Na; Elizabeth Paulo, Dodoma


Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais , Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan imeridhia kutoa kibali cha kuajiri watumishi 21,200 wa Kada za ualimu na Afya.



Hayo yameelezwa leo Aprili 12, 2023 jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Angellah Kairuki wakati akitoa taarifa kwa waandishi wa habari.



Amesema Idadi ya watumishi watakaoajiriwa katika Kada za Ualimu ni 13,130 ambao watafundisha katika shule za Msingi na Sekondari huku akitaja idadi ya watumishi watakoajiriwa katika kada za Afya kuwa 8,070 ambao watafanya kazi katika Hospitali za Halmashauri, Vituo vya Afya na Zahanati.


Waziri Kairuki amesema waombaji wa kada za ualimu wanapaswa kuwa ni wale wahitimu wa kianzia mwaka 2015 Hadi mwama 2022 huku upande wa kada za afya wakiwa ni wahitimu wasiozidi miaka 45.


Aidha Waziri Kairuki amesema waombaji wanatakiwa kuomba ajira kuanzia leo April 12, hadi 25,2023 saa 5:59 usiku.



”Waombaji wote wanatakiwa kuwa na sifa za jumla kama zifuatazo awe mtanzania,awe na ukomo wa umri miaka 45 Awe na vyeti kamili vya mafunzo ya fani aliyoisomea yaani Cheti Cha Kidato cha nne, taaluma,cheti Cha kidato Cha sita, Cheti cha Taaluma na usajili kamili (Full Registration) au leseni hai ya kufanya kazi ya taaluma husika, na kitambulisho Cha NIDA.”amesema Waziri Kairuki


Amesema muombaji asiwe mwajiriwa wa serikali au mwajiriwa wa Hospitali za mashirika ya dini ambao tayari mshahara wao unalipwa na Serikali kutokana na Serikali kuingia mkataba na Mashirika hayo hivyo kuchangia kwenye mishahara yao.


Katika hatua nyingine Waziri huyo amesema kwa wale waliotuma maombi yao awali kupitia mfumo wa maombi ya ajira waweze kuhuisha taarifa zao katika mfumo huo kwa kiunganishi cha ajira au kuomba upya Kulingana na sifa zao.


Waziri Kairuki ametoa angalizo kwa waombaji kuepuka utapeli utakaojitokeza wakati wa kuomba nafasi hizo. 


Amesema waombaji wote wawe tayari kufanya kazi katika halmashauri na vituo watakavyo pangiwa na wawe tayari kufanya kazi na mashirika au Taasisi zilizoingia ubia na Serikali na baada ya kupangiwa kituo cha kazi hakutakuwa na nafasi ya kubadilishiwa kituo cha kazi kwa muda wa Miaka mitano.


kwa upande wa waombaji wenye ulemavu Waziri Kairuki amesema kwa sifa zilizoainishwa katika tangazo hilo ni vyema wakatuma maombi kupitia mfumo na kwamba ni vyema maombi yao yaeleze aina ya ulemavu alionao na kuambatisha picha na uthibitisho wa Daktari kutoka katika hospitali za Serikali.


“Nitoe angalizo kwa watakaofanya udanganyifu hatua za kijinai na kisheria zitachukuliwa dhidi yao kwasababu tunaangalia vigezo vya ajira vya watu wenye ulemavu kwa mujibu wa Sheria na ipo namba iliyotengwa kwaajili yao katika ajira kwahiyo nafasi hizi zitaenda kwa hao waliolengwa kwa watu wenye ulemavu.”Amesema 


Nakuongeza“Atakayejitokeza na kujaribu kufaya udanganyifu wa aina yoyote kueleza kwamba yeye anaulemavu ajue tutaenda mbali sana.”


Share To:

ELIZA DOM

Post A Comment: