IMG-20230324-WA0177
Mratibu wa mafunzo na Afisa Udhibiti Ubora wa Mbolea wa TFRA, Allan Marik akifafanua jambo wakati wa mafunzo ya ukaguzi wa mbolea zinazopita bandarini na bandari kavu yaliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ((TARI- Mikocheni) Jijini Dar Es Salaam
IMG-20230324-WA0181
Afisa Udhibiti Ubora wa TFRA, John Sosthenes akitoa mada wakati wa mafunzo ya ukaguzi wa mbolea zinazopita bandarini na bandari kavu kwa watumishi wa Mamlaka .
IMG-20230324-WA0178
Watumishi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) kulia ni Afisa Utawala na Rasilimali Watu, Ruth Magesa (kulia) na kushoto ni Mtaalamu wa Maabara Yohana Masalapilu wakifuatilia mafunzo ya namna ukaguzi wa mbolea zinazopita Bandarini na nchi kavu unavyofanyika.
IMG-20230324-WA0176
Baadhi ya watumishi wa TFRA walioshiriki mafunzo ya ukaguzi wa mbolea bandarini na bandari kavu wakifurahia mada iliyokuwa ikiwasilishwa.
IMG-20230324-WA0180
Baadhi ya watumishi wa TFRA walioshiriki mafunzo ya ukaguzi wa mbolea bandarini na bandari kavu wakifurahia mada iliyokuwa ikiwasilishwa.
IMG-20230324-WA0179
Afisa Udhibiti Ubora Mwandamizi wa TFRA, Ester Kapakala, akifafanua jambo alipokuwa akiwasilisha mada ya mambo ya kuzingatia wakati wa uteketezaji wa mbolea zisizokidhi vigezo kwa watumishi walioshiriki mafunzo ya namna ukaguzi wa mbolea zinazopita bandarini na bandari kavu unavyofanyika.
 

Mamlaka ya Udibiti wa mbolea Tanzania, (TFRA) kupitia Idara ya Huduma za Udhibiti imeratibu na kutoa mafunzo kuhusu ukaguzi wa mbolea bandarini na bandari kavu ili kuwajengea uwezo watumishi wake juu ya namna ukaguzi wa mbolea unavyofanyika.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo yaliyofanyika kwa siku 2 katika ukumbi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI- Mikocheni) Jijini Dar Es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Idara hiyo, Scholar Mbalila alisema mafunzo hayo yanalenga kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa watumishi wa Mamlaka ili wajue hatua na miongozo mbalimbali inayosimamia Mamlaka katika masuala yote ya ukaguzi wa mbolea..

Mafunzo hayo yamefanyika kwa nadharia kwa siku mbili, tarehe 22 na 23 Machi, 2023 na tarehe 24 yatafanyika kwa vitendo ambapo watumishi watatembelea Bandari ya Dar Es Salaam na kutembelea maeneo inakofanyika shughuli ya upakiaji wa mbolea katika mifuko Jijini humo.

Mada zilizowasilishwa katika mafunzo hayo ni pamoja na maandalizi ya kwenda kufanya ukaguzi bandarini ambapo watumishi walipitishwa kwenye mambo ya msingi yanayopaswa kuzingatiwa wanapojiandaa kwenda kufanya ukaguzi pindi meli inapotia nanga baharini. 

Aidha, Wasilisho kutoka Mtaalamu wa masuala ya sheria, Bw. Godfrey Munisi aliwasilisha mada juu ya sheria ya mbolea na kuchambua vifungu mbalimbali vinavyotumika katika tasnia ya mbolea ikiwa ni pamoja na kifungu kilichoanzisha Mamlaka.

Munisi alieleza kuwa, mbolea zote zinazotumika nchini lazima ziwe zimekidhi viwango vya ubora na kutimiza matakwa yote ya kisheria kwa kupitia hatua za ukaguzi, usajili na baadaye kuidhinishwa baada ya Mamlaka kujiridhisha na kutokana vigezo hivyo.

Mada kuhusu uteketezaji salama wa mbolea haikuachwa mbali ambapo Mdhibiti Ubora Mwandamizi, Bi. Ester Kapakala alieleza kuwa, ipo miongozo inayobainisha hatua za uteketezaji wa mbolea zisizokidhi viwango vya matumizi nchini. 

Bi. Ester alifafanua kuwa, kuwepo kwa mbolea isiyotumika katika Mkoa au Wilaya pia ni ukiukwaji wa sheria na kueleza kuwa uteketezaji wake utafanyika kwa kuiondoa mbolea hiyo na kupeleka katika maeneo wanayotumia mbolea husika.

"Jambo kuu la kuzingatia katika mada ya uteketezaji kuwa, uteketezaji si kutupa tu bali unahusisha kuondoa mbolea isiyotumika kutoka eneo moja na kupeleka eneo ambako itafaa kwa matumizi", Ester alisisitiza.

Akitoa shukrani ya mafunzo hayo yanayoendelea, Afisa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Ruth Magessa amesema, mpango wa kutoa mafunzo hayo ni mzuri sana na kushauri uwe endelevu kutokana na kuwaweka watumishi katika ukurasa mmoja wa kiutendaji.

"Mafunzo haya yanatufungua macho watumishi tusiohusika moja kwa moja kwenye shughuli za ukaguzi wa mbolea hivyo tunakuwa msaada hata kwa wananchi katika kuelimisha jamii zinazotuzunguka pindi tunapoulizwa maswali kuhusu masuala mbalimbali ya ukaguzi", Ruth alisisitiza.

Kwa upande wake, Afisa Udhibiti Ubora wa Mbolea, Bw. John Sosthenes aliwapitisha watumishi kutambua hatua za kuchukua wakati wa kufanya ukaguzi bandarini na bandari kavu.

Aidha, aliainisha vitu vinavyopaswa kukaguliwa kwenye eneo la ukaguzi pamoja na namna ya kuchukua sampuli mbalimbali za mbolea kwa ajili ya kwenda kuzipima.
Share To:

Post A Comment: