Na; Elizabeth Paulo,Dodoma

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mheshimiwa Rosemary Senyamule ametoa rai kwa wananchi wa mkoa huo na Watanzania kwa ujumla kushiriki katika wiki ya Ubunifu ambayo kitaifa yanafanyika mkoani Dodoma katika viwanja vya Jamhuri.

Senyamule ametoa rai hiyo alipokua akizungumza katika viwanja hivyo mara baada ya kuzunguka mabanda ya washiriki wabunifu waliofika kuonyesha ubunifu wao.

Senyamule ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Taasisi zilizo chini yake kwa kuandaa maonyesho ya Wiki ya Ubunifu inayowakutanisha wabunifu mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi.

“Wabunifu hakikisheni bunifu zenu zinaingia sokoni kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii kwani nimetembelea mabanda Yenu, zinatosha kabisa na zinakidhi katika soko la ushindani”.Amesema Senyamule

Katika hatua nyingine amesema kuwa Mafunzo ya Ufundi Stadi ni zao Zuri la ajira kwa vijana kwani mafunzo hayo hutolewa kwa vitendo na linatoa vijana waliotayari kwa ajili ya kujiajiri na kuajiriwa.

"Mfano nilivyoona leo pale kwenye banda la VETA wamebuni Miwani maalumu ambayo inasaidia kumkumbusha dereva usalama wake awapo barabarani kwa mfano anaposinzia inasema na wengine wametengeneza gari linalotumia Sola (umeme wa jua) ubunifu huo utasaidia kupungunguza gharama za mafuta na ndio maana nawaomba sana hizi bunifu ziingizwe sokoni mapema,"Amesema na Kuongeza

 "Nimeambiwa maonesho haya yamekuwa yakifanyika kila mwaka na kwa mwaka huu yamepiga hatua kwa kuwa yamekuwa halisi, leo tunaona bunifu za vijana ambazo zinaingia sokoni," amesema Senyamule

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu Prof.Maulilio Kipanyula amesema kuwa Maonesho ya wiki ya Ubunifu mwaka 2023 yamekuwa tofauti kwani imeanzi katika ngazi za mikoa na huko wabunifu walianza kuonesha bunifu zao katika ngazi hizo na sasa maonesho hayo yamefikia katika ngazi ya taifa hivyo imewapa nafasi wabunifu wengi kuonesha bunifu zao.

Prof. Kipanyula ameongeza kuwa katika maonesho hayo kutakuwa na siku maalumu kwaajili ya Taasisi za VETA na Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC)

"VETA leo wameonesha bunifu zao na ndio maana leo ni VETA DAY dhumuni ni kuona ni namna gani uwekezaji uliofanywa na Serikali ya awamu ya sita katika elimu ya ufundi imefanyiwa kazi na kuzalisha wabunifu wenye uwezo wa kuigiza sokoni bunifu kwa ajili ya kutatua changamoto za jamii,"

Na kuongeza kuwa "kwa upande wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) nao watakuwa na TAEC DAY ambapo dhumuni la siku hiyo ni kuifanya Tume hiyo ijulikane na wananchi ,majukumu yake ni yapi, nini faida yake na mengine mengi ambayo yataelezwa.

Prof.Kipanyuka amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo ili kujionea bunifu mbalimbali ambayo zimebuniwa na wabunifu wa ndani huku ikichagizwa na wabunifu kutoka nchini Afrika Kusini kwani lengo la serikali na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ni kuifanya wiki ya Ubunifu Tanzania kuwa ya kimataifa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mafunzo ya Ufundi Stadi -VETA Ndg.Abdallah Ngodu amesema kuwa maonesho ya wiki ya Ubunifu kwa mwaka huu yamekuwa tofauti sana kwani wamepewa nafasi ya kuwa na siku maalumu kwa ajili ya VETA ambayo imekwenda kwa jina la "VETA DAY"

Ngodu ameongeza kuwa VETA DAY imetumika kutoa vyeti pamoja na zawadi kwa baadhi ya wabunifu ambao bunifu zao zimeshindanishwa na kukidhi viwango walivyokuwa wameweka na hayo yanafanyika kwa lengo la kuhamasisha vijana wengi kujiunga na mafunzo ya ufundi Stadi ambayo yanafundishwa kwa vitendo zaidi kuliko nadharia.

Pia amewataka wananchi kujitokeza na kuja kujione banifu mbalimbali kutoka VETA na kujiunga kwa ajili ya kupata Mafunzo mbalimbali ya ujuzi lwa ajili ya kuwatengenezea mazingira mazuri ya kujiajiri na kuajirika.








Share To:

ELIZA DOM

Post A Comment: