Na. James Mwanamyoto, OR-TAMISEMI


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-TAMISEMI (Miundombinu) Mhandisi Rogatus Mativila ameilekeza TARURA kuweka alama za vivuko vya watembea kwa miguu, barabara za pembezoni za watembea kwa miguu, taa za barabarani pamoja na za kuongozea magari kwa ajili ya usalama wa watumiaji wa barabara mpya ya mwangaza inayounganisha kisasa na medeli.

Mhandisi Mativila ametoa maelekezo hayo leo, alipoitembelea barabara hiyo na kubaini mapungufu hayo ambayo yanayohitaji maboresho kwa ajili ya kuimarisha usalama wa watumiaji wa barabara hiyo. 

“Nimetembelea barabara hii na kubaini hapa kwenye makutano ya barabara ya Mwangaza, Kisasa na Medeli kunahitajika maboresho ya kujenga vivuko, barabara za pembezoni, kuweka taa za barabarani na za kuongozea magari kwa ajili ya usalama wa watumiaji wa barabara hizi,” Mhandisi Mativila amesisitiza.

Mhandisi Mativila ameainisha kuwa, kuna maeneo ambayo watembea kwa miguu wamewekewa vivuko (zebra crossing) lakini hakuna sehemu za kusimama kabla ya kuvuka na za kuwavusha kwenda ng’ambo ya pili ya barabara.

Mhandisi Mativila amewataka TARURA kuweka kalavati kwenye mitaro iliyojengwa pembezoni mwa barabara ili kuwawezesha watembea kwa miguu kuvuka kwa urahisi ng’ambo ya barabara.

Aidha, ameitaka TARURA kuweka taa za barabarani (street light) na taa za kuongozea magari (traffic light) kwa ajili ya usalama wa watumiaji wa barabara kwani zimetengewa fedha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2024/25.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Mkoa wa Dodoma Mhandisi Edward Lemelo, amesema wamepokea maelekezo yote ya kuboresha barabara aliyoyatoa Mhandisi Mativila na kusisitiza kuwa, TARURA mkoa wa Dodoma  itaweka alama vya vivuko vya watembea kwa miguu katika barabara zote zilizokamilika ili kuimarisha usalama wa watumiaji wa barabara hizo.

Mhandisi Mativila amefanya ziara ya siku moja ya kukagua uimara wa barabara zilizojengwa na TARURA mkoani Dodoma, ambapo amezitembelea za Barabara za Mji wa Serikiali Mtumba, Barabara ya Nzuguni, Barabara ya Mwangaza, Barabara ya Swaswa Mpamaa, Barabara ya Mlimwa C, Barabara ya Chang’ombe, Barabara ya Mahakamani na Barabara ya Nala.

Share To:

Post A Comment: