Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji imeridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa mradi wa Maji Butimba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 69 wa Jijini Mwanza. 

Hayo yamedhihirishwa na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Almasi Maige (Mb) wakati wa ziara yao kutembelea mradi huo iliyofanyika leo Januari 13, 2023.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhishwa na hali tuliyoishuhudia, tumeona kazi inafanyika, mradi unakwenda vizuri. Ni matumaini yetu kero ya maji kwa wakazi wa Mwanza inakwenda kutatuliwa." Amesema Mhe. Maige.

Aidha, Kamati hiyo imeielekeza Wizara kuongeza usimamizi ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) amepokea maelekezo ya Kamati na ameihakikishia kuwa Wizara itaongeza usimamizi ili mradi ukamilike inavyopasa.

"Sisi kama Wizara tumepokea maelekezo ya Kamati na tunaahidi kutekeleza yote yaliyoagizwa ili lengo la Rais wetu mpendwa Mhe. Dokta Samia Suluhu Hassan ya kumtua Mama wa Mwanza ndoo kichwani inatimia." Amesema Mhandisi Mahundi.

Amesema nia ya Serikali ni kuhakikisha kila mwananchi anafikiwa na huduma ya majisafi, salama na yenye kutosheleza na kwamba Wizara itahakikisha nia hiyo inafikiwa bila kuwepo kwa vikwazo.


Share To:

Post A Comment: