Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma (NTLP) kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la KNCV, wamezindua utafiti wa mradi wa kutumia digitali wezeshi kwa kumsaidia mgonjwa kufuasa matibabu ya TB katika kipindi chote cha tiba. Mradi huu unalenga kuchangia jitihada za kupunguza maambukizi na vifo vitokanavyo na TB. 


Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa mradi huo, Meneja wa Mpango wa Taifa wa kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma kutoka Wizara ya Afya  Dkt. Riziki Kisonga ambaye alimuwakilisha Katibu Mkuu, alisema mradi huo unatekelezwa katika vituo 72 vya kutolea tiba katika Mikoa ya Arusha, Geita, Manyara na Mwanza. 


Alisema kutokana na ugonjwa huo kuongoza kuua watu wengi duniani ukitanguliwa na Uviko-19, inakadiriwa kusababisha vifo vya watu milioni 1.5 duniani kote. 


"Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani(WHO),kwa mwaka 2019  watu 32,000 kati ya 81,208 waliougua TB walifariki dunia kutokana na ugonjwa huo".


Dkt. Kisonga alisema vifo  vitokananvyo na TB vinaweza kuzuilika kama  vitaweza kugundulika mapema, kukamilisha matibabu sahihi kwa wakati kwani ufuasi mzuri wa dawa ni muhimu katika kuleta utendaji kazi na matokeo mazuri ya dawa kwani kwa ufuasi mbaya wa dawa za TB hupunguza ufanisi wa dawa kwa asilimia 50 mpaka 80  na matokeo mazuri ya matibabu ya TB yanatokana na kumaliza kikamilifu.


Akiwasilisha namna mradi huo unavyoenda kutekelezwa, Meneja wa Mradi wa Ascent, Dkt. Baraka Onjare, amesema kuwa, mradi huo unalenga kuchangia jitihada zilizopo kwa kupungiza maambukizi na vifo vitokananvyo na TB kwa kutumia visanduku maalumu vya dawa zilizounganishwa kidigitali na mfumo maalumu wa kompyuta kufuatilia mwenendo wa ufanisi wa dawa.


Amesema ikiwa mfumo huo humkumbusha mgonjwa kunywa dawa sambamba na kumpa taarifa mtoa huduma kufanya ufuatiliaji na msaada wa karibu juu ya mwenendo wa umezaji wa dawa wa wagonjwa.






Share To:

Post A Comment: