Katibu Tawala wa Wilaya  ya Liwale mkoani Lindi, Rajabu Kambangwa  akizungumza na wandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali nchini kuhusu mchango wa sekta ya misitu kwenye wilaya hiyo.
Afisa Sera na Majadiliano  wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA) Elida Fundi   akizungumza na waandishi wa habari walipokuwa kwenye ziara ya kuona namna Vijiji vya Darajani, Mihumo na Mtawatama zilivyofanikiwa katika jitihada za utunzaji shirikishi wa misitu.
Afisa Misitu wa Wilaya ya Liwale Nassoro Ali Mzui akizungumza na waandishi wa habari kuhusu jitihada wanazozifanya kwa kushirikiana na Serikali za vijiji na wadau wengine wa misitu kwenye ulizi shirikishi wa misitu.
Afisa Sera na Majadiliano  wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA) Elida Fundi akiwa kwenye picha ya pamoja na kamati ya maliasili ya kijiji cha Mtawatawa Wilayani Liwale.
 

Na Calvin  Gwabara, Liwale.


ZAIDI ya shilingi milioni 957 zimepatikana kwenye vijiji kutokana sekta ya misitu katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale mkoani Lindi na hivyo kuchangia katika kusaidia shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwemo elimu, afya na maji.

Hayo yamebainishwa na KatibuTawala wa Wilaya  hiyo,  Rajabu Kambangwa wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu mchango wa sekta ya misitu na ushiriki wa wilaya hiyo kwenye uhifadhi shirikishi wa misitu ya vijiji.

Alisema kuwa wilaya ya Liwale misitu ni chanzo kikubwa cha mapato ya wilaya kwani katika mwaka wa fedha wa 2019/2020 iliingizia serikali kiasi cha shilingi bilioni 2.6 ikifuatiwa na sekta ya kilimo na hivyo kuifanya sekta ya misitu kuwa sekta muhimu kwauchumi.

” Sisi kama wilaya tunanufaika sana na uwepo wa rasilimali hizi kwa hiyo tunafarijika sana ujio wa miradi kama huu ya Uhifadhi shirikishi wa misitu kwani inasaidia kuwajengea uwezo wananchi kwenye vijiji vyetu kuona umuhimu wa misitu na uhifadhi wake kwa maendeleo endelevu lakini kubwa zaidi kuona misitusi ya serikali bali ni mali yao” alisema  Kambangwa.

Katibu Tawala huyo alisema kwenye Kijiji cha Likombola pekee kiliingiza kiasi cha shilingi milioni 253 huku Kijiji cha Mtawatawa wakiingiza kiasi cha shilingi milioni 122 ambazo zimetumika kufanya shunguli mbalimbali za maendeleo kwenye vijiji hivyo ikiwemo kujenga vyumba vya madarasa, Zahanati, Nyumba ya Mtendaji wa Kijiji Pamoja naTrekta la Kijiji ambalo linawasaidia kwenye kilimo kwa kukodishiana  kwa gharama za chini na kwa wakati.

Alisema pamoja na mafanikio hayo makubwa lakini swala la uhifadhi bado linahitaji elimu kwa jamii maana Wananchi wasipoona faida za moja kwa moja kwenye vijiji vyao hawawezi kuitunza wala kuilinda na hivyo kusababisha misitu kupotea wakidhani ni mali ya Serikali.

Kwa upande wake Afisa Sera na Majadiliano wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA)Elida Fundi alisema kuwa vijiji vinafanyakazi kubwa na nzuri katika kuhifadhi misitu ya vijiji na hii inatokana na elimu na motisha wanayoipata kwenye vijiji vyao baada ya kuvuna misitu hiyo kwa uendelevu.

Alisema MJUMITA kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo na misitu wataendelea kushiriki kikamilifu kwenye kuzisaidia Halmashauri na vijiji katika awamu hii ya tatu ya mradi kuweka mipango bora yamatumizi ya ardhi na utengaji wa maeneo ya misitu ya hifadhi za vijiji ili itunzwe na kuvunwa kwa njia endelevu ambazo zitatunza misitu hiyo.

Kwa upande wake Afisa Misitu wa wilaya hiyo, Nassoro Ali Mzui alisema changamoto kubwa wanayokumbana nayo kwenye uhifadhi wa misitu hiyo ni vitendea kazi hasa vyombo vya usafiri kama pikipiki na zana zingine kwani misitu mingine inaukubwa wa zaidi ya hekta elfu 13 hivyo kuwawia vigumu kufanya doria na kuizunguka kwa miguu.

Alisema kwa kuwa vijiji vinachangia asilimia kumi ya mapato yatokanayo namisitu kwenda kwenye halmashauri wamekuwa wakifanya doria za pamoja na wanavijiji na kamati zao za maliasili za kijiji pamoja na maafisa wa maliasili na askari ili kusaidia kuongeza nguvu na kurahisha zoezi la ulinzi kwenye misitu hiyo.

Share To:

Post A Comment: