Watu watano akiwamo ofisa mtendaji wa kijiji cha Ulaya, wilayani Igunga mkoani Tabora,  Zablon Hussin wanashikiliwa polisi kwa mahojiano wakihusishwa na tukio la jengo la zahanati ya kijiji hicho kuungua moto.

Jengo hilo liliungua moto usiku wa Julai 14, 2018 na kusababisha hasara ya zaidi ya Sh85 milioni.

Akizungumza na wanahabari leo Jumamosi Julai 21, 2018  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley amesema majina ya watuhumiwa wengine wanaoshikiliwa yanahifadhiwa kuepuka kuharibu upelelezi.

"Wakati moto huo unazuka, zahanati ile haikuwa na mlinzi na tayari tumetoa maelekezo kwa viongozi wa Serikali za mitaani kuhakikisha maeneo yote ya umma yanakuwa na ulinzi," amesema Kamanda Nley.

Kaimu Mganga Mkuu wilaya ya Igunga, Dk Bonaventura Kalumbete amesema moto huo pia umeteketeza dawa na vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya Sh25 milioni.

Dk Kalumbete amesema juhudi zinaendelea kutafuta jengo jingine ili litumike kwa ajili ya huduma wakati mchakato wa ukarabati zahanati iliyoungua ukiendelea.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: