Na; Mwandishi Wetu – Dodoma

SERIKALI imefanya uwekezaji mkubwa na maboresho katika sekta ya Afya yanayokwenda sambamba na uwepo wa rasilimali watu itakayotoa huduma zenye ubora ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.


Hayo yameelezwa leo Aprili 18, 2023 na Mratibu wa Mipango ya Rasilimaliwatu katika sekta ya Afya Bw. Issa Mmbaga kutoka Wizara ya afya wakati wa mawasilisho yaliyohusu upatikanaji wa rasilimali watu katika sekta ya Afya, kwenye kikao cha wataalam kilichofanyika Jijini Dodoma.


Bw. Mmbaga alisema kuwa, baadhi ya maboresho yaliyofanywa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita katika sekta hiyo ni pamoja na ujenzi wa hosptali mpya, ongezeko la vifaa tiba na kuboreshwa kwa miundombinu iliyopo katika eneo la huduma.


“Maboresho haya yamesababisha mahitaji ya ziada ya watumishi katika sekta hii hivyo serikali ina mikakati maalum ya kuhakikisha kunaupatikanaji wa kutosha wa wataalam ili kuwa na sekta ya afya yenye nguvu na uwezo wa kutoka huduma bora za afya”. Alisema Bw. Mmbaga.


Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia masuala ya Sera na Program Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Crispin Musiba, amesema kuwa, uzalishaji wa madaktari na wataalamu wengine katika sekta ya Afya umekuwa mkubwa zaidi kiasi kwamba, idadi kubwa ya wataalam hao wapo nje ya ajira.



“Kwa hivyo ili kupunguza muonekano wa wataalam hao kuwepo nje ya Ajira, tumeita kikao hiki ili kuweza kuwa accommodate wataalam hao katika kupata ajira, na kikao hiki kimetoka na maazimio nane (8) ambayo tumepeana muda wa mwezi mmoja ili yaweze kukamilishwa na kuwasilishwa katika ngazi za juu.” Alisisitiza


Naye Mkurugenzi wa Afya kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapalagwe alisema, ipo haja ya kuendelea kuwa na program za elimu kwa umma kwa lengo la kuongeza uelewa kwa jamii hususan katika masuala ya huduma za kiafya ikiwemo zile za kibingwa zinazotolewa pamoja na kuwa na mikakati madhubuti ya tafiti mbalimbali zitakazoweza kusaidia kujua rasilimali iliyopo katika masuala ya afya.



“Maendeleo yaliyopo katika sekta ya afya, hayatazaa matunda ikiwa hatutaendelea kutoa elimu kwa umma kwa upana wake na kuwa na mikakati ya makusudi inayolenga kuboresha kada hii,”alisema Dkt. Ntuli


Kikao Hicho kilihusisha wataalam kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais Utumishi, Wizara ya Fedha na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu.



Share To:

ELIZA DOM

Post A Comment: