Jeshi la polisi mkoani Arusha leo limeungana na wadau wengine ikiwemo Chuo cha ufundi Arusha pamoja Chama cha Mawakala wa waongoza Utalii nchini (TATO) kutoa mafunzo kwa madereva wa magari ya watalii katika kuelekea msimu wa utalii (high season).

Mkuu wa usalama Barabarani mkoani humo Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Zauda Mohamed wakati akifungua mafunzo hayo amesema Jeshi hilo linatoa mafunzo hayo ili kuhakikisha usalama wa watalii ambao wataongezeka kwa wingi mkoani humo kuelekea msimu huo ambao unaanza hivi karibuni.

SSP amesema mafunzo hayo yatawaongezea weledi madereva hao katika utendaji wao wa kazi ambao utafanikisha watalii wote wanaofika mkoani humo kuwa salama wakiwa barabarani.

Sambamba na hilo pia amesema kupitia mafunzo hayo madereva hao wataelekezwa namna bora ya kuwasiliana na jeshi la Polisi ikiwa watapa changamoto za kiusalama pindi wanapokuwa barabarani na wageni ili jeshi hilo liweze kuzitatua kwa haraka.

Sambamba na hilo amewataka madereva hao kuhakikisha wanazingatia sheria za usalama barabarani ili watumiaji wa barabara hususani wageni wanaotoka sehemu moja kwenda nyingine kuwa salama.

Mkuu wa Kituo cha Polisi Utalii na Diplomasia Mrakibu wa Polisi SP Waziri Tenga amebainisha kuwa mafunzo hayo yameandaliwa kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais za kuutangaza Utalii ili kuongeza ujuzi na weledi kwa madereva hao katika kuhakikisha wanakua salama pindi wanapokuwa nao barabarani.

Naye Daktari Yusuph Mhando ambaye ni Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia masuala ya Taalumu na Utafiti toka Chuo cha Ufundi Arusha amesema chuo hicho kipo tayari na kimejipanga katika kuhakikisha wanatoa mafunzo bora kwa madereva hao ili shughuli zao ziweze kufanyika kwa ufanisi zaidi.

Bwana Sirili Akko ambaye ni Katibu Mtendaji wa TATO amesema waliomba mafunzo hayo kufanyika ili kuwajengea uwezo madereva hao kabla ya kuanza kwa msimu wa utalii hivi karibuni ambapo wanatarajia kupokea idadi kubwa ya wageni.

Kwa upande wake Bwana Elias Laizer ambaye ni dereva na muongoza watalii amebainisha kuwa mafunzo hayo yatawaongezea ujuzi na weledi ambao utapelekea kufanya shughuli zao kwa ufanisi zaidi.



Share To:

Post A Comment: