Na Mwandishi wetu, Mirerani
WADAU wa madini ya Tanzanite Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamepatiwa elimu ya sensa ya watu na makazi inalotarajiwa kufanyika Agosti 23 mwaka huu.

Afisa madini mkazi (RMO) wa Mirerani, Fabian Mshai akizungumza kwenye mafunzo hayo amesema wameiunga mkono Serikali kwa kutoa elimu ya sensa na makazi kwa wadau wa madini ili waweze kushiriki vyema zoezi hilo.

Mshai amesema ni vyema wadau wa madini nao wakapata elimu ya sensa na kuuliza maswali ya kuwaongezea uelewa ili kujengewa uwezo zaidi wa kushiriki vyema zoezi hilo.

"Hawa wamiliki wa migodi, wachimbaji, wanunuzi wakubwa na wadogo, walioshiriki kupata elimu hii watakuwa mabalozi wazuri katika kufikisha elimu hii ya sensa," amesema Mshai.

Mmoja kati ya wamiliki wa mgodi Dk Cutis Msosa amesema kupitia mafunzo hayo wamebaini hatua zitakazochukuliwa kwa wale ambao watashiriki kuzuia kufanyika kwa sensa hiyo.

Dk Msosa amesema wachimbaji wamebaini kuwa shughuli ya sensa na makazi ipo kisheria hivyo wachimbaji watatoa ushirikiano wa kutosha kwa makarani watakaofika kuendesha zoezi hilo.

Mchimbaji mwingine Isack John amesema wachimbaji wamejifunza kuwa mtu atahesabiwa kwenye sensa hiyo mahali alipolala nakuamkia na siyo anapoishi.

"Tumebaini kuwa mkuu wa kaya ataelezea kwa karani wa sensa idadi ya watu waliolala kwa siku hiyo ya kuhesabiwa na siyo watu wanaoishi kwenye makazi husika," amesema.

Mmiliki mwingine Shaibu Mushi amesema kupitia elimu hiyo amefahamu kuwa wasafiri watahesabiwa mahali walipo pamoja na wageni waliolala kwenye nyumba za wageni.

"Kumbe utaratibu umewekwa vizuri na serikali hivyo sisi wachimbaji hatakama tutakuwa migodini tutahesabiwa hata tukiwa tumepumzika eneo lingine tutahesabiwa pia," amesema Mushi.
Share To:

Post A Comment: