BENKI ya Stanbic Tanzania imetilia mkazo dhamira yake ya kusaidia wajasiriamali wadogo na wa kati kwa kutoa huduma zinazokidhi mahitaji yao na kutatua changamoto zinazowakabili.

Ahadi hiyo imetolewa na Mkuu wa Atamizi wa Benki ya Stanbic, Kai Mollel wakati wa Kongamano la sita la mwaka la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi lenye kaulimbiu; “Uwezeshaji wa Watanzania katika Uwekezaji” lililofanyika juzi Dodoma huku benki hiyo ikiwa ndiyo mdhamini mkuu.

Jukwaa hilo la siku moja lilihudhuriwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye aliwapongeza wadhamini wakuu kwa kuisaidia NEEC kufanikisha jukwaa hilo, huku akitilia mkazo kuwa serikali inathamini mchango wao kwa kuzingatia serikali iko katika mpango wa kutengeneza mazingira mazuri ili Watanzania waweze kushiriki katika shughuli za uwekezaji.

“Tunapenda kuihakikishia serikali, wafanyabiashara na wadau wote wa maendeleo kwamba sisi kama benki tutaendelea kushirikiana nanyi katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu,” alisema na kuongeza:

“Benki yetu inaongoza kwa uwekezaji, mwaka huu tumetunukiwa tuzo ya Benki Bora ya Uwekezaji na EuroMoney Market Leaders kwa mwaka 2022 kutoka kwa jarida la EuroMoney. Hii ni kwa sababu tumeendelea kutoa huduma mbalimbali zinazowawezesha Watanzania kushiriki na kunufaika na uwekezaji nchini,” alisema.

Share To:

Post A Comment: