WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan Serikali imetenga sh bilioni 1.2 kwa ajili ya awamu ya kwanza ya mradi wa ujenzi wa nyumba za wananchi watakaokubali kwa hiari kuhama katika hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro.

 

Awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi huo inahusisha nyumba 103 ambazo zipo katika hatua mbalimbali. Ujenzi ulianza 28 Februari 28, 2022 na hadi kufikia Machi 12, 2022 ujenzi wake umefikia asilimia 78. Nyumba hizo zinajengwa katika kijiji cha Msomera Wilayani Handeni, Tanga.

 

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumapili, Machi 13, 2022) wakati akizungumza na wananchi katika kijiji cha Msomera kabla ya kukagua ujenzi wa nyumba hizo ambazo kati yake nyumba 53 zimepauliwa na hatua za umaliziaji inaendelea, nyumba 42 zipo hatua ya boma na nyumba 8 zipo katika hatua za ujenzi wa msingi. 

 

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amezitaka Wizara, Taasisi na Idara zote za Serikali zinazoshughulikia uhamaji wa hiari wa wakazi katika hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro kuendelea kushirikiana kwa karibu ili kukamilisha zoezi hilo kwa ufanisi.

 

Waziri Mkuu amesema kuwa wananchi hao waliokubali kuhama kwa hiari licha ya kupewa nyumba na eneo lenye ukubwa wa ekari tatu kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za ufugaji. Wananchi hao wanahama ili shughuli za uhifadhi ziendelee katika eneo hilo.

 

"Serikali itahakikisha haki zote za binadamu zinazingatiwa katika zoezi hilo la kuwahamisha kwa hiari wananchi wanaoishi kwenye hifadhi ya Ngorongoro kwenda katika maeneo mbalimbali watakayayoyachagua kikiwemo na kijiji hicho cha Msomera, ambapo tayari Serikali imeshapima viwanja 2,500 na kutenga eneo la ekari 1,700 Kwa ajili ya kilimo na malisho”.

 

Hata hivyo Waziri Mkuu amewaagiza viongozi wa  mkoa wa Tanga wakutane na viongozi wa wa kijiji na wananchi wa eneo hilo ili waendelee kuwaelimisha kuhusu zoezi hilo na umuhimu wake kwa maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.

 

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema kuwa eneo hilo wamekusudia liwe shamba darasa la ufugaji wa kisasa wenye tija kiuchumi ili kuwasaidia wafugaji nchini waweze kunufaika zaidi na ufugaji wanaoufanya tofauti na ilivyo sasa, hivyo amewaomba watoe ushirikiano kwa Serikali yao.

Naye, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Ridhiwani Kikwete ametumia fursa hiyo kuwaomba viongozi na wananchi wa Handeni wahakikishe wanasimamia vizuri mipango ya matumizi bora ya ardhi ili kuepusha migogoro ya ardhi. “Maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za ufugaji yalindwe na yatumike kama ilivyokusudiwa.”

 

Nao wakazi wa kijiji cha Msomera wamesema wapo tayari kuwapokea wakazi wa Ngorongoro watakaokubali kwa hiari kuhamia karika kijiji chao, pia wanashukuru kwa kuwa ujio wao utaenda sambamba na uboreshwaji wa miundombinu ya huduma mbalimbali za kijamii kama maji, afya na umeme.

Share To:

Post A Comment: