Mkurugenzi Mtendaji wa Makumbusho ya Viumbe Arusha,  Dk. Christine Ngereza akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) katika maadhimisho ya Siku ya Makumbusho Kitaifa Duniani iliyoadhimishwa leo Mei 18, 2022. 


Na Dotto Mwaibale


KATIKA kuadhimisha Siku ya Makumbusho ya Kitaifa Duniani Makumbusho ya Taifa ya Viumbe iliyopo  Arusha  imetumia Siku hiyo kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kuwa na makumbusho.

Akizungumza leo Mei 18, 2022 na waandishi wa habari Mkurugenzi Mtendaji wa Makumbusho hayo Dk. Christina Ngereza alisema wametumia siku hii kutoa elimu kwa Umma kuhusu Makumbusho ni nini, Umuhimu wa Makumbusho katika maendelo ya nchi na haja ya kuwa na Makumbusho nyingi mbalimbali Tanzania. 

Aidha alisema kulikuwa na uhamasishaji  wananchi, Serikali jinsi ya utayarishaji wa makumbusho za aina mbalimbali hapa nchini hasa katika maeneo ya pembezoni kwa lengo la kuwa na vivutio vya utalii.

Alisema hapa nchini kuna makumbusho zinazomilikiwa na Serikali,wananchi,mashirika na jamii ambazo zimekuwa zikitembelewa na watu mbalimbali kuona vitu vya kale na kazi zinazofanyika.

Alisema makumbusho ya Viumbe iliyopo Arusha imetoa elimu na kuhamasisha  uanzishaji wa makumbusho za aina mbalimbali  kwa ajili ya kuhifadhi urithi wa taifa na kutoa elimu kama vyanzo vya mapato..

Akizungumzia kuhusu kuadhimisha kumbukizi hiyo Makumbusho ya Taifa  kupitia kituo chake cha Makumbusho ya Taifa ya Elimu Viumbe pamoja na mambo mengine wamejipanga kutoa elimu ya kuwajengea uelewa wananchi juu ya kutembelea makumbusho  kama sehemu ya kupata elimu na burdani kuhusu urithi wa nchi wa kale na wa Sasa wa Asili Mazingira, Utamaduni Sayansi, Teknolojia na Historia.

Dk. Ngereza alisema  makumbusho hiyo ilikuwa wazi hivyo kutoa fursa kwa wananchi kutembelea na  kupata elimu na mambo muhimu ambayo yanafanyika katika makumbusho hiyo. 

" Lengo la siku hii maalum ni kujenga uelewa kwa jamii kuhusu umuhimu wa Makumbusho katika Nyanja mbalimbali za maendeleo." alisema Ngereza.

Alisema katika kuadhimisha siku hiyo muhimu kila mwaka Jumuiya ya Kimakumbusho ya Dunia  (ICOM) huchagua mada katika kuadhimisha siku ya Makumbusho  Duniani ambayo ni agenda  muhimu katika jamii na kuwa Kauli Mbiu ya Maadhimisho hayo kwa  mwaka huu ni Nguvu ya Makumbusho. 


Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: