NA DENIS CHAMBI, TANGA.

ASILIMIA 60 ya ukatili wa kijinsia  kwa watoto hapa nchini umebainishwa kutekelezwa ndani ya familia na ndugu wa karibu wakiwemo wazazi huku asilimia 40  ukifanywa nje hii ni kulingana na utafiti uliofanywa na  serikali kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la kuhudumia watoto UNICEF.


Hayo yameelezwa na naibu katibu mkuu kutoka wizara ya maendeleo ya jamii jinsia wanawake na makundi maalum Amon Mpanju wakati akifungua semina kwa viongozi wa dini kanda ya kaskazini mkoani Tanga  kuhusu muongozo wa malezi kwa wazazi na malezi ya watoto kwa mwaka 2023 ambapo amesema kuwa viongozi wa dini wana nafasi kubwa katika kuwaelekeza wazazi,  kukemea na kupunguza  migogoro mbalimbali inayotokana na ndoa ambayo kwa kiasi kikubwa inachangia ukatili ndani ya familiya kwa watoto. 

"Ongezeko la mmomonyoko wa maadili imeathiri sana watoto na kwa mujibu wa  utafiti uliyofanywa  na serikali pamoja na shirika la kimataifa la kuhudumia watoto la UNICEF ulionyesha kuwa ongezeko kubwa  la vitendo vya ukatili majumbani  60% hufanywa na watu wa karibu wakiwemo wazazi , 40% ni nje ya nyumba  zetu na utafiti huu ulionyesha  wanaofanya vitendo vya ukatili  ni ndugu na jamaa ndani ya familiya"

"Serikali baada ya kuona tunayo changamoto hiyo ya mmomonyoko wa maadili,  malezi kwa watoto migogoro ya ndoa mapenzi ya jinsia moja  na sio sehemu ya  sheria zetu za nchi wala mila na desturi zetu hazitambui ndio tukasema kwa kushirikiana na wadau tutengeneze muongozo wa kitaifa  wa malezi kwa wajibu wa wazazi na walezi kwa malezi ya watoto na  familiya  kwa mwaka huu wa 2023  tukasema viongozi wetu wa dini muweze kutusaidia tuungane kuweza  kupeleka elimu sahihi  na kukumbushana wajibu  wa wazazi na walezi kwa watoto na familiya" alisema Mpanju.

Alisema kuwa muongozo huo umesimamia katika kuwaelekeza wazazi na walezi kuwajali watoto kuhakikisha wanapata mahitaji yote ya msingi  yanayolenga kumkuza na kumwendeleza mtoto  katika nyanja zote za kielimu kimalezi mpaka atakapofikia utimilifu wake wa kiakili pamoja na kumlinda dhidi ya ukatili wa kijinsia kuanzia majumbani ,  mashuleni na katika mazingira yoyote yanayomzunguka.

Mkurugenzi anayesimamia maswala  ya watoto kutoka  wizara ya maendeleo ya jamii  jinsia wanawake na makundi maalum ,  Sebastian Kitiku alielsza kuwa zipo changamoto mbalimbali zinazochangia mmomomyoko wa maadili kwa watoto hapa nchini ikiwemo mogogoro ya ndoa  baina ya wazazi,  muingiliano wa  mila tamaduni na desturi za kigeni  pamoja na maendeleo ya teknolojia.

"Bado kuna changamoto mbalimbali katika malezi ya watoto hasa ambazo wizara imezibaini ikichangiwa na migogoro ya ndoa baina ya wazazi ,  muingiliano wa mila na desturi za kigeni maendeleo ya teknolojia  kuwapa uhuru sana  watoto ,  wazazi wengi kuwakabidhi watoto kwa watu wengine wawalelee hizi ni miongoni mwa sababu ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa  kukosekana kwa malezi bora kwa mtoto" alisema Kitiku.

Viongozi wa dini wamefurahishwa na ujio wa mwongozo huo wa kitaifa juu ya malezi ya watoto ambapo licha ya jitihada mbalimbali zinazoendelea kutumika ikiwemo majukwaa ya kidini inaonekana kuleta mabadiliko ya kizazi cha baadaye kama tu mwongozo huo utatekelezwa kikamilifu.

Juma Ruhuchu ambaye ni Sheikh mkuu wa mkoa wa Tanga alisema " Wito wangu kwa wazazi na walezi ni kwamba wajitahidi katika maswala mazima ya malezi kwa watoto kwa sababu malezi mazuri kwa mtoto yatakuja kutufanya tupate taifa zuri la watu wazima wa baadaye hivyo tuwalee katika maadili ya kidini na ya kitanzania"

Padre Moris Mwambashi wa kanisa katoliki jimbo la Tanga alisema " katika semina hii ambayo inatoa muamko kwa wazazi na walezi katika sehemu zote zile wawe macho kuhakikisha watoto hawaingii katika wimbi la kurubuniwa na maswala ya utandawazi"

Mkurugenzi anayesimamia maswala  ya watoto kutoka  wizara ya maendeleo ya jamii  jinsia wanawake na makundi maalum ,  Sebastian Kitiku akizungumza katika semina ya viongozi wa dini kanda ya kaskazini kuhusu muongozo wa malezi kwa wazazi na malezi ya watoto kwa mwaka 2023 uliofanyika jijini Tanga july 32,2023,

Baadhi ya viongozi wa dini mbalimbali wakifwatilia semina inayohusu muongozo wa malezi kwa wazazi na malezi ya watoto kwa mwaka 2023 inayofanyika mkoani Tanga kwa siki 4

Sheikh mkuu wa mkoa wa Tanga Juma Ruuchu akizungumzia kuhusu muongozo wa kitaifa wa malezi ya mazi na mlezi kwa watoto wa mwaka 2023.
Padre Moris Mwambashi wa kanisa katoliki jimbo la Tanga akizungumzia kuhusu muongozo wa kitaifa wa malezi ya mazi na mlezi kwa watoto wa mwaka 2023.





Share To:

Post A Comment: