Mwandishi wetu,Arusha 


Mkuu wa wilaya ya Arusha,Said Mtanda anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa siku ya wahudumu ambayo inataraji kuzinduliwa Machi 28 mwaka huu.


Katika uzinduzi huo unaotaraji kufanyika eneo la Cocoriko Club Lounge Kijenge  baadhi ya wahudumu wa hoteli,migahawa na baa mbalimbali mkoani Arusha wanataraji kujumuika na kueleza changamoto mbalimbali zinazowakabili makazini.


Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa Mkurugenzi wa Cocoriko Club,John Mdenye alisema kwamba uongozi wao kwa kutambua umuhimu na mchango wa wahudumu wameamua kuwakutanisha kwa pamoja.


Mdenye alisema kwamba wahudumu wengi hawapati fursa ya kujumuika na kufurahi pamoja hivyo wameamua kuwapa siku yao kila jumatatu ya wiki ambapo watakuwa wakikutana na kupata burudani.


"Sisi kama uongozi wa Cocoriko Club tunatambua mchango wa kundi la wahudumu na ndio maana tumeona tuwape siku yao moja ya kukutana na kufurahi" alisema Mdenye 



Hatahivyo,alisema kwamba wahudumu wengi wanajituma kutoa huduma kwa watu mbalimbali wawapo kwenye burudani lakini wao hawakumbukwi na kuitaka jamii sasa kubadili mtazamo.


Alisisitiza kwamba wahudumu wa vyakula na vinywaji mkoani Arusha na maeneo ya jirani watajumuika kwa pamoja na kupata burudani ya nyimbo pamoja na kubadilishana mawazo sanjari na kueleza changamoto zinazowakabili makazini.


"Tunaamini siku hiyo na wao watapumzika na kuhudumiwa badala ya kuhudumu tu kila mara sisi tunapokuwa kwenye burudani" alisisitiza Mdenye 


Hatahivyo,alibainisha kwamba wanataraji siku hiyo itapanuka kutoka ngazi ya mkoa mpaka kitaifa ambapo itawakutanisha wahudumu kutoka mikoa mbalimbali.

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: