Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe.Paul Christian Makonda amemfuta Kazi Mtendaji wa kata ya Mateves Bwana Muyayi Kivuyo kutokana na kushindwa kuwajibika na kusimamia miradi ya maendeleo kwenye kata yake pamoja na Kumdanganya hadharani Mkuu wa Mkoa.

Mhe. Makonda amefikia hatua hiyo leo wakati wa Mkutano wake wa hadhara wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi ikiwa ni maelekezo na maagizo ya Mhe.Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi aliyoyatoa wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa Mhe. Paul Christian Makonda ameiagiza taasisi ya udhibiti wa rushwa mkoani Arusha kufanya uchunguzi dhidi ya Ofisi ya Mtendaji huyo juu ya matumizi ya fedha zilizokuwa zimetengwa kwaajili ya ujenzi wa madarasa kwenye shule ya msingi Olmosu na Shule ya Sekondari ya Mateves.

Mkuu wa mkoa amesisitiza kuhusu uwajibikaji kwa Watendaji na watumishi wa Mkoa wa Arusha akiapa kutokuwa na utani na watendaji wazembe na waongo ambao wamekuwa wakiendelea kusababisha chuki kwa serikali na kujihusisha na vitendo vya wizi na ubadhirifu kwenye Ofisi zao wakati wa kuwahudumia wananchi.

Share To:

Post A Comment: