Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa) limetangaza ukomo wa utumishi wa maofisa wake wawili kwa sababu ambazo hazijawekwa bayana.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa umma, watumishi hao ni Kamishna Mwandamizi wa Uhifadhi, Pascal Shelutete na Ofisa Uhifadhi Mwandamizi, Justin Lema na kwamba utumishi wao umekoma kuanzia Septemba 15, 2022.

“Uongozi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania unaujulisha umma wa Watanzania na wadau wote wa uhifadhi na utalii kuwa waliokuwa watumishi waandamizi wa Tanapa, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Pascal Shelutete na Ofisa Uhifadhi Mwandamizi, Justin Lema, utumishi wao umekoma kuanzia Septemba 15, 2022.

“Shirika halitahusika na jambo lolote watakalojihusisha nalo kwa niaba ya shirika,” inaeleza taarifa hiyo ambayo hata hivyo haijabainisha sababu za kukoma kwa utumishi wao.

Mwananchi lilimtafuta Ofisa Uhifadhi Mwandamizi wa Tanapa anayeshughulika na Mawasiliano, Catherine Mbena kujua sababu za kukoma kwa utumishi wa maofisa hao, hata hivyo hakuwa tayari kuzungumzia sababu hizo akidai kwamba shirika halijataka kuweka bayana.

“Tukiwa tunataka kufanya hivyo (kueleza sababu) tutawaambia, lakini for now (kwa sasa) tuna hilo tangazo tu,” amesema Mbena 

Share To:

Post A Comment: