Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Nelson Mandela ya Sayansi na Teknolojia Bw. Omari Issa ametoa rai kwa wanawake kujiunga na masomo ya Shahada ya Umahiri na Uzamivu kwa wingi ili kuleta uwiano wa idadi ya wahitimu Wanawake na Wanaume kwenye fani mbalimbali.


Mkuu huyo wa Taasisi Bw. Omari ameyasema hayo Agosti 31, 2023 wakati wa mahafali ya 9 ya kutunuku Shahada ya Umahiri na Uzamivu kwa wahitimu 89 wa Taasisi hiyo.

"Kauli mbiu yetu ni taaluma kwa jamii na viwanda hivyo tutazidi kuongeza ushirikiano wa karibu sana na wadau katika viwanda ili wahitimu wetu waweze kubiasharisha tafiti zao ziweze kuingia sokoni na kuifikia jamii” alisema Mkuu wa Taasisi Bw. Omari Issa

Ameongeza kuwa Taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali pamoja na wadau mbalimbali ili tafiti zinazozalishwa na wataalamu katika taasisi hiyo ziweze kuifikia jamii na kutatua changamoto mbalimbali.


Naye Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Bw. Sylvester kazi amewataka wahitimu hao kuendelea kuwa waadilifu kwa kufanya kazi kwa karibu na jamii ili taaluma waliyoipata katika taasisi iweze kuleta matokeo chanya katika kukuza uchumi wa nchi.

Kwa Upande Wake Makamu Mkuu wa Taasisi Professa Maulilio Kipanyula, ameeleza kuwa taasisi hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kufanya tafiti zinazoigusa jamii moja kwa moja.

"Taasisi yetu ina kituo cha atamizi ambacho kinafanya kazi kubwa ya kuatamia bunifu mbalimbali ambacho pia kitasaidia katika kuatamia bunifu kutoka katika jamii inayotuzunguka ” alisema Professa Maulilio Kipanyula

Katika mahafali hayo ya 9 jumla ya wahitimu 89 wametunukiwa Shahada za Umahiri na Uzamivu ,huku Shahada ya Umahiri (Master's Degree) wakiwa 62 na Shahada ya Uzamivu ( PhD) wakiwa 27.


 Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Nelson Mandela ya Sayansi na Teknolojia Professa Maulilio Kipanyula akiongea wakati wa sherehe za Mahafili ya Tisa ya taasisi hiyo yaliyofanyika Agosti 31, 2023.
 Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Nelson Mandela Ya Sayansi na Teknolojia Bw. Omari Issa(aliyeshika kofia) akimtunuku Mhitimu wa Shahada ya Uzamivu katika Mahafali ya Tisa ya taasisi hiyo yaliyofanyika Agosti 31,2023 kampusi ya Tengeru Arusha.



Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi ya Afrika Ya Nelson Mandela ya Sayansi na Teknolojia Bw. Sylvester Kazi ( kwenye Podiamu) akiongea na wahitimu wakati Mahafali ya Tisa ya taasisi hiyo yaliyofanyika Agosti 31,2023 kampusi ya Tengeru Arusha, waliokaa wa kwanza kuhoto ni Mkuu wa Taasisi Bw. Omari Issa, Makamu Mkuu wa Taasisi Professa Maulilio Kipanyula ( wa pili kushoto ) na Naibu Makamu Mkuu wa Taasisi Taaluma, Utafiti na Ubunifu Professa Anthony Mshandete.

 Mlau Kutoka Taasisi ya Afrika ya Nelson Mandela ya Sayansi na Teknolojia Professa Gabriel Shirima akiongoza maandamano wakati wa hafla ya Maafali ya Tisa ya Taasisi hiyo yaliyofanyika Agosti 31, 2023 Kampusi ya Tengeru Arusha.
Share To:

Post A Comment: