Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura), Mhandisi Victor Seff amemuondoa kwenye majukumu yake aliyekuwa Meneja wa Tarura Wilaya ya Kilombero kwa kushindwa kusimamia miradi kikamilifu.

Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa boksi kalavati katika barabara ya Mawala-Mofu-Ikwambi yenye urefu wa kilometa 30 iliyopo Halmashauri ya Mlimba, Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.

Mhandisi huyo amefikia uamuzi huo leo Jumapili Oktoba 16, 2022 wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi wilayani Kilombero na kubaini mapungufu katika usimamizi wa miradi ikiwemo ujenzi wa boksi kalavati katika barabara ya Mawala-Mofu-Ikwambi ambalo limejengwa chini ya viwango vya mkataba.


“Nimekagua na kujiridhisha kwamba mradi huu umejengwa chini ya kiwango, kwakweli sijaridhishwa kabisa na usimamizi wa hapa, hivyo nimemuondoa kwenye nafasi yake kuanzia leo aliyekuwa Meneja wa Tarura Wilaya ya Kilombero na atapangiwa majukumu mengine”, amesema Mhandisi Seff.

Mtendaji Mkuu huyo amemtaka mkandarasi aliyejenga mradi huo chini ya viwango vya mkataba kubomoa kwa gharama zake na kukamilisha ujenzi wa boksi kalavati jipya ndani ya kipindi cha mwezi mmoja.

Pia, Mhandisi Seff amewataka mameneja wa Tarura nchi nzima kusimamia kikamilifu miradi kwenye maeneno yao na kwamba hatua kali zitachukuliwa kwa yeyote atayeshindwa kutimiza majukumu yake ili kuhakikisha fedha inayotolewa na Serikali inaendana na ubora wa miradi inayotekelezwa.



H.T Mwananchi

Share To:

Post A Comment: