Na. Lusungu Helela- Dar es Salaam

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  Mhe.Ridhiwani Kikwete amewahakikishia Wajumbe wa Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi  Wakuu wa Kitaifa ya Baraza la Wawakilishi  Zanzibar  kuwa    Idara ya  Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa   ipo tayari kushirikiana na Ofisi ya Nyaraka Zanzibar ili kuhakikisha Ofisi hiyo inaboreshwa kwa maslahi mapana ya pande zote mbili  za Muungano.

Mhe. Kikwete ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Desemba 13, 2023 wakati akizungumza na Wajumbe wa Kamati hiyo  mara baada ya kutembelea   Ofisi ya Rais, Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Kanda ya Mashariki  iliyopo Jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kutunza na kuhifadhi nyaraka na kumbukumbu za Taifa.

Mhe. Kikwete amesema Taifa lolote lisilo na Kumbukumbu  ni Taifa lililokosa mwelekeo kwani halijui limetoka wapi na linaelekea wapi.

Kufuatia umuhimu huo, Mhe, Kikwete ameiahidi Kamati hiyo kuwa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa itatoa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha kumbukumbu na Nyaraka za Viongozi Wakuu wa Zanzibar zinatunzwa na kuhifadhiwa kwa maslahi mapana ya Taifa.

‘’ Tupo tayari kushirikiana nanyi ili kuhakikisha kumbukumbu na nyaraka za Waasisi wa Taifa letu zinalindwa na kuhifadhiwa kwa ajili ya kutusaidia kufanya maamuzi yenye muelekeo wenye maslahi kwa ajili ya  kizazi cha sasa na cha baadaye’’ amesisitiza Mhe. Kikwete.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu, Jamal Kassim Ali ameitaka ofisi ya Rais Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka kuunga mkono jitihada mbalimbali ili kuhakikisha kuwa Ofisi ya Nyaraka Zanzibar inaboreshwa.

Amesema kuwa ushirikiano kati ya Idara ya kumbukumbu na Nyaraka na Ofisi yanyaraka Zanzibar utasaidia sana kuratibu na kutunza nyaraka na kumbukumbu za taifa kwa ajili ya kizazi cha sasa na urithi wa vizazi vya baadae.

“Ofisi yetu bado ni changa, na hivi karibuni tunatarajia kuanza mchakato wa kutunza kumbukumbu za viongozi wa juu hasa waasisi wa Taifa, tunapoelekea kutimiza miaka 60 ya mapinduzi tunatarajia kuwa na namna ya utunzaji wa kumbukumbu za Rais Hayati Abeid Aman  Karume, hivyo tunaomba ushirikiano wenu wa hali na mali”.

Aidha, ameitaka Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka na Ofisi ya nyaraka Zanzibar kuhakikisha kuwa zinaweka mikakati ya kuhamasisha na kuuelewesha Umma umuhimu wa ofisi hizi ili kuzipa thamani inayoendana na kazi wanazofanya.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mheshimiwa Machano Othman Said amesema kuwa utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka za taifa ni shughuli muhimu sana katika maendeleo ya nchi.

Mhe. Machano  ameitaka Idara ya kumbukumbu kuendeleza ushirikiano na Ofisi ya Nyaraka Zanzibar katika maeneo ya elimu, vifaa pamoja na masuala ya kiutendaji na teknolojia.
Share To:

Post A Comment: