MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi Taifa Fadhil Maganya, mesema wataendelea kuenzi,kuthamini na kusikiliza nasaha za Wazee wa Chama hicho.

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza na Baraza la Wazee wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar katika ziara yake ya mara ya kwanza kufika Afisi Kuu ya CCM Zanzibar Kisiwandui toka achaguliwe nafasi hiyo.

Alisema Wazee wana mchango mkubwa wa maendeleo ndani ya Chama na Jumuiya zake hivyo wanatakiwa kuthaminiwa na kupewa kipaumbele cha pekee.

Maganya, alieleza kwamba mafanikio makubwa ya kisiasa,kiungozi,kiitikadi,kiuchumi na kimaendeleo yaliyofikiwa ndani ya CCM yametokana na nasaha,ushauri na miongozo ya Wazee hao.

Katika maelezo yake Mwenyekiti huyo Mganya, aliwashauri wazee hao waendelee kushauri na kutoa miongozi itakayochochea sera za kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wote.

“ Wazee wetu endeleeni kutukosoa,kutushauri na kutuongoza katika misingi mizuri ya kutujenga kwani nyinyi, mmepitia mengi na mnakijua Chama,Serikali na Taasisi zote kuliko kundi lolote ndani ya Chama Cha Mapinduzi.

Dua na ushauri wenu ndio zilizosaidia uwepo wa amani na utulivu wa Zanzibar, hivyo mnayo nafasi kubwa ya kutuonyesha njia sahihi za kupita kuelekea katika kilele cha mafanikio ya Chama na Jumuiya yetu ya Wazazi.” Alieleza Mwenyekiti huyo.

Mwenyekiti huyo alilisihi Baraza hilo, kuendelea kuwaombea dua Marais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassa ili Mwenyezi Mungu aendelee kuwajaalia wepesi wa kuongoza nchi kwa haki,maarifa,upendo uliotukuka.

Maganya,akizungumzia kipaumbele chake katika uongozi wake, alisema ana dhamira ya kuleta maendeleo endelevu kwa kuendeleza miradi iliyopo na kubuni miradi mipya itakayoleta tija kwa wanachama wote ndani ya jumuiya hiyo.

Naye Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Mwalimu Kombo Hassan Juma, alisema Afisi Kuu ya CCM Zanzibar ina historia kubwa ya mageuzi na maendeleo ya kisiasa nchini toka enzi za ASP mpaka sasa wakati wa CCM.

Alisema eneo hilo ndio aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar Marehemu Sheikh Abeid Aman Karume, aliuawa na wapinga maendeleo na kuzikwa kwa heshima katika eneo hilo ili kulinda historia ya Zanzibar kwa maslahi ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Mwalimu Kombo, alieleza kuwa CCM kwa upande wa Zanzibar pamoja na Serikali yake ya Mapinduzi  zimeendelea kuimarika kisiasa,kiuchumi,kimaendeleo na kidiplomasia kutokana na uimara,uhodari,uchapakazi wa viongozi wake.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Zanzibar  Waziri Mbwana, alieleza kuwa Wazee ndio walioasisi Afro- Shiraz Party (ASP) ambayo sasa ni CCM na kushiriki katika harakati za ukombozi wa Nchi kupitia Mapinduzi ya Mwaka 1964.

Alieleza kuwa Wazee hao pamoja na majukumu ya msingi waliyokuwa nayo ya kutoa miongozo na ushauri kwa Chama na Serikali kusimamia vyema Ilani ya CCM ya mwaka 2020/2025 pia wamekuwa wakishiriki katika harakati za maandalizi ya ushindi wa CCM katika uchaguzi Mkuu wa Dola mwaka 2025.

Katika ziara hiyo Mwenyekiti huyo ameongozana na Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Doto Iddi Mabrouk, Wajumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya pamoja na Watendaji wa ngazi mbalimbali za Jumuiya hiyo kwa upande wa Zanzibar.

 

Share To:

Post A Comment: