Ikiwa katika maandalizi ya kurejesha Minada ya Kimataifa ya Madini ya Vito na kuhakikisha inafanyika kwa tija, Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Naibu Katibu Mkuu Msafiri Mbibo umeendelea kujifunza kuhusu uendeshaji wa minada nchini Thailand na safari hii umejikita zaidi katika Mfumo wa uwezeshaji kifedha kwa wazalishaji wakati wa kusubiri minada.

Ujumbe huo umejifunza kuhusu uwezeshaji kifedha kwa wazalishaji wa madini ya vito kutoka kampuni ya Delgatto Capital DMCC yenye makao makuu yake nchini Marekani inayofanya kazi kwa kushirikiana na kampuni ya Bonas Group inayoendesha minada ya madini ya vito nchini humo.

Kampuni ya Delgatto imekuwa ikiwawezesha wachimbaji kupata fedha wakati wakingoja kufanyika kwa minada ili kuzalisha malighafi ambazo zinaingizwa katika minada bila kusitisha shughuli za uzalishaji na wakati huo wachimbaji wakiendelea na shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, kampuni hiyo imeanzisha huduma ya uwezeshaji kifedha katika siku za karibuni ili kujibu changamoto za wazalishaji wenye mitaji midogo waweze kuendelea kumudu gharama za uzalishaji wakati wakisubiri minada kufanyika.

Akizungumzia uzoefu huo, Naibu Katibu Mkuu Mbibo amesema ni nafasi nyingine kwa Tanzania kufahamu na kujifunza kuhusu mifumo mbalimbali inavyotumika katika uendeshaji wa minada hiyo hususan namna ambavyo wachimbaji wanaweza kushiriki na kuwezeshwa kifedha kupitia taasisi nyingine kwa ajili ya kuzalisha malighafi ya kulisha minada hiyo na kutumia nafasi hiyo kuwaalika watendaji wa kampuni hiyo kutembelea Tanzania.

‘’Hiki tulichojifunza leo ndicho tunachokitafuta kwa sababu wachimbaji wetu bado wana changamoto ya mitaji katika kuendesha shughuli zao, uzoefu wa kukutana na kampuni inayowawezesha wachimbaji wa vito vya thamani kupata fedha za kuzalisha malighafi wakati wakisubiri minada kufanyika ni jambo la muhimu kwetu na tunaiona ziara hii ni ya mafanikio,’’ amesema Mbibo.

Naye, Mkurugenzi wa Kanda wa Kampuni hiyo Rajiv Jain ameishukuru Wizara kumwalika ili kuanzisha ushirikiano wa kibiashara na Tanzania na kueleza kuwa, amefurahishwa na ujumbe wa Tanzania kutembelea kampuni ya Bonas Group ambayo imekuwa mshirika wa kibiashara na kampuni hiyo na kuongeza, ‘’nimeisikia Tanzania na kuiona katika taarifa mbalimbali kuhusu utajiri wake wa madini ya vito, hii ni fursa muhimu kwa kampuni yetu kushirikiana na Tanzania,’’ amesema Rajiv.

Wakati huo huo, Tanzania imeendelea kujifunza kuhusu uendeshaji wa miandaya madini ya vito kutoka kwa kampuni ya Bonas Group inayoendesha minada ya madini na imekuwa na uzoefu wa shughuli hizo kwa kipindi cha miaka 150 Sasa. Uzoefu huo kwa Tanzania unatarajiwa utaongeza tija kwa Wizara kuhusu namna ya kusimamia minada yake inayotarajia kuiendesha katika Mikoa ya Arusha, Dar Es Salaam na Zanzibar.

Tayari kampuni hiyo imeendesha minada ya vito kutoka kwa wateja katika nchi kadhaa duniani zikiwemo Brazil, Zambia, Ethiopia, Canada, Namibia, Siera Leone, Botswana na Msumbiji.

Bonas Group inautaja Bangkok kuwa kituo cha madini ya vito duniani na viwanda vingi vya uongezaji thamani madini vimeanzishwa nchini humo vikisanifu madini yenye thamani kubwa na imekuwa chaguo la kampuni nyingi na kueleza it wake kushirikiana na Tanzania.

Urejeshwaji wa minada ya madini ya vito na maonesho ya madini ni moja ya vipaumbele vya Wizara katika Mwaka wa Fedha 2023/24. Aidha, katika kuhakikisha suala hilo linatekelezwa, tayari Wizara imewasilisha Bungeni Muswada wa Marekebisho ya Sheria kuhusu uwepo wa Minada ya Madini ya Vito nchini.

Ziara hiyo ya mafunzo kuhusu minada ya madini ya Vito ni ya pili kwa Tanzania baada ya kwanza ambapo ujumbe wa Tanzania ulipata wasaa wa kujifunza namna ya kuendesha minada ya madini. Leo Februari 20, 2023 imepata fursa ya kujifunza kuhusu namna ya mifumo ya kifedha inavyofanya kazi katika uendeshaji wa minada hiyo.

Aidha, mbali na kujifunza kuhusu minada, ujumbe wa Tanzania unatarajia kushiriki katika maonesho ya Kimataifa ya 69 ya Bangkok Gems and Jewelry Fair yatakayofanyika nchini humo kuanzia tarehe 21- 25 Februari, 2024 ambapo pia wafanyibiashara na wachimbaji kutoka Tanzania wanatarajia kushiriki.

Share To:

Post A Comment: