Na; Elizabeth Paulo, Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa George Simbachawene Amezindua Mpangowa kuzuia na kukabiliana na Kipindupindu.

Katika kipindi cha Februari 19 Hadi machi 15, 2023 Serikali imepokea taarifa ya wagonjwa 60 wa mlipuko wa Kipindupindu katika mikoa minne ya Tanzania Bara.


Waziri Simbachawene ameeleza hayo leo Machi 22,2023 Jijini Dodoma Waziri wakati wa uzinduzi wa mpango shirikishi wa Taifa wa Kuzuia na Kukabiliana na Kipindupindu wa mwaka 2023-2027 uliobebwa na kauli mbiu isemayo "Ushirikiano wa Kisekta ni mkakati sahihi wa kuzuia ,kukabiliana na kutokomeza kipindupindu nchini Ifikapo mwaka 2030,".


“Hivi karibuni baadhi ya mikoa yenye wagonjwa ya kipindupindu ni Ruvuma 1, Kigoma 7, Katavi 34 na Rukwa18 na Manyara imekuwa ikipata milipuko ya Kipindupindu katika baadhi ya Halmashauri zake na kama mnavyojua ugonjwa wa kipindupindu kama yalivyo magonjwa mengine ya mlipuko, unasambaa kwa kasi na wakati mwingine kuvuka hata mipaka ya nchi hivyo lazima kuchukua tahadhari mapema,”amesema Simbachawene 


Pia ameitaka Wizara ya Afya kuongeza ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko ikiwemo Kipindupindu ili kuhakikisha unadhibitiwa usisambae nchini hususani katika maeneo ambayo yanapata milipuko ya mara kwa mara.


"Sisi wote ni muhimu katika kukabiliana na magonjwa ya milipuko ikiwemo ugonjwa huu wa kipindupindu ambapo chanzo chake kikubwa imeonekana kuwa ni matumizi ya maji yasiyo salama hivyo niwaombe wizara ya afya kuhakikisha wanapeleka nguvu katika maeneo yaliyoathirika sana na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu,"amesema Mhe.Simbachawene

 Simbachawene ameitaka Ofisi za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI),Halmashauri zote kushirikiana na Mamlaka za Maji Mijini na Vijijini (RUWASA) kuhakikisha hali ya uaptikanaji wa maji katika maeneo yao inaimarika pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuepuka uchafuzi wa vyanzo vya maji na kula vyakula vilivyopoa au visivyoandaliwa katika hali ya usafi pia Maji taka yasitiririke katika mazingira na makazi ya watu ili kuepukana na milipuko ya magonjwa ikiwemo ugonjwa wa kipindupindu.



Hata hivyo ,ameitaka ofisi hiyo kuongeza kasi katika kutoa elimu kwa wananchi juu ya matumizi ya vyoo bora,matumizi ya maji safi na salama ,kutotiririsha maji taka hovyo,kunawa mikono baada ya kutoka chooni na kabla na baada ya kula ili kupunguza milipuko ya magonjwa ikiwemo kipindupindu.


"kipindupindu ni ugonjwa wa aibu ambao haupaswi kutajwa katika nchi yetu ambayo imepiga hatua kubwa katika sekta mbalimbali ikiwemo Afya,Miundombinu na sekta zingine hivyo ni aibu sana kuendelea kuwa na tishio la ugonjwa huu wa aibu,"amesema Mhe.Simbachawene


Ameeleza kuwa kuna Taarifa kutoka shirika la Afya Dunia inaeleza kuwa na mlipuko mkubwa wa Kipindupindu nchini Malawi ambapo hadi kufikia tarehe 15 Machi 2023 kulikuwa na jumla ya wagonjwa 53,925 na vifo 1,658 vilivyotolewa taarifa.


“Taarifa hii inatupa tahadhari ya mlipuko huo pia kuvuka mipaka na kuingia nchini kwetu hususani pale tusipo imarisha afua mbalimbali za kujikinga na kipindupindu kwa jamii zetu hususani kwa Mikoa inayopakana na nchi hiyo,”amesema.


Pamoja na hayo ameeleza kuwa suala la Kuzuia na kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu ni mtambuka hivyo Wizara za Serikali, Taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi, Mashirika yasiyo ya Kiserikali na yale ya Umoja wa Mataifa yanapaswa kishirikiana Kwa ukaribu.


Naye Naibu Waziri wa Afya Dkt.Godwin Mollel amesema kuwa kwa mwaka 2015 Tanzania ilikuwa na visa vilivyoripotiwa vya ugonjwa wa kipindupindu 12,985 wakati kwa mwaka wa 2022 visa vilivyoripotiwa ni 537 na upungufu huo ni kutokana na uwekezaji uliofanywa na Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Mh Dkt Samia Suluhu Hassan.



"Tunawahakikishia wadau wetu kuwa wizara ya afya na Serikali kwa ujumla inatambua mchango wenu mkubwa mnaoutoa kuwasaidia watanzania katika kukabiliana na magonjwa mbalimbali ikiwemo kipindupindu na tunaahidi kuwa kama kuna changamoto yeyote tutakwenda kuifanyia kazi ili nanyi muweze kutekeleza majukumu yenu vyema,"amesema Dkt Mollel


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Ukimwi Mhe.Elibariki Kingu amesema kuwa uzinduzi wa mpango huo serikali inalenga kuhakikisha inaondoa kabisa ugonjwa wa kipindupindu na ibaki kuwa historia.

"Sisi ambao tunapata huduma zote zpmuhimu tunaweza kujikuta tunawasahau watu wa chini ila kwa mpango huu mnafanya kazi ya Mungu hivyo kamati inaahidi kushirikiana na nyinyi katika hili kuhakikisha ugonywa huu unatokomezwa na inabaki kuwa historia katika nchi yetu,"amesema Mhe.Kingu


Kwa Upande Mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri akitoa salamu za mkoa wa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Rosemary Senyamule amesema wanamshukuru na kumpongeza Rais Dkt.Samia Suluh Hassan kwa kuboresha miundombinu kwenye sekta ya afya ikiwemo vifaa tiba na kuboresha afya ya watu wake lakini hayo yote hayawezi kutimia kama hakuna mpango wa kuthibiti ugonjwa wa kipindupindu.


“Kama mkoa tutafuata taratibu zote mtakazotuambia ili kuhakikisha tunadhibiti magonjwa ya mlipuko hadi 2030 na kutokomeza kabisa ugonjwa wa kipindupindu na kuwa mfano kama makao makuu ya nchi”Amesema Shekimweri


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Save the Children Tanzania Angela Kauleni ,amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Januari mpaka machi mwaka 2023 shirika hilo kwa kushirikiana na waganga wakuu wa mikoa na wilaya wamefanikiwa kutoa mafunzo kwenye jamii ambapo watu 5000 wamepatiwa elimu ya kujikinga na ugonjwa wa kipindupindu.


Pia amesema changamoto walizokutana nazo ni pamoja na jamii ya wafugaji kutokukubaliana na elimu na kuendana na mabadiliko yaliyopo kwa sasa na baadhi ya jamii kuwa na mila potofu kuhusu mlipuko wa ugonjwa huo wakiamini kuwa ni ushirikina.


"Jamii nyingi za wafugaji zimekataa kabisa kukubaliana na elimu pamoja na mabadiliko yaliyopo kwa sasa na wengine wamekuwa na imani potofu kuwa mlipuko wa ugonjwa huo ni ushirikina jambo ambalo sio kweli na hapa serikali inatakiwa iongeze kasi katika kuelimisha jamii kuhusu magonjwa haya ya mlipuko,"amesema Kauleni


Amesema wanaishukuru serikali kwa kutoa ushirikiano katika mikoa ya katavi na manyara na wameweza kushirikiana vizuri na serikali za mikoa na wanashukuru hakuna magonjwa mapya.



” Tunafanya miradi ya maendeleo pamoja na miradi ya kujenga taifa kusaidia watoto kufikia malengo yao kuhakikisha kwamba watoto wanaishi na wanasaidiwa kujifunza kulindwa na kuhakikisha mtoto hafanyiwi ukatili wa aina yeyote”Amesema Angela


Naye mwakilishi kutoka UNICEF Tanzania Bi.Maniza Zaman ameipongeza serikali kwa kuweza kushiriki vizuri kuhakikisha inapambana na ugonjwa wa kipindupindu, elimu itaokoa maisha kwani kila mtu ataelewa ni namna gani atajikinga dhidi ya kipindupindu na wala sio kutumia pesa kwani pesa si chochote muhimu ni usafi.



“Kuzindua mpango ni rahisi lakini utekelezaji wa mpango ndio muhimu zaidi lazima kuhakikisha tunatekeleza na kutoa elimu kwa wananchi kwa kushirikiana na waganga wa eneo husika”Amesema Bi Maniza



Mwakilishi kutoka World health organization(WHO) Tanzania amesema tumezindua kitu muhimu kwenye maisha,kuokoa maisha ya watu,hatutaki na tunataka kuhakikisha tunatokomeza kabisa kipindupindu Tanzania 2030.


"Kukusanya sekta zote kwa pamoja itafanya sekta ya afya kufanya kazi kwa urahisi ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu".






Share To:

ELIZA DOM

Post A Comment: