Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka wananchi wa wilaya hiyo kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (iCHF) ili kunufaika na matibabu nafuu na kupunguza mzigo wa gharama za huduma za afya katika ngazi ya familia.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika Kata ya Msasa, Mhe. Nyamwese amesema kujiunga na bima hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, ambao ni miongoni mwa ahadi alizoahidi kuzitekeleza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya siku 100 baada ya kuchaguliwa kwake.

Amesema iCHF imeendelea kuwa mkombozi kwa wananchi wengi kutokana na kuwezesha upatikanaji wa huduma bora kwa gharama nafuu, hivyo kutoa nafasi kwa familia kupanga matumizi mengine ya kimaendeleo.

“Afya bora ni nguzo muhimu ya uzalishaji. Kila kaya inapaswa kuwa na bima ili huduma za matibabu zipatikane kwa wakati bila kuathiri uchumi wa familia,” amesema.

Awali, akiwasilisha taarifa ya mapambano dhidi ya Ukimwi wilayani humo, Mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Joyce Gideon, amesema halmashauri inaendelea kufanya vizuri katika kuwafikia wananchi wanaoishi na VVU.

Amesema watu 205 waliobainika kuwa na maambukizi wameanza dawa za kufubaza virusi, huku asilimia 99 ya watu wanaoishi na VVU wakijua hali zao. Aidha, aliongeza kuwa asilimia 98 ya wanaotumia dawa hizo wana kiwango kidogo sana cha virusi mwilini, ishara ya mafanikio makubwa ya matibabu.

Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani 2025 yamefanyika yakiwa na kaulimbiu: “Imarisha Mwitikio, Tokomeza UKIMWI”.

Share To:

Alex Sonna

Post A Comment: