Hayati Rais Dkt John Magufuli

Utangulizi

Wadau wa Sekta ya Asasi za Kiraia/Watetezi wa Haki za Binadamu tunapenda kutoa salamu za pole kwa Rais wetu, Mhe Rais Samia Suluhu kutokana na kifo cha aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

Aidha, kwa pamoja tumeendelea kuungana na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan pamoja, viongozi wengine wa serikali na watanzania wote kwa ujumla katika kuomboleza kifo cha Hayati Rais Magufuli. 

Wakati huo huo tunapenda kutumia fursa hii kumpongeza Mhe. Samia Suluhu kwa kupata nafasi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Mchango wa Hayati Rais Magufuli katika Maendeleo

Wadau wa Sekta ya Asasi za Kiraia kwa ujumla tutamkumbuka Hayati Rais Magufuli kwa jitihada kubwa alizozifanya katika kuleta maendeleo,kupiga vita rushwa, na ufisadi, kuweka nidhamu ya utumishi wa umma nk.  Tunatambua kuwa tangu mwaka 1995 alipochaguliwa kuwa Mbunge na baadae kuteuliwa kuwa Naibu Waziri, Waziri katika Wizara tofauti na baadae katika nafasi ya Rais,  Hayati Rais Magufuli alikua mstari wa mbele katika kupinga rushwa na kuleta uwajibikaji katika idara za umma. 

Aidha Hayati Mh. Rais alijitahidi kwa kiasi kikubwa kupigana vita dhidi ya umasikini na kuboresha miundo mbinu.

Tunatambua kuwa, kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kulikua na kilio kikubwa cha wadau wa Asasi za Kiraia kuhusu mambo kadhaa ikiwemo kukosekana kwa uadilifu katika sekta ya umma, utawala wa sheria, katiba mpya, haki za binadamu, umaskini miongoni mwa jamii, changamoto katika sekta mbalimbali kama elimu, afya, miundombinu na nishati.

Hayati Rais Magufuli alijitahidi sana kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto hizi pamoja na kwamba zipo changamoto ambazo zilikuwa zinaendelea kufanyiwa kazi.

 Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali ikiwemo Ilani za Uchaguzi za Vyama Vya Siasa na Asasi za Kiraia, yafuatayo ni baadhi ya mambo muhimu yaliyofanyika au kukamilika  katika kipindi cha uongozi wake katika kukuza uchumi wa kitaifa.

(i)     Kuendelea kuboresha utoaji na upatikanaji wa elimu kwa watoto. Utoaji wa elimu bure katika ngazi ya msingi ni hatua ya kupongezwa.

(ii)   Kuongezeka kwa vituo vya afya, zahanati na hospitali kutoka 7,014 mwaka 2015 hadi 8,446 mwaka 2020;

(iii) Kuongezeka kwa kiwango cha upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vya kutolea huduma za afya kutoka asilimia 42 ya mahitaji mwaka 2015 hadi asilimia 94.5 mwaka 2020;

(iv) Kukua kwa wastani wa pato la mwananchi kutoka shilingi 1,968,965 mwaka 2015 hadi shilingi 2,458,496 mwaka 2018, na Pato la Taifa limeongezeka kwa wastani wa asilimia 6.9 kwa mwaka.

(v)   Kuboresha miundo mbinu ikiwemo miundombinu ya nishati kama vile umeme wa mto Rufiji, barabara, reli, viwanja vya ndege na bandari.

 Haya yamefanyika kwa lengo la kurahisisha biashara na shughuli nyingine za kiuchumi kufanyika kwa urahisi na haraka.

(vi) Kuimarisha biashara kwa wafanyabiashara ndogondogo (wamachinga, mama lishe) kwa kuwaongezea unafuu wa kulipa ushuru wa Shilingi elfu 20 kila mwaka. 

Hali hii imechangia pia kurasimisha biashara hizi na kuongeza usalama wao ukilinganisha na hapo awali walipokuwa hawatambuliki na kunyanyasika sana.

(vii)                       Kufufua shirika la ndege la serikali (ATCL) kwa kununua ndege mpya kwa fedha taslimu. Hii ni hatua muhimu ambayo itatanua wigo kwa Watanzania kufanya biashara nje na ndani ya nchi pamoja na kupanua sekta ya utalii nchini.

(viii)                     Kudhibiti mianya mingi ya wizi na utoroshwaji wa mali na rasilimali za taifa kama vile madini. Jambo hili limepelekea ongezeko la pato la ndani la taifa. 

Kwa mfano katika kipindi cha miezi mitano ya kwanza ya mwaka 2018/2019 (Julai - Novemba), makusanyo ya ndani (ikijumuisha mapato ya Halmashauri) yalifikia TZS 7.37 trlioni sawa na 88.9% ya makadirio ya TZS 8.30 trilioni katika kipindi hicho. 

Mapato yameendelea kukua mwaka hadi mwaka kutokana na hatua stahiki zilizochukuliwa.

(ix) Kuongezeka kwa mapato yasiyo ya kodi – kutokana na kuimarishwa kwa ufuatiliaji kwenye taasisi, mashirika na kampuni kulikoiwezesha serikali kupata michango na gawio stahiki kutoka kwenye uwekezaji wake.

(x)   Kuimarika kwa matumizi ya technolojia katika ukusanyaji wa maduhuli kwenye wizara na idara zinazojitegemea kupitia Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato uitwao ‘Government Electronic Payment Gateway’ (GePG) ambapo kati ya Julai 2017 hadi Novemba 2018, jumla ya Taasisi za Serikali 325 zinatumia mfumo huu kukusanya maduhuli.

(xi) Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, kumekua na uongezeko la upatikanaji wa umeme kutoka megawati (MW) 1,308 mwaka 2015 hadi megawati (MW) 1,602.32 mwaka 2020. 

Pia, usambazaji wa umeme vijijini umeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka asilimia 16.4 mwaka 2015 hadi asilimia 67.1 mwaka 2020;

(xii)                       Kuimarisha juhudi za kutokomeza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake, watoto na wazee. Kutunga Sheria ya Msaada wa Kisheria ya Mwaka 2017 ilikua ni moja ya hatua kubwa kuhakikisha Serikali, Asasi za Kiraia na wadau mbalimbali wa haki za binadamu wanachangia katika kulinda na kutetea haki za binadamu.

(xiii)                     Uwepo wa utayari miongoni mwa wizara na idara mbalimbali za serikali kukutana na wadau wa Sekta ya AZAKI na kushirikiana nao kupunguza changamoto mbalimbali. 

Moja ya mikutano muhimu ni mkutano wa Januari 2021 uliokutanisha wadau wa AZAKI na Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ambao uliibua mambo mengi ya kufanyiwa kazi.

 Mikutano ya Kila Mwaka ya Wakurugenzi wa Azaki ambapo wageni rasmi wamekuwa ni Mawaziri. Mikutano mbalimbali ya Azaki kufunguliwa na Viongozi wa Serikali nk.

Haya ni baadhi ya mambo muhimu yatakayo kumbukwa na wadau wa sekta ya Asasi za Kiraia nchini. 

Haya mambo aliyoyatekeleza Hayati Rais Magufuli yanahitaji kusimamiwa na kulindwa kwa umakini ili tusirudi tulipotoka.

AZAKI tupo tayari kusaidiana na Mhe Rais Samia Suluhu Hassan kuendeleza haya mazuri aliyosimamia Hayati Rais Magufuli. 

 Kwa pamoja tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya HayatiRais Magufuli mahali pema peponi, Amina.

 

Pongezi kwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan

Kufuatia kuapishwa kwa Rais mpya wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, sisi wadau wa sekta ya Asasi za Kiraia tunapenda kutoa pongezi zetu za dhati kwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan. 

Tuna Imani kubwa naye kwa utendaji kazi uliotukuka katika kipindi chote cha uongozi wake katika nafasi mbalimbali alizoshika hapa nchini.

Itakumbukwa kuwa Mh. RaisSamia amekua mdau mkubwa wa sekta ya Asasi za Kiraia. 

Kabla ya kuingia kwenye siasa aliwahi kufanya kazi kwenye shirika la Association of Non-Governmental Organizations in Zanzibar (ANGOZA) pamoja na WorldVision. 

Na baada ya kuingia katika nafasi za juu serikalini, mara kadhaa amekua mstari wa mbele kushiriki katika makongamano na mikutano mbalimbali ya Asasi za Kiraia na taasisi za kiserikali. 

Haya yote ni baadhi tu ya mambo yanayoendelea kutupa imani kubwa katika nafasi yake mpya kama Rais wetu  na kwamba yeye ni mmoja wa viongozi wanaoijua vyema sekta hii ya Asasi za Kiraia.

Mnamo mwaka 2014 wakati wa mchakato wa kuandaa mapendekezo ya Katiba Mpya, Mhe. Rais Samia, akiwa kama Naibu Mwenyekiti wa Bunge la Katiba alikua mstari wa mbele kuongoza majadiliano kati ya wananchi, wabunge wa Bunge la Katiba na wadau mbalimbali ili tuweze kupata Katiba bora. 

Mara kadhaa alishiriki mikutano mbalimbali ikiwemo ile iliyoandaliwa na wadau wa sekta ya Asasi za Kiraia.

Katika nafasi mbalimbali alizoshika Mhe. Rais Samia amekua pia mstari wa mbele kufanya kazi na wadau wa Asasi za Kiraia katika kuhakikisha mambo mbalimbali muhimu kwa jamii yanatekelezwa. 

 

Miongoni mwa maeneo muhimu aliyosimamia moja kwa moja ni pamoja na uboreshaji wa vituo vya afya na huduma ya afya, huduma ya maji (maarufu kama kampeni ya ‘kumtua mama ndoo’), kuboresha hali ya lishe kwa wakina mama wajawazito, watoto chini ya umri wa miaka mitano, vijana balehe, na wazee, na kuzindua mradi wa kutokomeza unyanyasaji wa wanawake na watoto masokoni.

Pia amekua amekua akipambania kumuinua mwanamke kiuchumi pamoja na kuwa mlezi wa mabaraza ya kumuinua mwanamke kiuchumi.

Mwaka 2016, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe Ban Ki Moon alitangaza kuanzishwa kwa Jopo Kuu la Masuala ya Uwezeshwaji Wanawake Kiuchumi lilikuwa na jukumu la kuhamasisha hatua madhubuti za kuchukua katika kuleta usawa wa kijinsia, kutoa mapendekezo mahsusi ya utekelezaji wa malengo endevelu na hasa lengo namba 5 (kufikia usawa wa kijinsia; kuwawezesha wasichana na watoto) na lengo namba 8 (kuinua mustakabali wa kukuza uchumi na kuhakikisha ajira stahiki za kudumu). Aidha, Katibu Mkuu Mhe Ban Ki Moon alimteua Mhe Rais Samia akiwa Makamu wa Rais kuwa Mjumbe wa Jopo Kuu la Viongozi wa Dunia kama Mwakilishi wa Nchi za Afrika hivyo Mhe Rais wetu, Mhe Rais Samia anaouelewa mpana sana wa masuala haya ambayo ndio kilio cha watoto, vijana na wanawake nchini.

Si hivyo tu. Mhe. Rais Samia ameshiriki katika makongamano mengi yaliyoandaliwa na Asasi za Kiraia kwa lengo la kujadili na kuboresha upatikanaji wa haki za makundi mbalimbali katika jamii kama vile haki za Wanawake na watoto. Katika nafasi mbalimbali alizoshika na hata katika nafasi yake ya Makamu wa Rais, amekua akishiriki katika makongamano mbalimbali, mfano makongamano ya wanawake na makundi mengine katika jamii.

Miongoni mwa mikutano iliyoandaliwa na AZAKI aliyopata kuhudhuria ni pamoja na Ushiriki wake wa karibuni kabisa mnamo Tarehe 8 Machi 2021, aliposhiriki katika Maandhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mkutano ulioandaliwa na Asasi ya Mwanamke na Uongozi, na mkutano wa Mwanamke na Uongozi ulioandaliwa na Chama cha Waajiri nchini (ATE) Machi 4, 2021. 

 

Mikutano mingine aliyohudhuria ni pamoja na ifuatayo. Uzinduzi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Bara la Africa mwaka 2020 (African Women Leaders Network-AWLN), Maadhimisho ya Siku ya Wanawake mwaka 2019 (Mtandao wa Wanawake na Katiba),Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Chama cha Wanasheria Wanawake Nchini mwaka 2018 (Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania-TAWLA), Tamasha la 14 la Mtandao wa Kijinsia mwaka 2017 (TGNP), Maadhimisho ya Siku ya Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania mwaka 2017 (THRDC), naMkutano wa Watetezi wa Haki za Binadamu na Wabunge wa Bunge la Katiba mwaka 2014 (THRDC); na mikutano mingine.

Katika kushiriki mikutanoya AZAKI na kutoa ushirikiano kwenye kazi mbalimbali zinazoandaliwa na Asasi za Kiraia tunapata tumaini na nguvu kubwa ya kuimarisha utoaji huduma mbalimbali kwa jamii kupitia Asasi za Kiraia.

Yafuatayo ni baadhi ya maeneo ya muhimu ambayo sisi Wadau wa sekta ya Asasi za Kiraia tunatarajia kuendelea kuboresha na kufanya kazi karibu Zaidi na serikali ili kuhakikisha tunachangia katika mafanikio ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan:

(i)     Kuendelea kuchangia katika kukuza uchumi wa nchi kwa kuongeza fedha zinazotumika katika miradi mbalimbali. Katika taarifa iliyotolewa na Asasi za Kiraia katika wiki ya Asasi za Kiraia Novemba 7 mwaka 2019, mashirika 16 yaliyofanyiwa utafiti yalionyesha yameingiza nchini shilingi bilioni 236 katika kipindi cha miaka mitatu tu (2016-2018) kwa ajili ya kutelekeza miradi mbalimbali nchini.

(ii)   Kuboresha utendaji kazi wa Asasi za Kiraia na hivyo kuongeza tija katika utoaji wa huduma mbalimbali. Kwa mfano sisi wadau wa Asasi za Kiraia tutaendelea kusaidia katika kuongeza upatikanaji wa huduma muhimu za afya, elimu, maji na kadhalika.

(iii) Kuongeza miradi ya kibunifu na yenye tija kwa jamii na makundi mbalimbali kama vijana, watu wenye ulemavu, wanawake, watoto na wazee.

(iv) Kuongezauwezo wa kifikra na kiuchumi miongoni mwa wanajamii kupitia elimu na miradi mbalimbali ya kujenga uwezo itakayofanywa na  wadau wa Asasi za Kiraia

(v)   Kuchangia ongezeko la utawala bora katika taasisi za kiserikali kutokana na ufuatiliaji utakaoendelea kufanywa na Asasi za Kiraia na wadau mbalimbali wa utawala bora na haki za binadamu.

(vi)  Kuchangia kutokomeza umaskini nchini kupitia miradi mbalimbali ya AZAKI.

(vii)                       Kushirikiana na serikali kutoa huduma kwa maeneo mbalimbali

(viii)                     Kuweka mikakati na serikali ya namna ya kutoa ajira kwa maelfu ya vijana Tanzania.

(ix)    Kulinda Katiba, haki za binadamu na utawala bora

(x)   Kutoa msaada wa kisheria kwa wasiokuwa na uwezo wa kuweka wakili

(xi)  Kuendelea kuwa walipa kodi wazuri hapa nchini

(xii)                       Kufanya kazi zetu kwa uwazi na kwa weledi

(xiii)                     Kuishauri serikali katika mambo ya msingi yanayohusu usimamizi wa sekta ya AZAKI hapa nchini ikiwemo kuweka mazingira wezeshi ili sekta ya Asasi za Kiraia istawi kama ambavyo Ilani ya CCM 2020-2025 ilivyoahidi

(xiv)                     Kumshauri Mhe Rais Pamoja na serikali kuendelea kusimamia utumishi wa umma kwa ukakamavu mkubwa kwa mujibu wa taratibu na misingi iliyopo.

(xv)                       Kuendelea kuishauri maboresho ya sheria mbalimbali kandamizi ikiwemo namna bora ya kuimarisha utawala bora

(xvi)                     Kuendelea kuvishauri Vyama vya Siasa kuweka utaratibu wa kupata na kutambua Mwakilishi Bungeni wa Asasi za Kiraia (ikijumuisha mashirika ambayo sio ya kiserikali – NGOs) kama ambavyo Chama Cha Mapinduzi kilivyofanya na kuishauri Serikali kuwepo utaratibu wa kisheria wa kuitambua nafasi hiyo

(xvii)                   Kuendelea kuishauri serikali na wadau mbalimbali kuhusu kuboresha usawa wa kijinsia katika nafasi mbalimbali za uongozi.

(xviii)                 Kushauri viongozi, wadau mbalimbali na wananchi kuhusu mambo muhimu yatakayoweza kuboresha Amani ya taifa letu kwa mujibu wa Katiba na Sheri za nchi yetu.

Ni imani yetu kuwa kutokana na kazi kubwa aliyofanya Mh. Rais Samia katika nafasi mbalimbali alizoshika, ataendelea kutumia uzoefu wake na kwa kushirikiana na viongozi wengine walio chini yake katika kuhakikisha kuwa taifa letu linaendelea katika mwelekeo mzuri wa kimaendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii. Sambamba na hayo, ni matumaini yetu kuwa kadiri ambavyo ratiba yake itaruhusu, Mhe Rais Samia Suluhu Hassan atatupa fursa ya sisi kama wadau wa Asasi za Kiraia kukutana nae ili kupata dira na mahitaji yake ya namna bora ya kuendeleza na kuimarisha mashirikiano kati ya Asasi za Kiraia na idara mbalimbali za serikali.

Mwisho

Hongera Mh. Rais Samia Suluhu Hassan. Mungu akulinde na akuongoze.

Mungu Ibariki Tanzania.

Imetolewa leo tarehe 29 March, 2021

Na Asasi za Kiraia Tanzania 207 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar -------------------------------------------------------------

Mwandishi wetu alipompigia simu Mbunge wa Asasi za Kiraia(NGOs ) Mh Neema Lugangira alisema katika uandaaji wa tamko hili Mh Neema Lugangira (MB) amesema alishiriki kuanzia kutoa wazo,uandaaji wake hadi kukamilika

"Nikiwa kama Mbunge ninayewakilisha Asasi za Kiraia Bungeni kwa upande wa Tanzania bara nimefarijika sana kuona namna ambavyo wadau wa Asasi za Kiraia tumeweza kuja pamoja na tamko hili muhimu la Pole na Pongezi kwa Mhe Rais Samia Suluhu Hassani"Alisema Mbunge Neema Lugangira

"Lakini  nawashukuru sana wadau wa Asasi za Kiraia kwa kupokea wazo langu na kunipa fursa ya kuwa sehemu ya timu ya mchakato mzima wa uandaaji hadi kukamilika kwa tamko hili"Alisema Mbunge Neema Lugangira

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: