Na. Asila Twaha, Tanga


Serikali inaendelea  kuboresha miundombinu ya kutolea huduma za afya, kutoa elimu kwa jamii na kuweka mikakati  thabiti ili kudhibiti  magonjwa ya  mlipuko katika jamii.


Hayo yamesemwa  leo Disemba 14, 2022 na Dkt. James Kengia alipozungumza kwa niaba ya  Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe Ofisi ya Rais -TAMISEMI  katika kikao kazi cha Tathmini ya Programu  ya utoaji wa Elimu  ya Afya na Ushirikishwaji wa Jamii katika Majanga mbalimbali ya magonjwa ya mlipuko kinachofanyika mkoani Tanga.



Dkt. Kengia amesema lengo la kikao hicho kinachofanyika chini ya Ofisi ya Rais TAMISEMI ni kuwajengea uwezo washiriki,  kufanya tathmini, kubaini changamoto pamoja na  kuweka mikakati  ya namna bora  ya kudhibiti majanga yanayosababishwa na magonjwa ya mlipuko.  


"Nitoe rai kwa wataalam wa afya  kwa ngazi ya jamii, kuendelea kutoa elimu ya magonjwa ya mlipuko kwa wananchi ili mwananchi aweze kujikinga na magonjwa hayo, katika Ugonjwa wa UVIKO-19  tulishirikiana sana na viongozi wa dini katika kutoa  elimu ya tahadhari, tuendelee kushirikiana  nao ili tuwe na uwelewa wa pamoja" amesema Dkt. Kengia


Aidha, amesema  Serikali inaendelea kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa  kuimarisha  miundombinu  ya kutoa huduma za afya, kununua  vifaa tiba pamoja na  kuendelea kuajiri wataalam  wa afya ili kutoa huduma bora kwa wananchi.


Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Idara ya Afya kutoka Idara ya Kinga Kitengo cha Elimu ya Afya kwa Umma Wizara ya Afya  Bw. John Yuda amesema, Serikali inao wataalamu ambao wanafanya utafiti katika kutafuta  kinga na tiba sahihi ya magonjwa ya mlipuko ili kudhibiti maambukizi katika jamii hivyo amewataka wananchi kuendelea kuwasikiliza wataalamu wa afya  kwa kuchukua tahadhari  na kujikinga na magonjwa ya mlipuko ukiwemo  ugonjwa tishio wa Ebola ambao upo katika nchi jirani.


Naye Mwakilishi kutoka Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe Ofisi ya Rais – TAMISEMI Bi. Chipole Mpelembe amesema mafunzo hayo  ya siku tatu yatasaidia  kuongeza weledi na mbinu bora za kuongeza uwajibikaji katika kudhibiti  magonjwa ya mlipuko.


Kikao kazi hicho kimewashirikisha, Wizara ya Afya kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, Waratibu Afya Jamii kutoka mikoa 13 ya Tanzania Bara iliyopo katika hatari ya kupata ugonjwa wa Ebola, Wadau wa Maendeleo na Watafiti.

Share To:

Post A Comment: