Mwandishi wetu, Arusha

SHIRIKA la wanahabari la kusaidia jamii za Pembezoni (MAIPAC) limegawa vitabu vya maarifa ya asili katika utunzwaji wa mazingira, vyanzo vya maji na misitu kwa wakurugenzi wa mashitaka yasiyo ya kiserikali nchini.

Wakurugenzi wa mashirika hayo na ambao ni wanachama wa Mtandao wa watetezi wa haki za binaadamu (THRDC) walitembelea MAIPAC kujifunza utendaji wake.

Wakurugenzi na wawakilishi wa mashirika hayo, waliongozwa na mkuu wa dawati la wanachama la THRDC, Lisa Kagaruki.

Wawakilishi wa mashirika hayo, licha ya kutembelea MAIPAC pia waliweza kupatiwa vitabu vya maarifa ya asili katika utunzwaji wa mazingira, vyanzo vya maji na misitu ambavyo vimeandaliwa na MAIPAC kwa kushirikiana na CILAO kwa udhamini wa shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) kupitia program ya miradi midogo na Mfuko wa Mazingira duniani (GEF).

Vitabu hivyo ambavyo vilizinduliwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira na Muungano, Dk Selemani Jafo vimekuwa vikiombwa na wadau mbalimbali wa mazingira na tayari vimesambazwa katika maeneo kadhaa nchini ikiwepo mashuleni .

Vitabu hivyo ni sehemu ya mradi wa uhifadhi wa mazingira, vyanzo vya maji na misitu kwa maarifa ya asili ambao umetekelezwa katika wilaya za Monduli, Longido na Ngorongoro.

Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma akizungumza na ujumbe wa wakurugenzi na wawakilishi wa mashirika hayo, amesema MAIPAC ni taasisi ya wanahabari ambao wamekuwa wakiandika habari juu ya jamii za pembezoni.

Juma amesema wanahabari 86 hadi sasa ndiyo wanachama wa MAIPAC wapo mikoa ya Manyara, Mara, Dodoma, Dar es salaam, Pwani, Kilimanjaro, Singida, Mwanza, Shinyanga, Morogoro na wenyeji Arusha

Amesema pia kuna wanachama ambao si wanahabari lakini ni wadau wa masuala ya haki ardhi, mazingira na usaidizi wa jamii za pembezoni.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa vitabu vya maarifa ya asili, mratibu dawati la wanachama wa THRDC, Lisa Kagaruki alipongeza shirika la MAIPAC kwa kazi nzuri ambayo linafanya.

Lisa amesema MAIPAC ni shirika mwanachama wa muda mrefu wa THRDC na limekuwa likifanya vizuri katika utekelezaji wa miradi yake na kutumia vyombo vya habari.

"Tunawapongeza MAIPAC Kwa kazi nzuri ambayo mnafanya na sisi kama THRDC tutaendelea kuwapa ushirikiano Ili mfikie malengo yenu," amesema.

Amesema licha ya kutoa kitabu MAIPAC pia wamekuwa wakifanya kazi nzuri katika kufatilia haki ya Haki za binaadamu nchini hasa katika makundi ya jamii za pembezoni na katika vyombo vya habari.

"Tumekuwa tukishirikiana na MAIPAC pia katika masuala ya mapitio ya hali ya haki za binaadamu nchini (UPR) hasa katika makundi ya pembezoni na katika tasnia ya habari," amesema.

Mkurugenzi wa shirika la PWY la Mtwara Alfred Muttakakwa ameipongeza MAIPAC kwa kazi nzuri ikiwepo kuweza kuchapisha kitabu cha maarifa ya asili.

"Binafsi nimevutiwa na ofisi nzuri ya MAIPAC na jinsi ambavyo mnafanya kazi nzuri," amesema.

Mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Community Hands Foundation (CHF) ya jijini Dar es Salaam, Paul Makoe, amepongeza MAIPAC kwa kazi nzuri ambayo inafanywa.

Makoe amesema CHF na MAIPAC wanauhusiano mkubwa ikiwepo kushirikiana katika masuala kadhaa ya utendaji na kupata wahisani.

"Sisi tumekuwa na Mahusiano na MAIPAC tangu tumeanzishwa, tumeshirikiana vizuri katika utekelezwaje miradi ya shirika la CESO tutaendelea na ushirikiano wetu," amesema.



Share To:

Post A Comment: