NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo ameiagiza Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu wizarani hapo kuhakikisha inaratibu kufanyika mara kwa mara mafunzo kwa watumishi wa Wizara ili kuwajengea  uelewa kuhusu Kanuni za Utumishi wa Umma waweze  kujua haki na wajibu wao .

Amesisitiza kuwa, mafunzo hayo yatawawezesha watumishi kupata maarifa mapya, ufahamu na kuongeza ufanisi katika utendaji wao wa kazi ikiwemo kuwawezesha wajumbe wa baraza hilo kufahamu wajibu wao katika baraza hilo.

Ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo kwa wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Madini ambayo yatakwenda sambamba na mkutano wa baraza hilo yanayofanyika mkoani Morogoro.

Ameongeza kuwa, ikiwa watumishi watashindwa kujua Kanuni za Utumishi wa Umma, wajibu na haki itapelekea kupunguza tija na ufanisi  mahali pa kazi.

‘’ Nawasihi tukitoka hapa tukawafamishe na wenzetu ambao hawakupata nafasi ya kushiriki katika mafunzo haya ili wapate uelewa,’’ amesema Mbibo.

Naibu Katibu Mkuu Mbibo amesema katika siku mbili za mafunzo, wajumbe watapitishwa kwenye mada mbalimbali ikiwemo inayohusu utunzaji na Matumizi Sahihi na Salama ya taarifa za Serikali na kuwataka wajumbe hao kufuatilia mada hiyo kikamilifu kutokana na umuhimu wake katika shughuli za serikali.

‘’ Utunzaji wa taarifa za Serikali ni utunzaji wa usalama wetu, wakati mwingine tunayachukulia masuala haya kwa uzito mdogo lakini yanaweza kutuangusha,’’ amesisitiza Mbibo.

Katika siku ya kwanza ya mafunzo hayo, wajumbe wameelimishwa kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu  marekebisho na Kanuni za Utumishi wa Umma za  mwaka 2022,  elimu kuhusu Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (PSSSF)  pamoja na chimbuko la Baraza na majukumu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi.

Wakitoa mada katika mafunzo hayo,  Wataalam kutoka Mfuko wa Jamii (PSSSF)  Julius Shayo na Emmanuel Meshack kwa nyakati tofauti wamesisitiza kuhusu umuhimu wa watumishi kupitia taarifa za michango yao zikiwemo taarifa za kibenki, usahihi wa majina ya  mwanachama na  kusisitiza umuhimu wa waajiri kuwasilisha kwa wakati michango ya wanachama .

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi  wa masuala ya Utumishi na RasilimaliWatu  Nsajigwa Kabigi amewaelimisha watumishi kuhusu marekebisho mbalimbali yaliyofanyika katika Kanuni mbalimbali za utumishi wa umma.

Naye,  Afisa Elimu Mwandamizi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Emmy Rweyendela, amewaelimisha wajumbe kuhusu chimbuko la baraza la wafanyakazi na majukumu yake.

Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Madini lilizinduliwa rasmi mwezi Machi, 2022 na kuazimia wajumbe wake kupatiwa mafunzo kuhusu wajibu na majukumu yao.

Share To:

Post A Comment: