Na WyEST, MOROGORO


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Omari Kipanga (Mb) ameutaka uongozi wa chuo cha Ualimu wa Ufundi Stadi (VETA) Morogoro kuhakikisha ujenzi wa mabweni kwa ajili ya wanafunzi chuoni hapo unamalizika ifikapo tarehe 1 Septemba mwaka huu.


Mhe. Kipanga ameyasema hayo alipotembelea chuoni hapo kukagua maendeleo ya ujenzi huo ulioanza mapema mwezi Februari.


Ujenzi wa mabweni hayo ya kisasa umegharimu kiasi cha Shilingi milioni 400 na ulitarajiwa kukamilika Juni 3, hivyo Naibu Waziri amemtaka mkandarasi (Arusha Technical College) kumaliza ujenzi huo ndani ya siku 15.


“Mmefanya kazi nzuri lakini bado mpo taratibu ‘speed’ ni ndogo. Hatutaki kila tukija hapa tunaona bado mpo tu, tunataka ifikapo Septemba mosi mumkabidhi Mkuu wa Chuo funguo zake na tuanze maandalizi ya uzinduzi rasmi, ” amesema Kipanga.


Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Chuo hicho, Samweli Kaali amesema hadi sasa ujenzi wa mabweni hayo umefikia asilimia 95.








Share To:

Post A Comment: