye ulemavu”Alisema Mavunde

Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Alhaj Jabir Shekimweri anewataka maafisa wasafirishaji hao kutumia SACCOS kutatua changamoto za msingi za kiuchumi za vijana wengi na kuahidi kwamba serikali itakuwa nao bega kwa bega kuhakikisha inaweka mazingira rafiki ya ufanyaji wa shughuli zao.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma SACP George Katabazi amewataka maafisa wasafirishaji hao kuzingatia sheria za usalama barabarani na kwamba Jeshi la Polisi litaendelea kushirikiana nao kwa karibu kama wadau muhimu wa usalama katika jamii.

Akitoa shukrani zake Mwenyekiti wa UMAPIDO Ndg. Marwa Chacha Nyagate ameshukuru Mh. Rais Dkt. Sania S. Hassan kwa kuwajengea ofisi za chama hicho mkoani Dodoma na pia kumshukuru Mbunge Mavunde kwa mchango wa Tsh 15,000,000 kuiwezesha SACCOS yao kuanzishwa na kuahidi kwamba wataitumia SACCOS kuleta mageuzi ya kiuchumi kwa vijana wote waliopo kwenye tasnia hiyo.

Mwenyekiti Marwa pia alisisitiza umuhimu wa vijana hao kushiriki uchaguzi mkuu 2025 ili kutimiza takwa la kikatiba.

 


Serikali imetoa wito kwa wananchi kubadilika na kuwekeza katika bima ya afya kama njia ya kujiandaa na changamoto za kiafya, ikiwemo gharama kubwa za matibabu ya magonjwa kama saratani.

Wito huo umetolewa Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, alipokuwa akijibu swali la nyongeza kutoka kwa Mhe. Ester Matiko (Viti Maalum), ambaye alitaka kufahamu kama Serikali haioni haja ya kuweka kifurushi cha saratani kwenye bima ya afya ya chini ili kuwezesha wananchi wa kawaida kupata huduma, kutokana na gharama kubwa za matibabu ya ugonjwa huo.

Akijibu swali hilo, Dkt. Mollel amesema jamii inapaswa kubadilika na kuwekeza kwenye bima ya afya ili kuimarisha afya zao. 

"Watu wako tayari kuchangisha Milioni 100 kwa ajili ya harusi, lakini mtoto anapozaliwa hakuna anayechangia hata kwa ajili ya matibabu. Hii inaonyesha kwamba jamii inathamini sherehe kuliko afya,” amefafanua Dkt. Mollel.

Aidha, Dkt. Mollel amebainisha kuwa Serikali imetenga zaidi ya Shilingi Bilioni 200 kwa ajili ya msamaha wa matibabu, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha wananchi, hususan wasio na uwezo, wanapata huduma za afya bila vikwazo vya kifedha.

Naibu Waziri amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mifumo ya bima ya afya ili kuhakikisha huduma za afya, zikiwemo za magonjwa yasiyoambukiza kama saratani, zinapatikana kwa wote kwa gharama nafuu kupitia mfumo wa bima ya afya kwa wote unaotarajiwa kuimarika zaidi katika utekelezaji wa sera mpya ya afya.

Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Prof. Haruni Mapesa ameitaka Serikali mpya ya Wanafunzi wa Chuo (MASO), kuzingatia, kujifunza kwa weledi na kuyatumia mafunzo watakayoyapata katika semina elekezi ya kuwajengea uwezo ili wawe viongozi bora na wa kuigwa katika kipindi chote cha uongozi wao.

Hayo ameyasema Mkuu wa Chuo Prof. Mapesa   Wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo serikali mpya ya wanafunzi kwa mwaka 2025/26 yanayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kampasi ya Kivukoni.

Prof. Mapesa amesema mafunzo watakayoyapata wakayatumie  katika kufanya kazi kwa bidii  na kuendelea kuishi viapo vyao walivyoapa baada ya kuteuliwa kuongoza serikali ya wanafunzi wa chuo hicho.

“ Serikali ya wanafunzi (MASO) ni daraja kati ya wanafunzi na Menejimenti ya Chuo katika kuwasilisha maoni, kero, changamoto zinazowakabili wanafunzi hapa chuoni, hivyo mafunzo haya yatawajenga katika kutambua misingi ya sheria na taratibu za kufuata katika kuwasilisha mambo mbalimbali katika menejimenti”, Alisisitiza Prof. Mapesa.

Mkuu huyo wa Chuo pia  ameitaka Serikali ya wanafunzi kuwa mfano wa kuigwa kwa wenzao katika kuwashawishi kusoma kwa bidii ili kujiepusha na vitendo vya udanganyifu katika kipindi cha mitihani, kuwashawishi wanafunzi wenzao katika ulipaji wa ada pamoja na michango mbalimbali ya chuo, na kujiepusha na makundi ya migogoro katika muda wao ili waweze kuyafikia malengo ya kumaliza chuo kwa pamoja.

Baadhi ya mada zitakazowasilishwa ni pamoja na Dhana ya Uongozi na Utawala Bor. Kanuni, Taratibu na Matumizi ya Fedha za Umma. Migogoro, Utatuzi, na Wajibu wa Serikali ya Wanafunzi.

Mada nyingine zitakazowasilishwa ni Uongozi Bora, Maadili, Haki na Wajibu wa Kiongozi Bora, Mawasiliano na Matumizi ya Muda, na Kazi za Dawati la Jinsia.

Semeni hiyo elekezi kwa Serikali mpya ya Wanafunzi ni maalumu katika kuwajengea uwezo viongozi wa serikali hiyo ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi na weledi katika muda wote wa uongozi wao.


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano na Masoko

CHUO CHA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE

Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha mjini katika kuunnga juhudi za Rais awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo imefanikiwa kuanzisha mradi wa mgahawa ikiwa kama ni moja ya kitega uchumi kwa ajili ya kuweza kujikwamua kiuchumi pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba ya Katibu wa jumuiya hiyo.

Hayo yamebainishwa na Katibu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Cecilia Ndaru wakati wa kikao cha kikanuni cha baraza hilo ambacho kimeweza kukutana kwa lengo la kujadili masuala mbali mbali ya kimaendeleo, kujiandaa katika kuelekea uchaguzi mkuu, mapokezi ya Mwenyekiti wa UTW Taifa sambamba na kupokea taarifa ya utekelezaji wa ilani ya chama kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2020 hadi 2025 kutoka kwa madiwani wa viti maalumu.

Katibu Ndaru amesema kwamba lengo lao kubwa ni kuweka mikakati madhubuti ya kuendelea kubuni na kunzisha miradi mipya ambayo itaweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa jumuiya hiyo kuweza kujiongezea kipato pamoja na kuweka misingi imara ya kuweza kuimarisha jumuiya hiyo kuanzia ngazi za chini.

Katika kikao hicho cha baraza ambacho kilifunguliwa na Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Mwalimu Mwajuma Nyamka ambaye alikuwa mgeni rasmi amewataka wanawake hao kuhakikisha wanakuwa naa umoja na mshikamano hasa katika kioindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Nyamka katika baraza hilo amewahimiza wanawake kuchangamkia fursa za kugombea nafasi mbali mbali za uongozi ikiwemo katika nafasi ya udiwani pamoja na ubunge na kuwaomba wanampa kura nyingi za kishindo cha hali ya juu Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uchaguzi huo mkuu amebainisha kwamba lengo la chama ni kuhakikisha wanashinda katika nafasi zote.

"Nawapongeza sana wanawake wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini kwa kuweza kuchapa kazi kwa bidii na mimi nimefaarijika sana kuona meweza kusimamia vemaa utekelezaji wa ilani ya chama na pia mmeweza kuanzisha mradi wa mgahawa amabo utaweza kuwa ni chachu ya kujikwamua kuchumi sambamba na ujenzi wa nyumba ya katibu kwa hivyo kitu kikubwa mfanye kazi na viongozi ambao bado wapo madarakani achanane na kampeni amabzo hazina faida kwa kipindi hiki,"amebainisha Nyamka.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonja amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu kwa kuweza kutenga fedha nyingi ambazo zimekwenda katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, afya, maji,miundombinu ya barabara pamoja na huduma nyingine za kijamii.

Aidha Mgonja amemshukuru Mbungu wa Jimbo la Kibaha mjini Mhe. Silvestry Koka pamoja na mke wake Mama Selina Koka kwa kuweza kuwa mstari wa mbele kupambana katika kuwasaidia kwa hali na mali kufanikiwa ujenzi wa mradi wa mgahawa pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba ya katibu wa UWT kwa kushirikiana na wadau na viongozi wengine wa chama pamoja na jumuiya zake.

Naye mlezi wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini ambaye pia ni mke wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Mama Selina Koka amewahimiza wanawake wote kuwa na umoja na mshikamano hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuwaomba kuwa mstari wa mbele katika kupiga kura lengo ikiwa ni kuweza kushika katika nafasi zote za udiwani, ubunge, pamoja na nafasi ya urais.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka ambaye amefunga rasmi kikao cha baraza hilo ameishukuru kwa dhati jumiya hiyo ya wanawake kwa kuweza kumpa ushirikiano na sapoti kubwa katika kipindi chote ambacho aliingia madarakani na kuahidi kuendelea kushirikiano nao katika masuala mbali mbali ya kimaendeleo na kutatua changamoto ambazo wanakumbana nazo.

Koka amebainisha kwamba tangu aingie madarakani mnamo mwaka 2010 ameweza kuwa bega kwa bega na jumuiya ya UWT ambapo wameweza kushirikiana katika baadhi ya miradi mbali mbali ikiwemo ujenzi wa mradi wa nyumba ya Katibu pamoja naa kiteega uchumi cha mgahawa sambamba na kushirikishwa katika vikao mbali mbali vyebye kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo ikiwemo kutatua kero na changamoto za wananchi.



 


Wananchi wa Kijiji cha Mvuleni na vijiji vya jirani katika Kata ya Nyamato,Wilayani Mkuranga Mkoani Pwani wamenufaika na Huduma bora ya afya baada ya Ujenzi wa Kituo kipya cha Afya cha Mvuleni kilichogharimu Shilingi Milioni 559.

Kituo hicho kinachotoa Huduma za Wagonjwa wa nje,Huduma za Maabara,Upasuaji na Huduma za Uzazi, kimepunguza umbali kwa Wananchi kufata Huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Mkuranga.

Akizungumza wakati alipotembelea Kituo hicho,Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi Tanzania (UWT) Ndg. Zainab Khamis Shomari (MNEC) amewataka Wananchi wa Kata ya Nyamato  kuiunga Mkono Serikali ya Dkt. Samia Suluhu katika Juhudi zake za kuwaletea Maendeleo Watanzania.

"Katika maeneo yote tuliyozunguka tumekuta Vituo vya Afya,Zahanati na Maji Safi na Salama,hii ndio kazi inayofanywa na Serikali ya awamu ya Sita inayoongwa na Rais Samia Suluhu Hassan,lengo ni kusogea huduma muhimu kwa Wananchi"