Na John Walter-Manyara

Jumla ya fedha zilizochangwa hadi sasa chini ya uratibu wa ofisi ya Waziri Mkuu kwa ajili ya maafa ya maporomoko ya tope, mawe na magogo wilayani Hanang' mkoani Manyara ni shilingi Milioni 138,645,500.

Fedha hizo zimepokelewa kwenye akaunti ya Mfuko wa Taifa wa Misaada ya Maafa (National Relief Fund) iliopo Benki Kuu ya Tanzania zikiwa ni kando ya zile alizokadhibiwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, zilizochangwa na mashirika ya umma kiasi cha shilingi bilioni mbili (sh. 2,000,000,000/-). 

Kwa mujibu wa msemaji ya mkurugenzi wa idara ya habari maelezo na msemaji mkuu wa serikali Mobhare Matinyi, hadi sasa fedha 

zote zilizochangwa kupitia mfuko huo ni shilingi 2,138,645,500/.

Aidha Vifaa mbalimbali vya misaada vilivyotolewa ni pamoja na chakula mahindi kilo 47,627; maharage kilo 8,692; unga wa sembe kilo 37,745; unga wa ngano kilo 13,800; mchele kilo 39,330; mafuta ya kupikia lita 12,290 na sukari kilo 12,954.

Vifaa vya malazi magodoro 1,920; mahema ya familia 5; mabegi ya kulalia 600; mashuka 2,559 na maduveti 170. 

Vifaa vingine  ni ndoo za lita 10 jumla 1,485; ndoo za lita 20 jumla 331; madumu ya lita 10 jumla 240; madumu ya lita 20 jumla 141; mabeseni 720; pamoja na nguo za kike na za kiume, vyombo vya chakula, mataulo ya kike na vifaa vya uokozi kama tochi, majembe, buti za mvua, matoroli na glovu.

 Aidha, Serikali  imeshapokea mabati 5,200 ya kuwasaidia waathirika kujenga makazi mapya.

Serikali inaendelea kuwashukuru na kuwapongeza Watanzania pamoja na taasisi mbalimbali za umma na binafsi ndani ya nchi yetu kwa moyo wa utu na uzalendo. 

Misaada mbalimbali ya vitu na fedha inaendelea kupokelewa na taarifa yake itatolewa. 

Serikali inatoa wito kwa wanaojitolea kufanya hivyo kuleta vifaa vya ujenzi pale inapowezekana ili visaidie waathirika kuanzisha makazi mapya. 

Kamati ya Maafa ya Taifa iliyo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, imetangaza akaunti ya benki ya kuwekea fedha kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa  Maafa Na. 6 ya mwaka 2022. 

Akaunti hiyo ya kielektronikia inaitwa National Relief Fund - Na. 9921159801. Akaunti hii ina swift code TANZTZTX kwa wanaotuma fedha kutoka nje ya nchi. 

Taarifa ya msemaji mkuu wa serikali imebainisha kuwa Miamala inapotumwa inatakiwa kuwa na maelezo MAAFA HANANG. 

Akaunti hiyo inayopokea michango ipo Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na inapokea fedha kutoka ndani na nje ya nchi.

Share To:

Post A Comment: