Mbunge wa Kisesa, Mhe. Luhaga Mpina akiuliza swali la nyongeza bungeni Dodoma leo Novemba 3, 2021 kuhusiana na kupandishwa hadhi barabara ya Bariadi- Mwaukoli- Mwandu Itinje- Itinje- Kabondo- Mwabuzo hadi Igunga Tabora ambapo Serikali imekubali kufanya tathmini ya haraka ya barabara hiyo.

DODOMA

MBUNGE wa Jimbo la Kisesa, Mhe. Luhaga Joelson Mpina amehoji bungeni kuwa ni lini Serikali itaipandisha hadhi barabara ya kutoka Bariadi – Mwaukoli - Mwandu Itinje – Itinje – Kabondo -Mwabuzo hadi Igunga kuwa ya Mkoa baada ya TARURA kushindwa kuihudumia kutokana na ufinyu wa bajeti.

Akiuliza Swali la nyongeza bungeni Dodoma leo Novemba 3, 2021, Mhe. Mpina ametaka kujua mapendekezo yaliyowasilishwa serikalini kuhusiana na upandishaji wa barabara hiyo yaanza kutekelezwa lini ili kuwaondolea adha ya usafiri wananchi wanaotumia barabara hiyo muhimu kiuchumi inayounganisha Mkoa wa Simiyu na Mkoa wa Tabora.

“Asante  sana Mh Spika kwa nafasi hii kwa kuwa barabara ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Meatu, Mhe Leah Komanya ni barabara ambayo pia inaungana na barabara ya kutoka pale Mwabuzo ikaenda Kabondo, Itinje, Mwandu Itinje mpaka Mwaukoli na inaunganisha zote hizi inatoka Bariadi nyingine inatoka Meatu zinaenda zote Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Igunga sasa kwa sababu mapendekezo haya yote tuliyapeleka kwa pamoja kama ambavyo Naibu Waziri wa Ujenzi amejibu sasa anaweza kunihakikishia kwamba haya maombi yote yanafanyiwa kazi kwa pamoja na muda mfupi ujenzi utaanza wa mabarabara haya yatakuwa ya mkoa na baadae ujenzi kuanza mara moja ili kuondoa changamoto zilizopo kwa sasa za kutokana na Tarura kushindwa kumudu kukidhi mahitaji yake”amesema Mhe. Mpina

Akijibu swali hilo katika kipindi cha maswali na majibu bungeni Dodoma leo Novemba 3, 2021, Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Mwita Waitara amemuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Simiyu kufanya tathmini haraka ya barabara hiyo na kuwasilisha wizarani majibu ili Serikali ianze mara moja ujenzi wa barabara hiyo.

“Mheshimiwa Spika naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa  Mpina kama ifuatavyo naomba nitumie Bunge lako tukufu Mheshimiwa Spika kumuagiza Meneja wa Mkoa wa Simiyu, Shinyanga na Mwanza na maeneo yote ambayo waheshimiwa wabunge wameshaleta mapendekezo katika maeneo haya wafanye kazi ya tathmini haraka iwezekanavyo wawasilishe majibu wizarani na sisi kama Serikali tuweze kuchukua hatua ili maeneo hayo yaweze kutengenezwa kwa haraka wananchi waweze kupata huduma ya barabara” amesema Mh. Naibu Waziri wa Ujenzi Waitara.

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: