Afisa wa Shirika lisilo la Kiserikali  la Sustanable Environment Management Action (SEMA) la Mkoa wa Singida, Witness Andersoon  (kushoto) akitoa elimu kwa wananchi na wafanyabiashara wa Soko  la Vitunguu la Kimataifa la Manispaa ya Singida  namna ya kujikinga dhidi ya mlipuko wa ugonjwa wa corona mkoani hapa jana.
 Maafisa  wa Shirika hilo, wakitoa  elimu kwa njia ya mabango. 
 Elimu ikitolewa Stendi Kuu ya Mabasi.
 Msafiri akitoa maoni yake kwa mwanahabari kuhusu ugonjwa wa Corona.
  Elimu ikitolewa kwa Mama Lishe.
  Elimu ikitolewa katika vituo vya bodaboda.
 Elimu ikitolewa katika vituo vya kuuza mafuta.
 Elimu ikitolewa kwa madereva barabarani.
 Elimu ikitolewa kwa madereva barabarani.

Elimu ikitolewa kwa madereva wa Bajaj.




Na Dotto Mwaibale, Singida

MAAFISA wa Shirika lisilokuwa la Kiserikali  la Sustanable Environment Management Action  (SEMA) Mkoa wa Singida wamepita mtaa kwa mtaa mjini hapa kutoa elimu kwa wananchi  juu ya namna ya kujikinga na Virusi vya Covid 19 vinavyo sababisha Ugonjwa wa Corona

Shirika hilo linatoa Elimu hiyo kwa ufadhili wa Shirika la Stromme East Africa Foundation lenye Makao Makuu Kampala nchini  Uganda huku ufadhili mkuu wa mashirika hayo ukitolewa na Shirika la Stromme Foundation la Norway kupitia Mradi wa uwezeshaji Jamii kiuchumi uliolenga vijana wakiume, wa kike, watoto na wakina mama.

Akizungumza wakati wa utoaji wa Elimu hiyo kwenye eneo la Soko Kuu la Manispaa ya Singida jana Ofisa Mradi kutoka Shirika la SEMA Renard Mwasambili amesema program wanayoitekeleza ni utoaji Elimu ya namna ya unawaji Mikono, utoaji wa Vifaa sambamba na elimu ya utengenezaji wa vifaa vya kujikinga na Virusi vya Covid 19 vinavyo sababisha Ugonjwa wa Corona.

"Lengo la Elimu hii ambayo tunaifanya ni kutembelea maeneo mbalimbali yenye mikusanyiko ya watu na kutoa elimu kwa mtu mmoja mmoja,makundi na wafanyabiashara namna ya kujikinga dhidi ya Ugonjwa huu."alisema Mwasambili.

Alisema kwamba programu hiyo imewashirikisha pia maafisa wa wa Shirrika la Empower Youth Prosperity (EYP)  kutoka mkoani Mbeya na kuongeza kuwa Kila mtanzania mahali alipo anapaswa kuchukua tahadhari na kamwe asipuuze ushauri wa kitaalamu unaoendelea kutolewa na Serikali pamoja na wataalamu wa afya.

Mwezeshaji wa Mradi kutoka shirika hilo, Witness Anderson alisema homa kali ya mapafu inayosababisha Virusi vya Corona ni Ugonjwa unaoambukizwa kwa kuingiawa na maji maji yatokayo kwenye njia ya hewa wakati mtu mwenye Ugonjwa huo anapokohoa ama kupiga chafya.


Alitaja njia nyingine ya maambukizi ni kwa kugusa maji maji yanayotoka puani (kamasi),kugusa kitambaa au nguo zilizotumiwa na mtu mwenye maambukizi ya Ugonjwa huo au maeneo mengine yaliyoguswa na mtu mwenye Virusi vya Corona.

Akielezea jinsi ya kujikinga na ugonjwa huo alitoa tahadhari ya watu kukaa mbali angalau mita moja au mbili jambo litakalosaidia kujiepusha na maambukizi iwapo mmoja kati ya watu hao atakuwa na maambukizi.

Alisema tahadhari nyingine inayopaswa kuchukuliwa ni kufunika mdomo na pua wakati wa kukohoa kwa kutumia kitambaa safi au sehemu ya mbele ya kiwiko cha mkono,kuepuka kugusana na mtu mwenye dalili za ugonjwa huo, kusalimiana kwa kushikana mikono,kukumbatia na kubusiana.

"Safisha mikono yako mara kwa mara kwa maji tiririka kwa kutumia sabuni au dawa ya kutakasa mikono na baada ya kunawa epuka kugusa macho,pua au mdomo na nguo badala yake jifute kwa kutumia tishu ambayo itatupwa sehemu salama baada ya kutumika."alisema Anderson.

Baadhi ya maeneo ambayo shirika hilo limetoa elimu hiyo mkoani hapa ni pamoja na eneo la Soko Kuu la Manispaa ya Singida, Soko Kuu la kimataifa la Vitunguu, Kituo kikuu cha mabasi,vituo vya bajaji, bodaboda, vituo vya kuuza mafuta,  mama lishe, barabarani ambapo pia kuanzia kesho watakwenda kutoa elimu hiyo katika wilaya za Iramba, Manyoni, Ikungi, Singida DC.

Share To:

Post A Comment: