Na 
 Charles James, 


KUELEKEA Siku ya Wanawake Duniani ambayo hufanyika kila Mwaka Machi 8, Katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Dodoma Mjini, Diana Madukwa amesema umoja huo utaendelea kuwaandaa wasichana na wanawake ili kushika nafasi mbalimbali za kiuongozi.

Madukwa pia amempongeza Rais Dk John Magufuli kwa namna ambavyo ameendelea kuwaamini wanawake katika nafasi mbalimbali kubwa za kiuongozi na kimaamuzi kwenye Serikali yake ikiwemo kuwa na Makamu wa Rais wa kwanza Mwanamke tokea historia ya Tanzania.

Amesema UWT Wilaya ya Dodoma Mjini imekua ikiandaa Mafunzo na semina mbalimbali za kuwajengea wanawake na wasichana uwezo wa kujiamini kwamba wao wanaweza na siyo lazima awepo mtu mwingine wa kuwasukuma.

" Sisi kama UWT Wilaya mara kwa mara tunaandaa mafunzo na lengo lake ni kuwaambia wanawake na wasichana kutokukaa nyuma na kusubiri kufanyiwa maamuzi, wajiamini na kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za kiuongozi kuanzia kwenye Chama na sehemu nyingine.

" Mafunzo yetu yamekua yakijikita zaidi katika kuwajengea uwezo wa kupata uongozi bila kutoa rushwa ikiwemo ya Ngono, tunawajengea uwezo wa kuongoza, uwezo wa kujiendesha kiuchumi, kisiasa na kijamii," Amesema Diana Madukwa.

Amempongeza Rais Dk Magufuli kwa kuendelea kuwaamini wanawake katika nafasi mbalimbali kwenye serikali jambo ambalo limetoa ari na motisha kwa wasichana wengi zaidi kujikita kwenye siasa na kuona inawezekana kuwa sehemu ya uongozi wa Nchi yao.

" Nimpongeze na kumshukuru sana Rais wetu Dk Magufuli ameendelea kuwaamini wanawake kwenye nafasi kubwa na nyeti, pamoja na kuwa na Makamu wa Rais Mwanamke ambaye ni Mama Samia Suluhu Hassan pia tumeona idadi kubwa tu ya Mawaziri Wanawake, Wakuu wa Mikoa Wanawake na hata kwenye Majeshi yetu, tumeona Mkuu wa Idara ya Uhamiaji pia ni Mwanamke, tumpongeze Rais kwa hilo," Amesema Diana Madukwa.

Amesema UWT Wilaya ya Dodoma itaendelea kutoa elimu na mafunzo ya kuwawezesha wanawake kujiamini zaidi na kuingia kwenye ushindani wa nafasi za kiuongozi.

Share To:

Post A Comment: