MBUNGE wa Jimbo la Moshi vijijini wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro, Prof. Patrick Ndakidemi amewaomba viongozi wa chama kuwalinda viongozi waliopo madarakani ili waweze kutekeleza majukumu yao pamoja na ahadi walizoziahidi kwa wananchi.

Prof. Ndakidemi alitoa kauli hiyo jana wakati wa kikao cha halmashauri kuu ya CCM wilaya ya Moshi vijijini, ambapo alisema kuwa, ni jukumu la viongozi wa chama kuwalinda Madiwani na Wabunge waliopo madarakani kwa sasa watimize wajibu wao pamoja na kuwachukulia hatua wanachama ambao wameanza kujipitisha.

Alisema kuwa, muda wa kampeni haujafika kwa sasa ni muda wa kufanya kazi na kutekeleza Ilani ya uchaguzi kwa vitendo kwa maslahi mapana ya chama cha Mapinduzi.

Mbunge huyo alisema kuwa, katika kipindi cha miaka miwili na nusu ya serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia jimbo la Moshi vijijini limeshapokea zaidi ya Bilioni 42 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Hili halijawahi kutokea ni upendo wa Rais Samia kutoa fedha nyingi kwa ajili ya miradi mbalimbali ya jimbo letu ipo ujenzi wa hospitali ya wilaya ambapo ametoa Bilioni 2.9, upo mradi wa umwagiliaji Bilioni 5.1, mradi wa maji telamambe milioni 95” Alisema Prof. Ndakidemi.

Aidha Mbunge huyo aliwataka Madiwani kushikamana na kuacha kugawanyika kwani muda wa sasa ni wa kutekeleza kazi na kusimamia Ilani ya chama itekelezeke kwa vitendo.




Share To:

Post A Comment: