Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Chande akijiandaa kupanda mti katika bustani ya miti akiashiria uzinduzi wa programu ya shule ya kutunza Mazingira katika Shule ya Bright African iliyopo Kivule, Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto ni Mbunge wa Jimbo la Ukonga Mhe. Jerry Slaa.


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Chande akizindua kibao cha kumbukumbu ya upandaji mti katika Shule ya Bright African iliyopo Kivule, Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto ni Mbunge wa Jimbo la Ukonga Mhe. Jerry Slaa.


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Hamad Hassan Chande akiwa na uongozi wa Taasisi ya Bright African Environment Development Group kabla ya zoezi la upandaji miti lililoandaliwa na taasisi hiyo mwishoni mwa wiki.

********************************

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Hamad Hassan Chande mwishoni mwa wiki ameshiriki katika zoezi la upandaji miti lililoandaliwa na Taasisi ya Bright African Environment Development Group na kusisitiza kuwa ni kitendo cha kuigwa na kupongezwa na hivyo kutoa rai kwa jamii kuiga mfano huo

Mhe. Chande ameupongeza uongozi wa Taasisi hiyo inayomiliki Shule ya Bright African kwa kusimamia mazingira kwa vitendo hasa uanzishaji wa vitalu vya miche ya miti na matunda kwa wanafunzi wake.

Amesema sasa hivi jamii inakabiliwa na changamoto ya uharibifu wa Mazingira ambao umechangia matatizo mengi yanayoathiri maendeleo ya nchi yetu ikiwa ni pamoja na upungufu wa umeme na mgao wa maji.

“Mmefanya jambo jema sana kuanza kuwapa ujuzi wanafunzi juu wajibu na umuhimu wa kutunza Mazingira. Hii ni jitihada inayopaswa kuungwa mkono na kujenga kizazi ambacho kinajua faida za kutunza Mazingira na kuepusha uharibifu wake” Chande alisisitiza.

Pia ameitaka Shule ya Bright African kushiriki katika programu mbalimbali za mazingira zinazoandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais ikiwa ni pamoja shindano linalohusisha Kampeni Kabambe ya Kitaifa ya Uhifadhi na Usafi wa Mazingira inayondeshwa na Ofisi yake ili kujifunza uhifadhi wa Mazingira.

“Serikali inafanya juhudi mbalimbali katika kuhifadhi Mazingira ili kuifanya nchi yetu iwe na mazingira mazuri yanayoweza kutupatia maendeleo endelevu” Alisisitiza Naibu Waziri Chande.

Taasisi ya Bright African Environment Development Group iliyopo Kivule Jijini Dar es Salaam imejikita katika kuwapa maarifa wanafunzi kwa vitendo katika uhifadhi wa mazingira kwa mujibu wa mitaala ya elimu. Shule hiyo ina miche ya miti takriban 3000 ambayo itapandwa katika eneo la shule na kila mwanafunzi atapaswa kuwa na miti miwili ya kutunza hadi atakapo hitimu shule.

Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: