Jamhuri ya Watu wa Finland imesema itaendelea kuisaidia Tanzania katika sekta ya Elimu kwenye eneo la ubunifu ili kuhakikisha vijana wanakuwa wabunifu ili kuweza kujiajiri pindi wanapomaliza masomo.
Kauli hiyo imetolewa na Balozi wa Jamhuri ya watu wa Finland nchini Tanzania Pekka Hukka wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako katika ofisi ndogo za Wizara zilizopo jijini Dar es Saalam kuhusiana na namna bora ya utekelezaji wa awamu ya pili ya programme ya ubunifu inayotekelezwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia(COSTECH).
Waziri Ndalichako amesema atahakikisha Wizara yake inasimamia kwa karibu utekelezaji wa programu hiyo ili kuhakikisha malengo ya programu yanafikiwa.
Waziri Ndalichako amesema Serikali inatambua msaada ambao umekuwa ukitolewa na Finland katika sekta mbalimbali nchini ikiwemo sekta ya Elimu na kuahidi kuwa fedha zitakazotolewa zitatumika kama zilivyokusudiwa.
Programu hiyo ya miaka mitano inatarajiwa kuanza 2018 na kukamilika 2022.
Imeandaliwa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
7/12/2017
Post A Comment: