Na John Walter-Manyara
Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania TARI imekabidhi msaada ya pembejeo za kilimo kwa waathirika wa maafa ya maporomoko ya mawe na tope kutoka mlima Hanang hii leo Disemba 13, 2023.

TARI imekabidhi mbegu za Maharage kilo 400, Alizeti kilo 100 pamoja na mbegu za Ngano kilo 300 ili kusaidia wakulima ambao mashamba yao yameathiriwa na maafa hayo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi mbegu hizo Mkurugenzi wa Utafiti na Ubunifu,TARI Dkt.Furaha Mrosso ametoa salamu za pole kwa Serikali na waathirika wote wa maafa hayo huku akisema wameamua kuleta mbegu Daraja la msingi zenye ubora ili waweze kulima na kujipatia chakula kwa wingi.

“Tumetoa mbegu hizi ili kuleta nafuu kwa wakulima waliopata madhara ya maafa kutokana na uharibifu wa mazao uliosababishwa na maafa, tutaendelea kufanya hivi kadri inavyowezekana,” alieleza Dkt. Mrosso

Naye Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Ugani kutoka Wizara ya Kilimo Dkt.Upendo Mndeme, akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ameeleza kuwa, kwa kuzingatia madhara ya maafa hayo ikiwemo uharibifu wa mashamba hivyo wamechangia mbegu hizo zitakazozalisha haraka na kuendelea na shughuli zao za kila siku.

Akitoa neno la shukran mara baada ya kupokea msaada huo Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amewapongeza TARI kwa kuwashika mkono wakulima wa Hanang waliofikwa na maafa hayo na kueleza msaada huo utawafikia wote na kutumika kama ilivyokusudiwa.

Share To:

Post A Comment: