Muonekano
wa sehemu ya uanzishwaji wa barabara mpya ya Mwandiga hadi Mwamgongo
mkoani Kigoma inayokadiriwa kuwa na urefu wa kilometa 65 baada ya
kukamilika kwake. PICHA NA WUU
Mbunge
wa Jimbo la Kigoma Kaskazini Asa Makanika, akimuelezea jambo Naibu
Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, wakati Naibu
waziri huyo akikagua mradi wa uanzishwaji wa barabara mpya ya Mwandiga
hadi Mwamgongo mkoani Kigoma inayokadiriwa kuwa na urefu wa kilometa 65
baada ya kukamilika kwake.
Meneja
wa Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Kigoma, Mhandisi Narcis Choma,
akitoa maelezo ya ujenzi wa daraja dogo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi na
Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, katika mradi wa uanzishwaji wa
barabara mpya ya Mwandiga hadi Mwamgongo mkoani Kigoma inayokadiriwa
kuwa na urefu wa kilometa 65 baada ya kukamilika kwake. Kulia ni Mbunge
wa Jimbo la Kigoma Kaskazini Asa Makanika.
Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya, akitoa
maelekezo kwa Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Kigoma,
Mhandisi Narcis Choma (kushoto), wakati akikagua ujenzi wa daraja dogo
katika mradi wa uanzishwaji wa barabara mpya ya Mwandiga hadi Mwamgongo
mkoani Kigoma inayokadiriwa kuwa na urefu wa kilometa 65 baada ya
kukamilika kwake. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini Asa
Makanika.
Imeelezwa kuwa Serikali imeanza ujenzi wa barabara ya Mwandiga- Chankere
- Mwamgongo (Km 65) kwa kiwango cha changarawe ili kurahisisha huduma
za usafiri na usafirishaji kwa wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini na
mikoa jirani kwa ujumla.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa
Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, wakati wa ziara yake
mkoani Kigoma alipokuwa akikagua barabara hiyo.
Kasekenya,
amesema kuwa nia ya Serikali ni kuifungua barabara hiyo na kuikamilisha
kwa kiwango cha changarawe ambapo imekuwa ikitenga fedha mbalimbali kwa
ajili ya ujenzi wa barabara hiyo.
"Nimefika na nimejionea
mwenyewe na sasa ni utekelezaji zaidi, niwahakikishie wananchi wa Kigoma
Kaskazini kuwa Serikali ipo kazini na barabara hii itaendelea kutengewa
fedha kila mwaka ili kuhakikisha inakamilika", amesema Kasekenya.
Amemtaka
Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Kigoma,
Mhandisi Narcis Choma, Kuhakikisha ujenzi wa barabara hiyo unafika
hadi Kagunga na ipitike wakati wote, pamoja na kuhakikisha kuwa
anaweka zege kwenye maeneo yenye miinuko mikubwa sana na kuweka
makalvati mengi na imara kwenye maeneo yenye maporomoko ya maji.
Kwa
upande wake, Mbunge wa jimbo la Kigoma Kaskazini, Mheshimiwa Asa
Makanika, amesema kuwa Barabara hiyo ni muhimu kwani ni mkombozi kwa
watu wa Kigoma Kaskazini na pia itarahisisha huduma za usafiri na
usafirishaji hususan katika kata za Ziwani, Mugongo na Kagunga.
"Tunategemea barabara hii kuwa mkombozi kwa wananchi wa huku, kwani kwa
sasa wananchi wengi hutumia usafiri wa majini kufuata huduma muhimu
kama za kiafya na elimu na wanatumia masaa Saba kufika mjini, naamini
kujengwa kwa barabara hii kutakuwa ni kicheko kwa wananchi wangu,
amesema Mheshimiwa Makanika.
Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara
Tanzania (TANROADS) mkoa wa Kigoma, Mhandisi Narcis Choma, amesema kuwa
mpango uliopo sasa ni kuweka uzio pembeni ili kuzuia magari kuanguka
hasa kwenye miinuko mikali.
Ameongeza kuwa tangu mwaka wa fedha
2018 /2019 Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa
barabara hiyo kwa kwa kiwango cha changarawe na kufafanua kuwa mpaka
sasa eneo la kilometa nane la mlima limeshakatwa na linapitika.
Post A Comment: