Matukio mbalimbali katika picha baada ya washiriki wa Kongamano la Kimataifa la Gesi 2023 kutembelea Kampuni ya Oryx Gas iliyoko Kigamboni jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuona shughuli zinazofanywa na kampuni hiyo katika kuendeleza sekta ya gesi . 

********** 

Na Mwandishi Wetu 

WASHIRIKI kongamano la kimataifa la wadau wa gesi Afrika Mashariki ambalo pia limehusisha mataifa mengine wamefanya ziara ya kutembelea Kampuni ya Oryx Gas huku wakieleza kuvutiwa na uwekezaji uliofanywa na kampuni hiyo. 

Wakizungumza baada ya ziara hiyo iliyofanyika katika kiwanda cha kampuni hiyo siku mbili baada ya kumalizika kwa kongamano hilo, baadhi ya washiriki hao wamesema wamevutiwa na teknolojia ya kisasa inayotumika katika ujazaji wa gesi, matengenezo ya mitungi na usafirishaji. 

Akizungumzia ziara ya washiriki hao, Meneja Operesheni wa Oryx Gas Lukas Banzi, amesema wadau hao wamefika kiwandani hapo na kuona shughuli mbalimbali zinazofanyika. 

“Wameona mitambo yetu ya kisasa kabisa, jinsi tunavyojaza gesi kwa kuzingatia ubora, tunajaza gesi kwa mitambo iliyothibitishwa kwa ubora na tunawahakikishia wateja bidhaa ambazo wanazipata kutoka kwetu zinakwenda sambamba na thamani ya fedha wanayotoa. 

“Kwa hiyo wageni wetu wameona na kufurahia jinsi tunavyofanya kazi, wameona jinsi tunavyohifadhi gesi, tunavyofanyia matengenezo mitungi yetu na usalama uliopo eneo la kiwanda. Tunajivunia kwani mbali ya kusambaza gesi, pia tumetoa ajira kwenye maeneo mbalimbali,” amesema. 

Ameongeza kuwa, wanajivunia kusambaza gesi ya matumizi ya nyumbani, hivyo kuwa sehemu ya kuunga mkono juhudi za serikali katika kuepusha wananchi kuendelea kutumia nishati chafu ya kupikia hususani kuni, mkaa na badala yake wanatumia gesi kuhifadhi mazingira. 

Kwa upande wake Mratibu wa ziara hiyo ambaye pia ni mratibu wa kongamano hilo la gesi kimataifa 2023, Catherine Ho, amesema washiriki wa mkutano huo wamepata nafasi ya kuona jinsi Tanzania inavyoendelea kujiimarisha katika uwekezaji wa gesi na kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza katika sekta hiyo. 

“Umefika wakati kwa wadau wa sekta ya gesi Afrika Mashariki, Afrika na dunia kwa ujuma kuunganisha nguvu kwa pamoja kuhakikisha matumizi ya gesi yanapewa nafasi kubwa, yanatumiwa na kila mmoja wetu na kwa usalama,” amesema Ho. 

Wakati huo huo Mkurugenzi wa Kampuni ya Top Masai inayojuhusisha na usambazaji wa gesi, Winner Lukumay, ambaye ni miongoni mwa washiriki waliotembelea Oryx Gas amesema amevutiwa na uwekezaji unaondelea katika sekta hiyo. 

“Uwepo wa nishati ya gesi unaongeza fursa za kibiashara kwa Mtanzania yeyote na kiwango chochote, usambazaji hauishii tu kwa msambazaji mkubwa bali unakwenda hadi kwa msambazaji mdogo, kwa hiyo sekta ya gesi inafungua nchi kiuchumi, imefungua mipaka ya nchi yetu,” amesema. 

Mdau wa sekta ya gesi Mhandisi Isaac Maguhwa ameipongeza Oryx Gas kwa uwekezaji mkubwa ambao umefanyika kwenye kampuni hiyo kwani wameshuhudia mitambo ya kisasa inayotumika kutkeleza shughuli mbalimbali zinazohusiana na gesi. “Tumekuja kwenye ziara hii kuona Oryx Gas nini wanafanya , wamefanya uwekezaji mkubwa lakini mwito wetu Tanzania tumebahatika kuwa na gesi nyingi , hivyo kama nchi tuendelee kuitangaza na kuhamasisha matumizi ya gesi majumbani kufika kwa watu wengi.”
Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: