Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha TLP, Augustino Mrema na mke wake Doreen Kimbi wakiwa katika ziara ya siku sita kwenye hifadhi nne za wanyama kwa ajili ya kukamilisha fungate yao ziara waliyoimaliza juzi.


Na Thobias Mwanakatwe, Moshi


MWENYEKITI wa Taifa wa Chama TLP, Augustino Mrema, ametoa wito kwa watanzania kuendelea kuimarisha ulinzi kwenye hifadhi zilizopo nchini kwa kushirikiana na vikosi vya ulinzi ili kuweza kukabiliana na tatizo la ujangili.

Alitoa wito huo wakati akizungumza katika mahojiano na waandishi wa habari jana baada ya kumaliza ziara yake ya siku sita kwenye hifadhi nne za wanyama akiwa na mke wake Doreen Kimbi kwa ajili ya kukamilisha fungate yao.

Mrema alisema pamoja na kwamba kumeimarishwa kwa vikosi vya ulinzi kwenye hifadhi lakini bado wananchi ambao vijiji vyao vipo karibu na hifadhi wana nafasi ya kusaidia ulinzi ili kumaliza tatizo la ujangili.

Aidha, Mrema aliwataka wananchi kujenga utamaduni wa kutembelea hifadhi za wanyama badala ya kidhani kuwa kazi hiyo ni kwa ajili ya wageni tu kutoka nje.

Alisema Watanzania wanapaswa kumuunga mkono rais Samia Suluhu Hassan ambaye amejipanga vizuri kwa ajili kutangaza vivutio vyetu vya utalii ndani na nje ya nchi kupitia filamu ya Safari Royal Tour kwa kutembelea mbuga  za wanyama.

"Nimekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani y Nchi, nimekuwa Waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana, nimekuwa Naibu Waziri Mkuu, nimekuwa mbunge Vunjo lakini sikuwahi kutembelea kwenye mbuga za wanyama  lakini kiukweli kuna mambo mazuri ya kujifunza unapopata fursa usikose kutembelea hifadhi zetu," alisema.

Naye mke wake Mrema, Doreen Kimbi, alisema katika mbuga za wanyama kuna vitu vingi vizuri vya kujifunza hivyo wananchi kila mwezi wewe wanapanga ratiba kutembelea hifadhi zetu.

Doreen alisema wazo la kufanya fungate kwenye hifadhi za wanyama alilitoa yeye na mume wake (Mrema) kulikubari haraka kwani hiyo ndio njia mojawapo ya kumuunga mkono rais Samia ambaye amekuwa akisisitiza umuhimu wa wananchi kutembelea hifadhi zetu zilizopo nchini.

Naye Afisa Uhifadhi Utalii wa Hifadhi ya Ziwa Manyara, Renard Twinzi, alisema katika kipindi cha kuanzia Julai 2021 hadi April 2022 hifadhi hiyo imetembelewa na watalii 57,485.

Alisema hifadhi hiyo kwa kushirikiana na wadau wengine wa utalii imeweka mikakati ya kuhamasisha utalii wa ndani ili kuweza kufikia malengo ya hifadhi kutembelewa na 100,000 kwa mwaka.

Mrema na mke wake katika ziara hiyo iliyopewa jins la Mr&Mrs Mrema Honeymoon tour’walitembelea hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Tarangire, Manyara na Ngorongoro 

Share To:

dottomwaibale

Post A Comment: