MKUU wa Mkoa wa Tanga, Omari Mgumba, amewataka viongozi na wadau wa elimu kuweka mikakati ya kuongeza ufaulu kwa kupambana na viashiria vinavyosababisha kutofanya vizuri kwenye mitihani ya kitaifa.

Baadhi ya viashiria hivyo ni ukatili, mimba za utotoni, ajira kwa watoto na kuimarisha upatikanaji wa chakula shuleni.

Ametoa maelekezo hayo wakati akizungumza na wadau wa elimu Mkoa wa Tanga katika kilele cha siku ya wadau wa Elimu ngazi ya mkoa na kufanya tathmini na mikakati ya kuongeza ufaulu

amewataka maofisa elimu na wakuu wa shule kuzibaini changamoto hizo na kuja na mbinu ya kukabiliana na tatizo la ufaulu mdogo katika madarasa ya mitihani.

“Miongoni mwa changamoto tulizonazo ni mdondoko wa  wanafunzi, wanaanza wengi la kwanza lakini wakifika darasa la pili wanakuwa wachache na hadi wakifika darasa la saba wanakuwa wachache zaidi.

“Hivyo naelekeza kwa wakurugenzi wote kufuatilia na kutoa taarifa kila mwezi ya mahudhurio ya wanafunzi, ili kufahamu changamoto inayoendelea na kutafutia ufumbuzi,” alisema RC Mgumba.

Ofisa Elimu Mkoa wa Tanga,  Newaho Mkisi amesema kuwa kuna changamoto nyingi zinazosababisha ufaulu kuwa wa chini  na kubwa ni wazazi kushindwa kufuatilia maendeleo ya watoto wao, hali inayosababisha kuwepo utoro uliokithiri.

Share To:

Post A Comment: