Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)  Mkoa wa Singida Mzalendo Widege (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari jana wakati akitoa taarifa ya kipindi cha  robo ya mwaka kuanzia Oktoba hadi Desemba 2021. Kulia ni Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Singida, Adamu Kilongozi.
Maafisa wa Takukuru Mkoa wa Singida, wakiwa kwenye mkutano huo wa utoaji taarifa. Kutoka kulia ni Tatu Shaurikesho, Gabriel Musuguri na Theopister Tembo.
Maafisa wa Takukuru, Dorcas Mkama na Hamisi Kidulani wakiwa kwenye mkutano huo.
Afisa wa Takukuru Monica Nyamagwira akiwa kwenye mkutano huo.
Muonekano wa Jengo la Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Singida.


Na Dotto Mwaibale, Singida


TAASISI ya Kuzia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida imekagua miradi yenye thamani ya Sh. 1.2 Bilioni ambayo imetekelezwa kwa mujibu wa fedha zilizopokelewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi husika ya maendeleo.

Hayo yamebainishwa jana na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Singida Mzalendo Widege wakati akitoa taarifa kwa waandishi wa habari ya kipindi cha kuanzia Oktoba hadi Desemba 2021.

Aliitaja miradi hiyo kuwa ni Afya ambao ulikuwa na thamani ya Sh. 250,000,000, maji miradi miwili yenye thamani ya Sh. ya Sh.960,651,113, Elimu mradi mmoja (bweni) wenye thamani ya Sh 80,000,000 jumla ya miradi yote ikiwa na thamani ya Sh. 1,290,651,113. 

Katika Dawati la Uchunguzi kwa  kipindi cha Okotoba hadi Desemba,2021 TAKUKURU Mkoa wa Singida waliweza kutekeleza majukumu yao ambapo jumla ya malamiko 101 yalipokelewa, taarifa 63 zilihusu vitendo vya rushwa na taarifa 38 hazikuhusu vitendo vya rushwa.

Alitaja malalamiko yaliyopokelewa kisekta ni TAMISEMI 44, Afya 14, Ardhi 13, Mahakama 08, Polisi 06, Elimu 04, Binafsi 03,Fedha 03, Kilimo 01, Manunuzi 01, Maliasili o1, Maji 01, Nishati 01, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii 01.

Alisema malalamiko 63 yalihusu rushwa uchunguzi wake unaendeleakatika hatua mbalimbali na malalamiko 38 ambayo yalibainika hayahusiani na rushwa walalamikaji walipewa ushauri na kuhamishiwa idara nyingine kwa hatua zaidi.

Widege alisema katika kipindi hicho jumla ya kesi tatu zilifunguliwa Mahakamani na kufanya jumla ya kesi zinazoendelea mahakamani kuwa 15 na kuwa katika kipindi hicho cha cha kati ya Oktoba na Desemba kesi sita zilitolewa uamuzi mahakamani na Jamhuri ilishinda katika kesi zote. 

Akizungumzia Dawati la Elimu kwa Umma, ili kuiwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika Mapambano Dhidi ya Rushwa TAKUKURU kupitia Dawati  la Elimu kwa Umma hutumia mbinu mbalimbali kuwaelimisha na kuwashirikisha wanajamii wa makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na vijana wa shule za Msingi,Sekondari na vyuo . Pia Ili kuwafikia na kuwaelimisha walengwa TAKUKURU inashirikiana na wadau wengine wa mapambano dhidi ya Rushwa ambao ni pamoja na Taasisi za dini, mashirika ya Umma, mashirika yasiyo ya serikali, asasi za kiraia na sekta binafsi. 

Alisema TAKUKURU mkoani hapa kwa kushirikiana na Chama cha Skauti Tanzania imefanikiwa kuanzisha umoja ujulikakao kwa jina la TAKUKURU-SKAUTI (TAKUSKA) ambapo walezi wa umoja huoni Wakuu wa wilaya kwa ngazi zote na mwongozo umetolewa wa mshikamano kati ya TAKUKURU na Skauti.

"Elimu kwa Umma ilitolewa kwa makundi mbali mbali katika jamii na pia katika kipindi tajwa ofisi iliendelea  kuelimisha umma juu ya madhara ya Rushwa  ambapo jumla ya mikutano ya Hadhara 22 imefanyika ,Semina 19 zimefanyika,  Klabu  za wapinga Rushwa 34 ziliimarishwa" alisema Widege. 

 Alisema katika Uzuiaji wa Vitendo vya Rushwa, Uimarishaji wa mifumo hufanyika kwa kufanya uchambuzi wa mifumo, kuweka mikakati ya Kudhibiti Mianya ya Rushwa na kufuatilia utekelezaji wa mikakati.  

Akizungumzia miradi ya maendeleo alisema mojawapo ya majukumu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ni kufuatilia matumizi ya rasilimali za umma (PETS) katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuwa ufuatiliaji huo unalenga kubainisha mianya ya rushwa, ucheleweshaji wa utekelezaji, uvujaji na ushirikishwaji wa wananchi. 

Widege alisema Mtiririko wa fedha hufuatiliwa kutoka chanzo (Hazina, wafadhili au vyanzo vya ndani) mpaka kwenye mradi husika ili kubaini kama kutakuwa na matumizi mabaya ya fedha hizo.

Alisema TAKUKURU huchukua hatua kadhaa zifaazo kulingana na kinachobainika katika ufuatiliaji, zikiwemo kushauri au kujadiliana na wadau kuhusu namna ya kuondoa upungufu uliobainika ili thamani ya fedha ifikiwe, kuelimisha wananchi na wadau, kufanya uchambuzi wa mifumo na kuanzisha uchunguzi. 

Alitaja baadhi ya mambo yaliyobainika wakati wa ukaguzi wa Miradi hiyo ni ukiukwaji wa taratibu za manunuzi kwenye baadhi ya miradi, kukosa ushirikiano wa nguvu za wananchi, ucheleweshaji wa fedha kwenye vituo kutoka Halmashauri na changamoto wakati wa utekelezaji wa Sheria Mpya inayoelekeza manunuzi ya vifaa kwa wazabuni waliosajiliwa  na GPSA ambao wengi wao gharama zao zipo juu na hivyo kusababisha miradi kutokamilika.

Alieleza hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kuanzisha uchunguzi, kutoa ushauri juu ya uboreshaji miradi na uelimishaji kwa wananchi na wadau ili washiriki vyema katika kusimamia miradi yao na kuzuia vitendo vya Rushwa pamoja  ushauri wa kurekebisha mradi ili ufikie malengo.

Akizungumzia TAKUKURU inayotembea alisema ilifika Chuo cha Uuguzi Kiomboi (KNTC) kilichopo Wilaya ya Iramba lengo la kuwaelimisha na kupokea kero mbalimbali kuhusu Rushwa.

Alisema kupitia uelimishaji huo walipokea malalamiko kwamba, baadhi ya Wanachuo wanafadhiliwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Uhifadhi wa Masomo kwa watoto wa kike wanaoishi katika mazingira magumu- CAMFED ambao walilalamika kuwa baada ya kuingiziwa fedha kiasi cha Sh.720,000 kinyume na utaratibu wa chuo pamoja na Shirika la CAMFED.

Alisema baada ya TAKUKURU kupitia sheria na taratibu za chuo ilibainikuwa wanachuo hao hawakutakiwa kufanya hivyo na iliamuliwa kila mwanafunzi aliyetoa fedha Sh.720,000 kwa uongozi wa chuo warudishiwe fedha hizo.

Aidha Widege alisema katika fedha zilizopelekwa na Serikali Mwezi Oktoba mwaka jana  mkoani humo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo walipofanya uchunguzi matumizi yake vilikuwepo vitendo vya rushwa vilivyojitokeza hivyo wameendelea na uelimishaji unaolenga kushirikisha jamii katika mapambano dhidi ya rushwa ikiwa ni pamoja na kuendelea kutekeleza Mpango Kazi wa TAKUSKA.

Alitaja mkakati wa utendaji kazi wa TAKUKURU mkoani hapa kwa robo ya tatu ya mwaka 2021/ 2022 inayoanzia Januari hadi Machi 2022  ni kuendelea kufanya uchunguzi kwa taarifa zote za vitendo vya Rushwa zitakazoibuliwa, kufanya uelimishaji kwa jamii kuhusiana na madhara ya Rushwa, ufuatiliaji wa kina katika miradi ya maendeleo ya maji, Afya, elimu,ujenzi wa miundombinu ya Barabara na watahakikisha wanafuatilia wakala wote yaani Tanroads na Tarura  kwa lengo la kuona uwiano wa fedha zilizotolewa na Serikali na kujikita katika kufuatilia mfumo mzima wa Force Akaunti ambao unatumika katika ujenzi wa majengo ya Serikalipamoja na kutekeleza Mpango Kazi wa TAKUSKA. 

TAKUKURU Mkoa wa Singida inazidi Kutoa rai kwa wananchi wote kwa ujumla kujiepusha na vitendo vya Rushwa na kushiriki kikamilifu kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kwa kufika Ofisi zetu za Mkoa na Wilaya , kupiga simu namba 113  au kumpigia Mkuu wa TakukuRu Mkoa wa Singida Namba 0738150208 .Pia  kutoa ushirikiano kwenye uchunguzi na kushiriki kutoa ushahidi Mahakamani. 

Aidha TAKUKURU Mkoa wa Singida inawatahadharisha wale wote wanaowatapeli au wanaopangakuwatepeli wananchi kwa kujifanya Maafisa wa TAKUKURU au vyombo vingine vya dola kuacha kwa sababu watakaobainika hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kuwafikisha Mahakamani.

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: