Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Nape Moses Nnauye ameahidi kutoa shilingi laki tano kwa kila goli litakalofungwa na timu ya Serengeti Boys katika mchezo wa kuwania kufuzu fainali za Kombe la mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17 utakaofanyika kesho katika Uwanja wa Taifa dhidi ya Congo-Brazzaville.

Akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam Nape amesema milango ipo wazi kwa wadau wengine wa michezo kujitolea katika kuiwezesha timu na hivyo kufanya vizuri katika mechi hii ambayo ni muhimu sana kushinda ili kufuzu kwa fainali hizo.

“Hii timu ni yetu sote hivyo inahitajika tuimiliki, tuepe nguvu, tuiombee ili iweze kufanya vizuri na hatimaye kufuzu kuingia fainali kwa kuitoa timu ya Congo-Brazzaville” amesema Nape.

Ameongeza kuwa kesho asubuhi atakutana na wachezaji wa timu hiyo ili kuwapa maneno ya faraja kabla ya kuanza kwa mechi na kuwataka watanzania kujitokeza kwa wingi uwanjani ili kuwapa motisha wachezaji kwa kuwashangilia na kuwatia moyo.

Mbali na hayo Waziri Nape ametoa ufafanuzi kuhusu matumizi ya kadi za kieletroniki zilizozinduliwa hivi karibuni kwa kueleza kuwa kadi hizo bado hazijaanza kutumika rasmi ili zitaanza kutumiwa katika mchezo baina ya Wabunge wa Simba na Yanga pamoja na Bongo Fleva.

Timu ya Serengeti Boys inaundwa na vijana wa Kitanzania wenye umri chini ya miaka 17 ambapo katika mchezo wa kesho watahitaji ushindi na baadaye kufanya mechi ya marudiano mnamo Oktoba 2 mwaka huu nchini Congo-Brazzaville.


www.msumbanews.blogspot.com

 

Share To:

msumbanews

Post A Comment: