KATIBU Mtendaji wa Tume ya Madini nchini mhandisi Yahaya Samamba anatarajia kufanya ziara Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, jumatatu ya Mei 16 mwaka huu.


Afisa madini mkazi (RMO) wa mkoa wa kimadini wa Simanjiro, Fabian Mshai amesema Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini atakutana na wamiliki wa migodi, mameneja na wataalamu wa kulipua miamba ya migodi.

RMO Mshai amesema pamoja na kuzungumza na wadau hao wa madini pia atasikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wachimbaji madini.

Amesema kiongozi huyo akiwa na wasaidizi wake pia atawajazia uwezo zaidi kwa kutoa elimu ya uchimbaji na ufanyaji kazi salama ili kuepusha ajali migodini.

"Wamiliki wote wa migodi, mameneja na walipuzi wa migodi ya madini wa Mirerani, Mwajanga, Landanai, Nadonjuki, Kitwai na maeneo mengine wanakaribishwa kwenye kikao hicho.

Katibu wa chama cha wachimbaji madini Mkoa wa Manyara, Tariq Kibwe amewaasa wadau hao wa madini kujitokeza kwa wingi ili kukutana na kiongozi huyo ambaye pia atasikiliza kero za wachimbaji.

"Changamoto mbalimbali za kuhusu uchimbaji ambazo haziwezi kutatuliwa kwenye ngazi ya RMO zinapaswa kufikishwa kwake hivyo wajitokeze kwa wingi," amesema Kibwe.

Mmoja kati ya mameneja wa migodi ya madini ya Tanzanite, Rashid Mohamed amesema hiyo ni fursa nzuri kwao kukutana na kiongozi huyo mkubwa kwenye sekta ya madini.

"Tutashiriki kwa wingi kwenye kikao hicho kwa lengo la kujaziwa uwezo zaidi kwani RMO amesema tutapatiwa elimu juu ya masuala ya uchimbaji madini," amesema.
Share To:

Post A Comment: