Muonekano wa Barabara ya lami ya Mjimwema-Daniel yenye urefu wa km 2.2 katika  Halmashauri ya Mji Mbinga iliyojengwa na wakala wa Barabara  mjini na vijijini Tarura wilaya ya Mbinga  chini ya Mkandarasi Kampuni ya Ovans  Construction Ltd  kwa gharama ya Sh.bilioni 1.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Ovans Construction Ltd Valence Urio kulia na meneja wa Tarura wilaya ya Mbinga Mhandisi Oscar Mussa wakikagua sehemu ya Barabara ya lami ya Mjimwema-Daniel yenye urefu wa km 2.2 iliyojengwa na Kampuni  ya Ovans Construction Ltd ambayo imekamilika kwa asilimia 100.

 SERIKALI imetoa kiasi cha Sh,bilioni Moja zilizowezesha kujenga km 2.2 za barabara ya lami na hivyo kumaliza changamoto ya muda mrefu ya mawasiliano kwa wananchi wa kata ya Mjimwema Halmashauri ya mji Mbinga mkoani Ruvuma.

Pia, fedha hizo zimetumika kufunga taa 20 za barabarani zinazotumia umeme wa jua na kujenga mitaro ya kupitisha maji ya mvua kwenda maeneo husika ambayo awali yalilazimika kwenda hadi kwenye makazi ya watu kutokana na kukosekana kwa mitaro ya uhakika.

Hayo yamesemwa na meneja wa Tarura wilayani Mbinga Oscar Mussa, wakati akizungumza na waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji wa miradi  ya barabara katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Mbinga.

Amesema kati ya fedha hizo,milioni 500 za maendeleo ya mfuko wa jimbo na  Sh.milioni za maogesho zilizotolewa na serikali kuu na barabara hiyo inajengwa na kampuni ya Ovans Contrution Ltd ya Mbinga.

Amesema, lengo kuu la barabara hiyo ni kuwawezesha wananchi wa kata ya Mjimwema kuwa na mawasiliano ya uhakika kwenda katika maeneo ya uzalishaji na kuiwezesha serikali kutoa huduma bora kwa wananchi na kuibua fursa za uwekezaji katika kata hiyo ili kukuza uchumi mtu mmoja mmoja,wilaya  na Taifa.

Amesema,mpango uliopo katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha 2023/2024 ni kuendelea kujenga kipande kilichobaki chenye urefu wa mita 800 na kuunganisha na barabara nyingine ya Mbinga Lipalamba pamoja na kufunga taa ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Amesema,kwa mwaka  wa fedha 2022/2023 Tarura wilaya ya Mbinga imejenga jumla ya km 3.5 kwa kiwango cha lami,kufunga taa za barabarani 30 na katika bajeti ijayo wanatarajia kujenga barabara mpya urefu wa km 4 kwa kiwango cha lami.

Mussa ameishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan,kuendelea kuipatia Tarura fedha kwa ajili ya kujenga barabara za lami ambazo zitakwenda kuchochea kukua kwa uchumi na maisha ya wananchi wa Mbinga

Amewatoa rai kwa wananchi kutunza barabara hiyo na zinazojengwa katika maeneo mbalimbali kwa kutozidisha uzito,kutomwaga mafuta,kufanya shughuli za kilimo kando kando ya barabara ili ziweze kudumu kwa muda mrefu.

Mkurugenzi wa kampuni ya Ovans Construction Ltd inayojenga barabara hiyo Valence Urio,ameishukuru serikali kwa kuwaamini wakandarasi wa ndani na kutoa fedha nyingi za ujenzi wa miradi ya barabara hapa nchini.

Urio,amewaasa wakandarasi  wenzake juu ya suala la uaminifu,kuzingatia muda wa mikataba na kufanya kazi kwa  viwango ili serikali iendelee kuwaamini na kuwapa kazi za miradi ya ujenzi wa barabara  badala ya kulipua.

Naye msimamizi wa mradi huo kutoka kampuni ya Ovans Construction Mhandisi Vilgilia Ndunguru amesema,barabara hiyo imejengwa kwa ubora wa hali ya juu na kuiomba serikali kuiamini kampuni hiyo kwenye ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Makazi wa kata ya Mjimwema Stephen Komba amesema,hapo awali hali ilikuwa mbaya sana kutokana na utelezi na maji kusambaa kwenye makazi yao hasa nyakati za masika pamoja na mashimo na hivyo  kutopitika kwa urahisi.

Daniel Kumburu,ameishukuru serikali kwa kuona umuhimu wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami na kurekebisha baadhi ya maeneo korofi ambayo yalichangia shughuli za kiuchumi katika kata hiyo kusua sua.
Share To:

Post A Comment: