WANAKIJIJI wa Lemoti Wilaya ya Monduli wameanza kunufaika na huduma za afya baada ya kuzinduliwa kwa Zahanati yao iliyo umbali wa zaidi ya Km 70 kutoka Hospitali ya Wilaya waliokuwa wakiitumia kupata huduma. 

Uzinduzi huo umefanywa na Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel baada ya kupokea maelekezo kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa CCM bara Ndg. Abdulrahman Kinana kwa niaba ya Chama hicho.

Amesema, historia imeandikwa baada ya uzinduzi wa Zahanati hiyo ambayo tayari imeanza kutoa huduma, na kuwahakikishia wanakijiji hao uwepo wa dawa zakutosha, vitanda vya kujifungulia na wahudumu wa afya, huku akisisitiza Serikali itaendelea kuleta vifaa zaidi. 

Aidha, Dkt. Mollel ameweka wazi kuwa, kwa mwaka huu 2023 Wilaya ya Monduli imepata kiasi cha shilingi Bilioni 2.7 katika eneo la kuboresha Sekta ya Afya ikiwemo kuboresha miundombinu, dawa na upatikanaji wa vifaa tiba vitavyosaidia kuwahudumia wanakijiji wa Lemoti. 

Ameendelea kusema kuwa, Serikali tayari imepokea barua kutoka ofisi ya Mbunge wa Jimbo hilo, ikiomba kuendelea kupanua huduma katika Zahanati hiyo ili kuwapunguzia hadha wananchi ya kufuata huduma katika hospitali ya Rufaa ya Wilaya iliyo zaidi ya Km 70 kutoka kijiji hicho.

Kwa upande mwingine, Dkt. Mollel amewaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Wafawidhi wote kusimamia ubora wa huduma katika maeneo yao ya kutoa huduma, na kusisitiza kuwa Serikali itawapima utendaji wao kama wanafaa au hawafai kupitia ubora wa huduma katika maeneo yao ya usimamizi. 

Pia, amewaelekeza MDS kuhakikisha upatikanaji wa dawa wakati wote, huku akisisitiza Rais Samia ametoa zaidi ya Bilioni 200 iliyofanya upatikanaji wa dawa kuongezeka kutoka 32% mpaka 62%, huku akisisitiza mpango wa Serikali ni kuhakikisha upatikanaji wa dawa usipungue 98%.

Katika maeneo yetu ya kutoa huduma kuna mapato ya ndani yanapatikana, tunasisitiza mapato hayo yatumike kwenye kuboresha upatikanaji wa dawa, na kuwataka MSD kutoa mrejesho juu ya uwepo au kutokuwepo kwa dawa ndani ya siku moja ili kutoa fursa kwa kituo kununua dawa hizo katika maeneo mengine kabla ya kusababisha usumbufu kwa wananchi. 

Pia, ametoa wito kwa viongozi ngazi zote kushirikiana kwa karibu katika kusimamia dawa tangu zinapotoka msd mpaka zinapofika katika kituo, huku akiwataka kuunda kamati za jamii za afya kusimamia dawa zinapoletwa na kusimamia zinavyotumika na kutuma taarifa kwa hiyo kwa viongozi wa Wilaya, Jimbo na Halmashauri. 

Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutenga fedha kwaajili ya kuboresha na kusogeza huduma karibu na wananchi ili kuwaondolea usumbufu wa kwenda mbali kuzifuata huduma hizo.
Share To:

Post A Comment: