Na Ahmed Mahmoud Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amepiga marufuku utoaji holela wa miguu bandia bila ya kumpima mtu mwenye uhitaji. Marufuku hiyo ameitoa leo Machi 5, 2022 jijini Arusha alipokuwa anakabidhi vifaa vya huduma za utengamao vilivyopatikana kwa jitihada za Mbunge wa Arusha mjini Mhe. Mrisho Gambo pamoja na wadau mbalimbali vyenye thamani zaidi ya shilingi Milioni 300 kwa walemavu ikiwemo miguu bandia 117, viti mwendo 100, Kadi za Bima ya Afya 100 pamoja na fimbo za wasioona 30. Waziri Ummy amesema kama kuna mdau ameguswa na watu wenye ulemavu wenye mahitaji ya miguu bandia ni vyema akaenda kwa Mganga mkuu wa Mkoa au Halmashauri ili taratibu za kuwafikia walengwa zifuatwe na wapimwe ili kupata kiungo ambacho hakitamletea ulemavu mwingine. “Huduma za utengamao zinatolewa ili kumuwezesha mtu mwenye ulemavu aweze kumudu maisha kwa kutumia viungo alivyonavyo au vifaa saidizi”. Amesema Waziri Ummy. Aidha, amesema kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 ilibainisha kuwa, asilimia 5.8 ya sensa ya watanzania wote walikiwa na tatizo la ulemavu ambao wanaweza kuwa na uhitaji wa huduma ya utengamao. Waziri Ummy amesema Serikali imeboresha dodoso la sensa ya watu na makazi la mwaka 2022 ili kuweza kuwa na uwanda mkubwa wa kuweza kubainisha kiwango na aina ya ulemavu. Kwa upande wake Mbunge wa Arusha mjini Mhe. Mrisho Gambo ambae ameunganisha wadau mbalimbali hadi kupatikana kwa vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni 300 ametoa shukrani kwa Wizara ya Afya kwa kuunga mkono juhudi hizo pamoja na wadhamini wote waliofanikisha kufanyika kwa hafla hiyo.
Share To:

Arusha Newsroom

Post A Comment: